Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kusema na kuweka wazi kwamba sitaunga mkono hoja hadi hapo masuala yangu ya kimsingi yatakapopewa majibu na hayo majibu anipatie Mheshimiwa Waziri akiwa anajua ninachokisema na nitayapima majibu yake kadri atakavyoyatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya kwanza Mheshimiwa Waziri Mkuu aliunda Tume ya kushughulikia mgogoro kuhusu masuala ya ranchi, alieleza humu Bungeni kwamba wananchi wawe na subira, alikuja Misenyi akaeleza wanachi wawe na subira ili tuweze kupata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati wananchi wanaendelea kuwa na subira Serikali itoe ufumbuzi wa migogoro ile, viongozi wengine wa nafasi za chini, wala sina sababu ya kuwataja majina na nafasi zao kwa sababu ni wa chini mno kiasi ambacho Mbunge kuwataja ni kuwaonea, wanaandika barua kwa wananchi kwamba waondoke mara moja kwenye maeneo yenye migogoro.

Sasa namuomba Mheshimiwa Waziri kwa sababu chanzo cha migogoro ni Wizara yake atakapokuwa anajibu aeleze kwanini wanaendelea kufanya mizengwe ya kutaka kufukuza wananchi, kwenye maeneo ambayo bado hayajapatiwa ufumbuzi, wakati yapo maelekezo ya Serikali kwamba tusubiri tuwe na subira, wananchi wamekuwa na subira kwanini wao hawahitaji kuwa na subira? Hilo ni jambo la kwanza nitahitaji majibu ya kina.

Mheshimiwa Spika, pili ninayo ramani hapa inaonesha unapovuka Mto Kagera ukaenda mpaka Uganda eneo lote lile ni Misenyi Ranch, hakuna mtu ambaye hata kama ni mtoto angezaliwa leo anayeweza kukubaliana na ramani hii. Kwa sababu ya kanuni sitataja kiongozi mmoja ambaye alishaagiza ramani hii irejeshwe ili ifutwe kwa sababu haiko sahihi. Naogopa kumtaja kwa sababu mwingine anaweza kusimama akasema Kanuni haziruhusu, sasa sitaki kuombewa mwongozo bila ya sababu, lakini ramani hii sio sahihi, kwa sababu unapovuka Mto Kagera unakutana na Makao Makuu ya Wilaya, unapoenda mbele unakuta vijiji, unakuta Kata, sasa unapokuja na ramani unaitumia kugawa blocks Misenyi Ranch ukasema kuanzia Mto Kagera kwenda mpaka Uganda yote ni ranch, ukagawa ukapata blocks 22 siwezi kukubaliana na masuala haya. Ndiyo maana nasema Mheshimiwa akija atoe maelekezo na majibu sahihi.

Mheshimiwa Spika, pia ipo ramani nyingine inayoonesha kwamba Misenyi Ranch imezungukwa na vijiji, ukiangalia nyaraka mbalimbali ambazo nizazo hapa vijiji hivi vina hati, vimesajiliwa na vinatambulika na vilipimwa. Ukisoma taarifa hii kuna sehemu Mheshimiwa Waziri anasema kuna vijiji vimevamia ranch. Napenda niseme mimi kama Mbunge wa Jimbo la Nkenge kwamba ranchi ndiyo imevamia vijiji. Sasa hatuwezi kuruhusu mambo ya namna hii hatuwezi kuruhusu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mtu wa mwisho kupokea mambo ya namna hii. Nikisema hivi, wako wengine walitaka kunipima sitaki kuwataja kwa sababu ukishakuwa Mbunge, Mbunge unasimamia Serikali, wako waliojaribu kunipima, kuna bwana mmoja alinipa barua akasema nenda uwaambie wananchi wako waondoke. Nilimjibu nikasema Mheshimiwa kwa nafasi yako huwezi kuniagiza, mimi naisimamia Serikali na wewe ni sehemu ya Serikali sasa lazima kila mtu aheshimu nafasi yake. Ukiwa Mkuu wa Mkoa, ukiwa sijui nani wewe fanya kazi yako na mimi acha nifanye kazi yangu. Hilo nililisema na naendelea kulisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mtu wa mwisho kuwaambia wananchi waondoke kwenye maeneo yao ambayo wana haki ya kukaa, na mimi nikiwa hapa natamka wananchi wangu katika maeneo yao wakae mpaka hapo nitakaposema kwamba sasa Serikali imeleta taarifa Bungeni na taarifa hiyo nimeikubali, vinginevyo wanapoteza muda wao bure hizo barua wanazoandika wanapoteza muda wao bure na hii vita niko tayari kuisimamia, niko tayari kupambana ndani ya Bunge, nje ya Bunge na kokote kule watakaponipeleka nipo tayari na nitafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nisema kwamba mipaka ya ranchi na Misenyi na vijiji inaeleweka, mwaka 1968 ranchi hiyo ilipokuwa inaanzishwa, walioanzisha ranchi hiyo walienda wakakutana na wananchi na wananchi hao baadhi yao bado wapo wanaendelea kuishi. Walikubaliana kwamba mipaka ya ranchi itakuwa Mto Kiboroga pamoja na Mto Kyakakuru. Mheshimiwa Waziri utakapotoa majibu hapa unieleze hii mipaka kwa nini hamuioni na kwa nini hamtaki kuitambua?

