Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu katika sekta yangu hii iliyo muhimu sana lakini haijulikani kama ni muhimu. Napenda sana kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, Makatibu Wakuu Wataalamu na Watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hotuba hii ya Waziri kutoka mwanzo ili muda ukiniishia, nisionekane kwamba siungi mkono jitihada za Serikali. Hata hivyo, napenda kusema yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mifugo na samaki inaangaliwa kama ni mali ya mtu mmoja mmoja, lakini kwa ukweli ni rasilimali muhimu ya Taifa. Siyo mali ya mtu mmoja mmoja ila ni rasilimali ya Taifa. Ningependa kusema kwamba, Tanzania ni nchi ya pili kwa wingi wa mifugo. Tanzania ni nchi yenye maziwa mengi na kwa hiyo, ni nchi yenye samaki wengi. Kwa hiyo, tuna bahati kubwa ya kuwa na rasilimali hii ambayo ikisimamiwa na wote na wanaohusika, nchi itanufaika na hii hali ya umaskini ni rahisi kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hivyo kwa sababu tuna ng’ombe milioni 30, tuna mbuzi milioni 18 na kondoo zaidi ya milioni tano. Utaona jinsi nchi ilivyokuwa na rasilimali kubwa kutokana na mifugo hii. Mwaka 2017 tumezalisha nyama tani laki sita na zaidi; tumekamua maziwa lita bilioni 2.4. Sekta hii imekua kwa asilimia 2.8, ingepaswa ikue kwa asilimia zaidi na kuchangia pato la Taifa kwa asilimia 6.9. Uchangiaji huu ni mkubwa kuliko hata Sekta ya Madini. Hata hivyo utaona kwamba macho mengi yanaangalia madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, madini kwa mwaka 2017 imechangia pato la Taifa kwa asilimia 3.5. Inasikitisha kuona kwamba fedha za maendeleo zilizotengwa ni shilingi bilioni nne lakini pamoja na kutenga fedha hizo senti hata moja haikutolewa kwenye sekta hii ambayo ni muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuna namna ya kuikimbia sekta hii, nani ambaye haitaji protini? Nani ambaye hahitaji maziwa? Mtoto gani anayekua bila ya maziwa? Wafugaji ni wachache lakini mahitaji kutoka kwa wafugaji ni makubwa na ni ya watu wote. Naomba tuone hii. Hatua hii ya kutokutoa fedha ya maendeleo, inaonesha kwamba hatuipi sekta hii umuhimu unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na sekta hii Serikali imekusanya shilingi bilioni 16 na zaidi. Utaeleza vipi? Kwa nini fedha ya maendeleo haijatolewa jamani kama siyo wa kutotoa umuhimu kwenye sekta hii? Inaonesha kwamba hatuipi umuhimu stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii ina migogoro mingi; wakulima na wafugaji, hifadhi na wafugaji, hata wale wenye maeneo ya madini wana migogoro na wafugaji. Migogoro hii inatatuliwa kwa kusimamia sheria bila kuwa na moyo wa ubinadamu. Nasema hivyo kwa nini? Kwa sababu naamini wale wanaotekeleza, pengine azma ya Serikali ni nzuri, lakini wale wanaotekeleza hawana nia nzuri, wana nia mbaya au ovu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, angalia ilivyofilisi watu. Ng’ombe waliochukuliwa kwenye hifadhi, ama wamekufa, ama wameuzwa bila kushirikisha wafugaji. Wamewafilisi wafugaji. Angalia jinsi inavyogombanisha wakulima na wafugaji katika kusimamia sheria hii. Angalia jinsi ambavyo tunapunguza amani kati ya Serikali na watu wake. Kwa hiyo, naomba sana nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba jamani operation hizi ziendeshwe; nami siko against au sipingi lakini lazima kuwe na moyo wa ubinadamu kuona kwamba ng’ombe ni rasilimali ya Taifa na wale wanaochukuliwa ng’ombe wanaumia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali, badala ya kufilisi au badala ya watu kufa, tutumie sheria hii ili tuwasaidie wafugaji. Tuone kwamba fedha hizi zinazotumika kwenye operation zinapelekwa kwenye malambo, madawa ya tiba na chanjo. Ionekane kwamba hata wanapopigwa chapa siyo kuharibu ngozi au alama isionekane. Tukichukua hatua zinazostahili, tutakuwa tumewasaidia wafugaji. Ilivyo hapa sasa hivi wafugaji wanaona hawapo kwenye nchi yao, wanaona kwamba wapo porini kama wanyama wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine muhimu ambalo nataka niliseme, kwa nini kila Wizara isitenge eneo la wakulima na wafugaji? Hizi fedha za kwenda kwenye operation zingetumika kuwa na matumizi bora ya ardhi ili wafugaji wajue kwetu ni hapa na wakulima wajue kwetu ni hapa, lakini katika kufanya shughuli zao watakuwa wanashirikiana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini tukifanya hivyo na sisi tuko nyuma ya Mheshimiwa Waziri. Nayasema hayo siyo kuonesha weakness yake, nataka nimshauri ili tushirikiane tuweze kutunza rasilimali hii iongezeke, iweze kunufaisha watu mmoja mmoja na inufaishe Taifa letu

Mheshimiwa Naibu Spika, ningekuwa na muda mrefu, ningesema na watu wa Hanang ambao ni watu wafugaji, wameonewa swagaswaga na kwenye mapori mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri.