Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nami nianze kwanza kwa kuwapongeza sana Waziri na Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, nimesimama kwa kuelewa kwamba sekta ya mifugo na uvuvi zinagusa sana mambo ya sheria. Katika utekelezaji wa sheria, tufahamu kwamba sheria inaweza kuwa nzuri lakini utekelezaji wake ukawa na kasoro hapa na pale. Kasoro zinazojitokeza katika utekelezaji wa sheria zisitufanye tuone kwamba ile sheria haifai kabisa.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa na wewe unafahamu kabisa kwa sababu unatoka kwenye eneo hilo ni kuweka uwiano kati ya uhifadhi na matumizi ya rasilimali ili wananchi wetu waweze kuneemeka. Kwa hiyo, pamoja na mambo yote tunayoyazungumza, napenda Waheshimiwa Wabunge tuzingatie kabisa kwamba sheria hizi zote zimetungwa kwa nia njema ili kwa upande mmoja tuhifadhi wanyamapori, misitu na samaki kwa faida yetu sisi na vizazi vijavyo. Hata hivyo, najua kwamba katika utekelezaji kumekuwa na matatizo ya hapa na pale.

Mheshimiwa Spika, nimesimama kueleza jambo fupi tu kuhusu baadhi ya mifugo iliyokamatwa na kutaifishwa katika mbuga zetu za hifadhi. Nalisema hilo kwa sababu linaangukia pia katika Ofisi ya Mashtaka na chini ya Mkurugenzi wa Mashtaka.

Mheshimiwa Spika, nipende kueleza Bunge lako kuwa baada ya kupata malalamiko mbalimbali kutoka kwa wananchi kupitia kwa Waziri wa Mifugo, jana Mkurugenzi wa Mashtaka amepitia mashtaka mbalimbali ambayo yamefikishwa mbele yake ili kuona ni yapi anaweza kuyachukulia hatua. Kwa kupitia mamlaka yake aliyonayo kwa sheria na katiba, ameamua kuachia ng’ombe 553 za wafugaji katika eneo la Swagaswaga ambao baadaye wataelezwa utaratibu. Kwa hiyo, Mkurugenzi wa Mashtaka ameamua kwamba katika kesi hizo nne katika eneo la Swagaswaga ambalo linahusu ng’ombe 553 hatakata rufaa na amri imetolewa ng’ombe hao waachiwe kuanzia leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo jumla ya kesi tano zina rufaa katika Mahakama ya Rufaa ambapo Mkurugenzi wa Mashtaka amekata rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu. Kesi hizi kwa sababu ziko Mahakamani tunaomba ziendelee lakini ambacho tutajitahidi kuiomba Mahakama ziharakishwe kusikilizwa.

Mheshimiwa Spika, pia ziko kesi nyingine ambazo wenyewe wafugaji wamekata rufaa. Tungewaomba wafugaji wenyewe waliokata rufaa katika kesi hizo ni vyema wakashauriwa kufuta rufaa zao ili pia kuharakishwa kuachiwa kwa mifugo yao, kwa sababu kama kesi ziko kwenye Mahakama ya Rufaa zitaendelea kusikilizwa.

Mheshimiwa Spika, kuna jumla ya kesi 23 kati ya 27 ambapo watuhumiwa walilipa faini bila kupelekwa Mahakamani na wakarejeshewa mifugo yao. Pamoja na kulipa faini ambayo ni kati ya shilingi 10,000 na shilingi 300,000 lakini bado kuna malalamiko kuwa wamelipishwa faini kubwa kinyume cha sheria. Tungependa wale wote ambao wana malalamiko ya kweli wayawasilishe ili pia yaweze kufanyiwa kazi ili pale panapolazimika haki itendeke.

Mheshimiwa Spika, la jumla na mengine tutayazungumzia siku ya Wizara ya Maliasili na Utalii, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka baada ya kuwa ametengeneza maelekezo mahsusi kwa Wapelelezi na Waendesha Mashtaka kwa ajili ya kesi zinazohusu wanyamapori na kuzinduliwa na Mheshimiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sasa anajipanga kutengeneza mwongozo mwingine kwa ajili ya Maafisa wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maliasili na Utalii na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili ziweze kuweka utaratibu wa kushughulikia kesi zinazohusu mifugo, uvuvi na atashirikiana na Mahakama ili kuona jinsi gani kesi zinazohusu mifugo zitaendeshwa mapema.

Mheshimiwa Spika, katika Bunge hili tutaleta Muswada wa kuanzisha Mahakama Zinazotembea (Mobile Court). Ni imani yetu kwamba Mahakama hizo zikiundwa kwa kushirikiana na Wizara zinazohusika operation hizi zitakapofanywa basi hiyo mahakama inayotembea itakuwa hapo ili kuhakikisha kwamba haki inatendeka.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.