Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Nami nianzie alipomalizia mwenzangu, nitaanza kuzungumzia kwenye migogoro ya mipaka kati ya hifadhi za vijiji pamoja na mapori yetu ya akiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekaji wa vigingi limekuwa ni tatizo kubwa sana kwa wananchi wetu lakini kibaya zaidi suala la ushirikishwaji halipo. Wananchi wamekuwa wakipigwa lakini cha kushangaza ni kwa nini Serikali haitaki kushirikisha wananchi. Kingine nachojiuliza ni kwamba uanzishwaji wa vijiji inashirikisha Wizara ambayo inatokana na Serikali hii. Ni kwa nini sasa wanapoanzisha vijiji wasingeshirikisha Wizara zinazohusika mfano TAMISEMI, Maliasili na Ardhi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tatizo limekuwa kubwa sana na ni mmoja wa Wajumbe wa Kamati na naunga mkono taarifa ya Kamati yetu kwamba ni vizuri zoezi hili likasimamishwa ili utaratibu wa ushirikishwaji wa wananchi ukafanyika. Kutumia bunduki na risasi siyo suluhisho la kumaliza migogoro. Wananchi wamekuwa wakipigwa na hii imesababisha maumivu makubwa sana kwa wafugaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafugaji wa nchi hii wamekuwa wakilia kila siku, mifugo yao imekuwa ikiuwawa na hii inasababishwa na askari wale ambao si waaminifu wamekuwa wakiswaga mifugo na kuiingiza kwenye hifadhi zetu za Taifa. Sisemi kwamba askari wote ni wabaya lakini wapo baadhi yao hawana utu, wamekuwa wakidai rushwa kwa wananchi wetu na ukishindwa kutoa rushwa mifugo yako wanaiingiza kwenye hifadhi lakini mingine inapigwa risasi na mingine inakufa kwa kukosa matunzo. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri na Waziri alieleza kwenye Kamati yetu kwamba wako ng’ombe waliokamatwa na kuingizwa kwenye hifadhi na alitoa amri ng’ombe hao waachiwe lakini mpaka leo kuna baadhi ya ng’ombe hawajaachiwa. Sasa huu ni ukiukwaji wa taratibu na sheria kwa wafugaji wetu na tuelewe kabisa kwamba mifugo kwa wafugaji ndiyo maisha yao. Mifugo hiyo ndiyo wanayosomeshea watoto wao, wanalisha familia zao na hata kupata afya bora wanaotumia fedha zinazotokana na mifugo. Kwa hiyo, ni lazima tuwafanyie haki wafugaji hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamesema wenzangu nchi hii wafugaji wanalia, wakulima wanalia, wafanyabiashara wanalia usalama unatoka wapi. Kama watu wote tunalia kwa sababu ya ukiukaji wa sheria, hii siyo sawa, tumwombe Waziri ahakikishe kwamba haki inatendeka ili wananchi wetu waweze kuishi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la wafanyabiashara ya wanyama hai. Mwaka 2016 wafanyabiashara hawa walizuiliwa kufanya biashara hii. Wafanyabiashara hawa walikuwa wamekata leseni, wamelipia ada wanazostahili kulipia lakini pia walikuwa walishatafuta usafiri wa kusafirisha wanyama hao. Likatolewa agizo la kusitisha usafirishaji wa wanyama hawa. Waziri alikuja mbele ya Kamati lakini alisema ndani ya Bunge hili kwamba mnaanza mchakato wa kuwarudishia fedha za leseni lakini pia na kupanga utaratibu mzuri wa kuweza kuwaruhusu waendelee na biashara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanyama wanaokamatwa ni wale ambao wanasumbua sana katika jamii yetu mfano, kweleakwelea, tandu, ngedere, lakini badala ya kuwashukuru wafanyabiashara hawa imekuwa ni tatizo kwako. Ni muda mrefu sasa umepita wafanyabiashara hawa walikopa fedha benki, wengine wameuziwa nyumba zao, maisha yao ni magumu sana kwa sasa. Kwa hiyo, niombe sana Wizara ichukue hatua za haraka kuhakikisha wafanyabiashara hawa wanaruhusiwa kufanya biashara hiyo ya usafirishaji wa wanyama hai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni suala la biashara ya uwindaji. Biashara hii imeshuka na sababu za kushuka tumeelezea kwenye taarifa yetu ya Kamati ni baada ya matamko ya Mheshimiwa Waziri ambapo alisitisha biashara hii na ikasababisha vitalu vingi kurudishwa zaidi ya vitalu 18 vimerejeshwa.