Mheshimiwa Spika, tulifanya operation kubwa ya kuondoa ng’ombe kwenye hifadhi za Serikali, ng’ombe wakaondolewa Biharamulo, jambo la kushangaza baada ya ng’ombe hao kuondolewa Biharamulo sasa wamepelekwa katika Ranchi ya Misenyi. Taarifa nilizonazo kwa mfano katika block No. 15 mwenye kitalu amepokea shilingi 50,000 kutoka kwa wachungaji wawili wenye ng’ombe 600, ukichukua shilingi 50,000 mara 600 unapata shilingi milioni 30. Hizo ni pesa kapokea tu kwa kuwapa ardhi ya vijiji watu wachungie. Nashangaa Waziri anaposema hana hela, hela unazo sema hutaki kuzikusanya.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri ameeleza kwamba kuna vitalu kumi vimefanyiwa tathmini, lakini ukiangalia ramani hii niliyoionesha hapa wao walisemawana vitalu 22, kama una vitalu 22 kwa nini hivi vitalu vingine hutaki kufanyia tathmini unafanyia 10 tu? Hautaki kufanyia tathmini vitalu vyote kwa sababu taarifa zilizopo na nina uhakika hizi ni taarifa za kweli, mkitaka taarifa natoa hapa, ninayo taarifa hapa inaonesha katika Ranchi ya Misenyi katika zile blocks tuliowapa tukifikiri ni wawekezaji siyo wawekezaji ni wachungaji tu. Misenyi Ranch kumejaa ng’ombe za kutoka nchi jirani hakuna asiyejua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeenda kule nimeingia kwenye ranchi nilifanya ziara ya kushtukiza nimeingia mle kwanza ni rahisi kuingia kutambua kwa sababu ng’ombe wote wa Ranchi ya Misenyi wanajulikana. Nilipoingia mle nikakuta kuna ng’ombe wengi tu ambao ni aina ya Ankole. Ranchi ya Misenyi haina ng’ombe aina ya Ankole, wale ng’ombe wote na ushahidi ninao nilipiga picha na hizo picha nimezihifadhi kwenye sehemu mbalimbali na zingine nimeziweka sehemu zingine ili zisiweze kuibiwa, kwa hiyo mtu yeyote asije akaniteka akafikiri akiniteka hizo picha atazipata, hutazipata kwa sababu zimehifadhiwa pengine na watu wana password.

Mheshimiwa Spika, ng’ombe wale cha kushangaza wala hawajapigwa chapa, sasa viongozi wakuu wa nchi wameagiza ngo’mbe wote wapigwe chapa lakini kule Ranchi ya Misenyi ng’ombe wamo, kwanza siyo wa Misenyi Ranch, lakini wanakula kwenye majosho ya Misenyi Ranch wanalindwa, nani anawalinda hao? Lakini kwa mwananchi mmoja tu akijaribu tu ng’ombe wake kuingia kwenye ranch anakamatwa anatozwa faini 50,000.

Mheshimiwa Spika, nasema wazi kabisa hapa, hakuna mwananchi wangu katika Jimbo la Nkenge katika Kata ya Kakunyu na maeneo yote atakayetoka kwenye ardhi hata kwa inch moja hadi hapo nitakaposema. Vita hii nipo tayari kuisimamia, ninazungumza mimi, Balozi Dkt. Diodorus Buberwa Kamala na katika hili nitaweka Ubalozi kidogo pembeni ili nifanye vizuri kwa sababu kuna rafiki yangu alikuwa ananiambia Mheshimiwa toka umekuwa Balozi umebadilika. Ndiyo nimebadilika kidogo lakini Balozi ni yule yule na Kamala ni yule yule na utaalam ni ule ule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa wavuvi wa Kashenye, nazungukwa na Ziwa Victoria, wale wavuvi siku moja nilienda kule nilitaka niangalie wanapata samaki kiasi gani, nikakaa kwenye mwalo pale wakaenda kule, vijana walivyokuja hawakurudi na samaki. Nikauliza vipi samaki wapo wapi? Wakasema Mheshimiwa unajua kwa nini tulete samaki wetu hapa tukishawapata huko kwenye maji tunaenda kuwauza Uganda kwa sababu Uganda kodi zao kimsingi ziko chini, lakini tukikanyaga upande wa Tanzania kodi nyingi mnoo lakini tukiwa tunakuja hivi, kuna operation juu ya operation, kwa hiyo tunaona ni bora tukishapata samaki wetu twende tuuze Uganda. Kwa hiyo, Mheshimiwa Balozi kwa kweli kama bado una muda wa kukaa hapa, kaa uendelee kusubiri hautaona samaki wowote. Kwa hiyo, nikapiga salute nikawashukuru nikaondoka. Hivyo Mheshimiwa Mpina hizi kampeni unazozifanya hebu ziangalie zisije zikatuletea matatizo. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nasema siungi mkono hoja hadi hapo nitakapopata majibu ya kina kuhusu hoja nilizozitoa hapa.