Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Niende moja kwa moja kwenye Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi hasa katika Sekta ya Mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa kila nikipata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii, kilio changu ni kuhusiana na suala zima la mazingira wezeshi, mazingira ambayo yanaweza kuwafanya wafugaji wafanye shughuli zao na hii nikiwa na maana kwamba Serikali imefanya maamuzi ya kupeleka mifugo Mkoa wa Lindi na hasa Wilaya ya Kilwa, lakini mpaka hivi ninavyozungumza hakuna chochote kimefanyika kuhusiana na miundiombinu ambayo ingeweza au itaweza kuwasaidia wafugaji wale kufanya shughuli zao ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mapori yote ya Kilwa sasa yamevamiwa na mifugo, lakini hakuna bwawa, hakuna josho kwa hiyo wafugaji wale wanafanya shughuli zao kiholela. Nichukue nafasi hii kuishauri Wizara, naomba mjenge mabwawa na majosho Kilwa ili basi mifugo ile iweze kustawi kama ambavyo tumekusudia. Kwa hali iliyopo sasa ni ugomvi tu baina ya wenyeji wakulima na ndugu zetu wafugaji. Kama ambavyo wanafahamu, sisi watu wa Kilwa hatufugi sisi kazi yetu ni kuvua, kazi yetu kulima, tukiona ng’ombe watoto wanakimbia ndiyo kwanza tumeanza kuona ng’ombe, sasa wameleta kwa maelfu bila kipimo, wanatupa shida, tunapata tabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii labda mimi naeleza kwa hisia nyepesi nyepesi Mheshimiwa Ulega anafahamu, alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, anafahamu ninachokizungumza, ni mashaka. Kwa hiyo, tunaomba hatuna shida na wafugaji lakini andaeni sasa miundombinu ili sisi basi tufanye shughuli zetu kama wavuvi, kama wakulima na wafugaji wafanye shughuli zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala zima la zoezi la upigaji chapa, kuna zoezi hili linaendelea na kusudio lake lilikuwa sasa kuweza kutengenisha wapi sasa wanatakiwa wawepo wafugaji na eneo gani wakulima wataendelea kuwepo na kufanya shughuli zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii ni tajiri wa mapori na ardhi ambayo unaweza ukafanya shughuli za kilimo ipasavyo na shughuli za ufugaji, lakini katika hali ya kushangaza, katika program hii, wakulima na wafugaji wanachanganywa na ili kuondokana na hili ndiyo likaja wazo sasa la kupiga chapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hili la kupiga chapa linaendeshwa kwa urasimu mkubwa. Tunashindwa kuelewa. Kwa mfano, Lindi tuna Selou, tuna mapori ambayo hayana kazi, lakini wafugaji hawa wanakuja kung’ang’ania kukaa katika maeneo ya wakulima, haieleweki tatizo ni nini. Naishauri Wizara wafugaji wawaweke tofauti na wakulima, tuna maeneo mengi katika vijiji vyetu, wafugaji hawa wanaweza wakafanya shughuli zao tofauti kabisa na wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala zima la maendeleo ya uvuvi. Kwangu Kilwa ni wavuvi lakini mpaka sasa ukimuuliza mvuvi ni lini alisaidiwa na Serikali hakuna siku ambayo mvuvi alisaidiwa na Serikali na Serikali haijakuja na program yoyote ya kuwasaidia wavuvi.

Naishauri Serikali iwaangalie wavuvi kama ambavyo inawaangalia wafugaji na wakulima. Wavuvi nao waangaliwe, wapewe vifaa vya kisasa, wawezeshwe kwenda kuvua kwenye kina kirefu cha maji ili waweze kupata tija katika shughuli zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali ilivyo sasa, wavuvi wale wanafanya shughuli zao kienyeji na sasa hivi hizi operesheni za ndugu yangu Mheshimiwa Mpina kwamba kila siku anakuja na programu mpya, inawadidimiza kabisa wavuvi wetu. Kwa hiyo, naomba Serikali ije na programu maalum ya kufanya ustawi kwa wavuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wote wanaweza kuwa mashahidi. Leo ukisafiri kwenda Mikoa ya Kusini, sehemu ambayo unaweza kwenda ukasimama ukapata samaki wazuri ni maeneo ya Somanga. Somanga ile ambayo tunapata samaki, lakini hakuna Soko la Samaki. Tasi na changu wananunua kienyeji, hakuna Soko la Samaki. Hii inaonesha namna gani ambavyo Wizara haijapanga kuwasaidia wavuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali, Mheshimiwa Ulega alikuwa Kilwa pale, basi na ndugu zangu wale wa Somanga pawepo na soko ambalo sasa Waheshimiwa wakipita, watapata samaki wa kupaka na wali wa nazi, mambo yanaenda sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.