Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Hizi dakika tano inabidi uwe na speed kama ya Profesa J kwa sababu inahitaji uwe na speed kubwa sana. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie fursa hii kuwapongeza Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wake kwa kazi ambayo ina changamoto nyingi lakini ni kazi ambayo inataka uvumilivu wa hali ya juu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hoja moja tu na ndiyo maana nimekubali kuchangia dakika tano au dakika mbili zinaweza kunitosha. Jimbo lote la Ulyankulu ni hifadhi, toka tumeanza kuambiwa Kamati ya Wizara mbalimbali itakutana kuliamulia jambo hili bado hatujapata suluhisho. Mwaka 1972 msitu ulikuwa mkubwa waliletwa wakimbizi ndugu zetu kutoka Burundi lakini kama kuna sheria za kikoloni sheria hizi zilimkuta Mtemi Mirambo na mpaka leo Mtemi Kadutu yupo. Kwa hiyo, hakuna suala la kusema kwamba wananchi waliwakuta wakoloni maana wakoloni hawawezi kufika sehemu ambayo haina watu. Kwa hiyo, jambo hili ni kama vile artificial ifike


mahali sasa Serikali itueleze wananchi wa Ulyankulu wapi tutakwenda kama bado wameng’ang’nia hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati wa uchaguzi, wenzangu mtanisamehe kidogo kwa maneno yangu wakati mwingine. Wakati wa uchaguzi tuliambiwa baada ya siku tatu tutapata wilaya, tutapata halmashauri lakini mpaka sasa hakuna. Kila tukikumbusha habari ya halmashuri, tukikumbusha kupewa wilaya tunaambiwa hifadhi. Kwa hiyo, hili neno hifadhi ni msamiati wa Kijapan au Kinyamwezi au wa wapi. Tunataka Serikali ituamulie inatupeleka wapi basi? Kama sisi tulikuwepo kabla ya hizo sheria za hifadhi, leo hii watu tumeenea jimbo zima halafu unatuambia hii ni hifadhi jimbo zima ni jambo la ajabu kabisa, yaani bora msitu kuliko wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unatufahamu sisi Wanyamwezi tunaweza kubadilika na tukaanza mapambano, hilo linajukana tutazuia kila kitu kisifanyike kila siku nasema hapa. Mheshimiwa Waziri mdogo wangu HK tuletee taarifa hapa wananchi wa Ulyankulu wapate imani vinginevyo wazee wenzangu huku 2020 ni kiboko. Suala hili la kuwahamisha watu halitakubalika, hatuwezi kuwa tunawaahidi watu wakati wa uchaguzi halafu tukishashinda tunawatelekeza, haiwezekani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri hebu tusaidie hiyo Kamati ya Wizara mbalimbali lini itakuja na maneno hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ndiyo maana nimesema sina maneno mengi, Mheshimiwa Waziri alikuja Ulyankulu akiwa Naibu Waziri wa Afya. Kwa kidogo sana aliona changamoto zilivyo, niwaalike sasa Waziri pamoja na Naibu Waziri njooni Ulyankulu mjionee wenyewe, je bado kuna haja ya kusema hifadhi maana eneo lote lina watu na linatumika. Sasa njooni wenyewe badala ya kupata taarifa tu kutoka kwa wataalam na ambao hawajafika mjione Ulyankulu je bado inaendelea kuitwa hifadhi au ni makazi ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana lakini naunga mkono hoja.