Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri pamoja na timu yake yote kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na hotuba iliyojaa matumaini ya kuendeleza wakulima na hatimaye kuvuna mazao yenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kahawa ni zao kuu la biashara ambalo linaingiza pesa za kigeni, lakini zao hili sasa hivi ni zao ambalo haliangaliwi wala halina tija tena. Hivyo basi niishauri Serikali yangu ipeleke miche ya kutosha ya kahawa ili kuweza kufufua zao hili na pia zipelekwe pembejeo pamoja na zana zote zinazohitajika katika kilimo hicho. Pamoja na hayo Serikali ihakikishe inawapa miche bure kuisimamia kwa karibu. Pia Serikali inatakiwa itafute masoko ili mkulima huyu aweze kupata bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyojua zao la kahawa lina hatua nyingi, mpaka kufikia kuvuna na kuuza inakuwa imegharimu pesa nyingi. Kwa hiyo, bila kutafuta soko zuri wakulima hawa watakata tamaa na kuacha kabisa kulima zao hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto ilikuwa inatoa zaidi ya tani 300,000 lakini zao hili limeshuka. Kwa sasa huwezi kupata hata tani 50 kwa msimu na bado uzalishaji unazidi kushuka. Yote haya yanasababishwa na kushuka kwa bei ya zao hilo na wakulima kuacha kahawa ife yenyewe mashambani. Pia mibuni mingi ni ya zamani kwa hiyo imezeeka na kufa na kuzaa mazao kidogo sana. Hivyo basi kuna uhitaji mkubwa sana wa kupeleka miche ya kutosha katika Wilaya ya Lushoto ili kufufua zao hili ambalo ndilo mkombozi wa wananchi wa Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto ni Wilaya ya wakulima wa mboga mboga na matunda na katika Halmashauri ya Lushoto mapato mengi yanatoka huko. Hivyo basi ipo haja kubwa ya kuwaangalia wakulima hawa ili nao waweze kupata pembejeo au kuwapunguzia bei ya dawa kwani wakulima wananunua dawa kwa bei ya juu sana na ukizingatia magonjwa ya mboga mboga yanaongezeka kila kukicha hasa huu ugonjwa wa kantangaze unasumbua sana wakulima hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mkulima aweze kulima kwa uhakika kama Ilani ya Chama chetu inavyosema, kwamba kilimo ndio uti wa mgongo, ni lazima tuwaandalie wakulima wetu mazingira ya kila hitaji.

Kwanza, lazima kujengwe mabwawa ya kutosha kila kijiji ili waweze kulima kilimo cha umwagiliaji; pili, lazima wapate zana za kilimo kwa wakati; tatu, pia lazima watengenezewe miundombinu ya barabara ili wasafirishe mazao yao kwa wakati na nne, kuwapatia pembejeo za wakati. Yakizingatiwa yote haya naamini yatatimiza ndoto yetu ya kuelekea kwenye uchumi wa viwanda na viwanda vyetu kupata malighafi katika mazao yetu haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala la kurudisha vyama vya ushirika. Hili suala litakuwa ni gumu sana kusimamia kwani ushirika hawa ndio waliotufikisha hapa tulipo na ushirika hawa wana madeni makubwa sana na imefikia hatua benki zimefilisi baadhi ya mali za vyama hivyo. Leo hii mnataka ndio wanunue mazao ya kulima, hili ni suala ambalo wakulima wamelikataa, kuuza mazao yao katika vyama hivyo. Suala hili lingewezekana kama Serikali ingejenga imani kwanza kwa wakulima na kwa kutoa elimu mpaka hapo wananchi watakapoelewa. Lakini zaidi ya hapo naamini zoezi hili halitafanikiwa na Serikali itazidi kupoteza fedha bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kilimo cha katani katika Mkoa wa Tanga, zao hili la katani ni zao ambalo kwa sasa lina soko zuri, lakini lina changamoto nyingi. Hivyo basi niiombe Serikali iliangalie zao la katani kwa jicho la huruma kwani zao hili tayari lipo vizuri sasa na litaingiza fedha za kigeni, pamoja na soko la ndani lipo kwa kufufua viwanda vyetu vya magunia, kwa hiyo, Serikali ipeleke vifaa vya kilimo katika zao hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali iunde vikundi vya vijana na kuviwezesha mitaji na kuwawekea miundombinu wezeshi ili vijana hawa waweze kulima katika vikundi. Hii itatoa fursa ya vijana kujiajiri na kuacha kukaa vijiweni. Pamoja na hayo niishauri Serikali ianzishe benki za kilimo katika kila mkoa kwani hii itarahisisha wakulima wetu kupata mikopo kwa wakati na bila kwenda mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.