Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa dakika tano hizi kwangu ni chache sana lakini nitajitahidi niweze kuwasilisha ujumbe wangu. Uchumi wa Taifa kwa ujumla wake unategemea sana uchumi wa mtu mmoja mmoja na Wizara hii ya Uvuvi na Mifugo ni Wizara muhimu sana specifically kwenye eneo la uvuvi linachangia asilimia 2.2 ya pato la Taifa, lakini sioni kama Taifa tunaweka umuhimu kwenye uvuvi na mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa napitia, kwa mfano nilipitia mwongozo wa maandilizi ya mpango wa bajeti 2018/2019, sioni eneo lolote ambalo mpango huu unagusa eneo la uvuvi, kidogo imenisikitisha sana. Hata hivyo, uvuvi kwa ujumla wake kwa mfano kwenye eneo la Kanda la Ziwa ni siasa, ni maisha na ni kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikiongelea kwa mfano operesheni sangara, Mheshimiwa Kanyasu ameongea vizuri sana kinachofanyika kwenye Kanda ya Ziwa hususani operesheni sangara ni unyanyasaji, ni uonevu, ni dhuluma, inafanyika dhidi ya wavuvi. Matendo wanayofanyiwa si mambo ambayo yanapaswa kuendekezwa wala kuyakubali katika Taifa hili. Watu wanafilisiwa, wanapoteza maisha wanafanyiwa vitendo vya ajabu sana ambavyo vinatia simanzi na huzuni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukizingatia kwamba hii Sekta ya Uvuvi, kwa mfano, watu takribani milioni nne wanategemea uvuvi na implication yake ni nini hata wale wanaotegemea watu hawa zaidi ya watu milioni tano, milioni kumi wanategemea sekta hii ya Uvuvi. Kwa hiyo, unapovuruga Sekta hii ya Uvuvi wananchi zaidi ya milioni kumi ambao ni zaidi ya asilimia 20 ya wananchi wa Taifa hili wanaathirika na mambo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende moja kwa moja kwenye ushauri kwa sababu hatuwezi kuendelea kufanya haya wananchi wanaathirika, leo asubuhi tumeahirisha Bunge hapa na toka nje napigiwa na wavuvi kutoka Ukerewe. Kwa sababu Operesheni Sangara sasa kuna watu ama ni wahuni tu au namna gani wanatumia njia hii kuwabughudhi watu kule. Wameenda kule kwa sababu walichomewa nyavu zao wametafuta rasilimali pesa wakanunua nyavu nyingine zinazotakiwa, wameenda watu tena leo wanataka kuwachomea zile nyavu kwamba siyo halali, sasa maisha gani watu wataishi katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niende tu kwenye ushauri; la kwanza nimepitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, lakini sijaona sehemu yoyote ambayo kuna eneo la mafunzo kwa wavuvi wetu, kwa sababu haiwezekani kwenda kuwaadhibu tu wavuvi hata kama ni mtoto huwezi kwenda kumuadhibu kabla ya kumwonesha ni kitu gani anapaswa afanye. Sasa tunatakiwa tutoe elimu kwa wavuvi wetu, tujue kwamba hawa ni wavuvi na shughuli zao ni uvuvi. Sasa ni uvuvi gani sasa wanatakiwa waufanye, ni wajibu wetu kama Serikali kutoa elimu hii lakini kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri sijaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili kuna marekebisho ya sheria namba 22 ya mwaka 2003, kwenye hotuba wameonyesha iko kwenye mchakato, kwenye hatua nzuri, lakini je, sheria hii wakati wa kufanya marekebisho wadau wameshirikishwa kwa kiasi gani. Kwa sababu moja kati ya malalamiko ni kwamba tumekuwa tunatunga sheria na kufanya marekebisho, lakini hatuwahusishi wadau kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo ni kwamba, tunatunga sheria za upande mmoja bila wadau kushiriki na kutoa changamoto na mtazamo wao juu ya yale ambayo tunayatunga. Kwa hiyo, niombe kwamba sheria hii au marekebisho haya yatakapokuwa yanaletwa tujiridhishe kwamba wadau hasa wavuvi wameshirikishwa katika mabadiliko ya sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri mwingine ni juu ya nyavu. Tumezuia nyavu hizi walizokuwa wanatumia kwamba ni nyavu haramu, sasa hizi nyavu zinazopaswa kutumika ziko wapi? Kwa sababu wavuvi hawana nyavu hizi, wale ambao walikuwa wanaagiza nyavu hizi wamezuiliwa kuingiza nyavu hizi, sasa nini kitakachotumika na wale waliopewa jukumu ya kutengeneza nyavu hizi walikuwa wanatengeneza vyandarua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nyavu zinazotumika sasa hivi kwa mfano za dagaa watu wanatumia ndani ya mwezi mmoja nyavu zile zimeharibika, inabidi wanunue nyavu nyingine, ni gharama kubwa kwa wavuvi wetu hawa ambao kwanza tumewatia umaskini kwa kuwachomea nyavu zao, halafu inabidi watafute rasilimali pesa nyingine kununua nyavu nyingine. Kwa hiyo, kama hatuna uwezo wa kuzalisha nyavu hapa nchini turuhusu nyavu kutoka nje ziweze kuingizwa nchini ili wavuvi waweze kufanya shughuli zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwa Mheshimiwa Waziri niombe, wadau wangu Ukerewe sisi tunavua samaki aina nyingi. Kuna samaki aina ya gogogo kwetu maarufu kama ngere ni samaki maalum na muhimu sana wanavuliwa kwa msimu, watuambie wanavuliwa kwa nyavu size gani na wale wanapatikana kwa msimu. Msimu wake ni kuanzia mwezi huu kuendelea mpaka mwezi wa Nane.

Mheshimiwa Naibu Spika, watafiti wa Mheshimiwa Waziri inawezekana hawajui kwamba samaki hawa wanapatikana kwa msimu, lakini wale wanatakiwa sasa ndio waanze kuvuliwa. Kwa hiyo, tunaomba sasa watuambie tunavua kwa nyavu size gani ili wananchi waweze kupata, lakiniā€¦(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)