Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa ili niweze kuchangia katika hotuba hii iliyo mbele yetu ya Bajeti Kuu ya Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Mpango pamoja na Naibu wake.

Mheshimiwa Spika, kwanza niungane kwa dhati kabisa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya katika Taifa hili katika kupigania maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nifunguke tu kwamba Bunge lako hili kabla ya mimi sijawa Waziri hapa nimepitia maeneo mengi sana na Bunge hili limenipeleka kwenye Taasisi mbalimbali kwenye Mabunge ya Afrika, nimeenda kwenye Mikutano mingi ya kikanda na ya Kimataifa sijawahi kuona Kiongozi ambaye committed kama Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Nampongeza sana kwa kazi kubwa anayoifanya katika nchi yetu hii ya Tanzania katika kupigania maendeleo ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nikupongeze wewe sana, moja ya sifa ya Kiongozi ni kutengeneza viongozi. Toka ulivyokuwa Mwenyekiti wa Bunge hili, baadaye ukawa Naibu Spika, baadaye ukawa Spika umetengeneza viongozi wengi sana kwenye Bunge hili. Kwa hiyo, uwezo wako siyo wa kutiliwa mashaka yoyote na mtu yeyote anayejua historia na mimi pia tu nikuombe kwamba kwa baadhi ya wale Wabunge wageni ambao hawaijui historia wasiwe wanakurupuka kushambulia watu wasiowajua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo na nirudie pia kumpongeza sana Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango na Naibu wake Ashatu Kijaji kwa kazi kubwa sana ambayo wanayoifanya katika kulinda uchumi wa nchi yetu. Katika kipindi hiki kifupi cha Utawala huu wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali hii ya Awamu Tano mambo mengi yamefanyika sana, mageuzi makubwa yamefanyika ya kiuchumi ambapo Mheshimiwa Dkt. Mpango tunampongeza sana kwa kazi hiyo kubwa kwa kuendesha hilo gudurumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtakumbuka na Wabunge watakumbuka hapa na wengine wameni-refer kwenye michango yao niliwahi kulia mbele ya Bunge hili na kukataa Bajeti ya Serikali, kipindi ambacho kilikuwa kigumu sana kwangu pia kwa chama changu, lakini yalikuwa ni baadhi ya mambo ambayo leo hii yamefanyiwa marekebisho makubwa na mageuzi makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo mambo makubwa nsihukuru, nimpongeze hapa Mheshimiwa Stanslaus Mabula ambaye alipata nafasi hapa ya kuchangia kuna mambo makubwa katika Taifa hili ambayo tulikuwa tukiingia hasara kubwa na tulirekodiwa kati ya nchi ambayo ina-facilitate zoezi la Illicit Financial Flow kwa kiwango kikubwa. Hata hivyo, mapambano yaliyowekwa, mechanism zilizowekwa, kupiga vita suala la Illicit Financial Flow katika nchi yetu, huwezi kuamini leo akina nanii ambao wanafanya tathmini ya Illicit Financial Flow, tunawakaribisha Tanzania waje watu- access.

Mheshimiwa Spika, watakuja kuona jinsi udhibiti mkubwa uliyofanyika na sasa zoezi hili linafanyika kwa kiwango cha chini sana hapa nchini kwetu. Pia mambo ya transfer pricing vilevile, mambo ya dollarization vilevile na suala gumu hili lilishindikana siku zingine suala la credit rating na lenyewe katika kipindi hiki limeweza kufanyika. Kwa hiyo, viongozi wetu ambao wanaongoza jukumu hili, Waziri wa Fedha na msaidizi wake, pamoja na Katibu Mkuu wake na wengine wote wanaohusika katika usimamizi wa uchumi wetu tunawapa heko na tunawapongeza sana kwa bidii hizo za kazi.

Mheshimiwa Spika, basi baada ya kusema hayo, niweze kuzungumza kidogo kuhusu baadhi ya mambo ambayo yamezungumzwa ambayo yanatekelezwa katika Wizara yangu:-

Mheshimiwa Spika, moja ni jambo la chanjo na uogeshaji wa mifugo kwamba, tunayo shida kubwa. Ni kweli kabisa nakubali kwamba, suala la chanjo na uogeshaji wa mifugo ambapo mifugo mingi inakufa kila mwaka kwa kukosa chanjo na mifugo mingi inakufa kila mwaka kutokana na kupe na kwa kutokana na kutokuogeshwa. Sasa tunafanya kila aina kuhakikisha kwamba, jambo hili tunalifanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, Chuo chetu cha Utafiti cha Uzalishaji wa Chanjo cha Kibaha kinaendelea vizuri kuzalisha chanjo hapa nchini. Vilevile tumepata bahati ya kupata mwekezaji mpya kutoka India ambaye naye anakuja kujenga kiwanda hapa kwa ajili ya kuzalisha chanjo kwa wingi. Kwa kufanya hivyo, tutaweza kuwahakikishia wananchi wetu na kuwa-guarantee kupatikana kwa chanjo kwa muda na kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kama hiyo haitoshi pia, kwamba, Wizara yangu inatengeneza sasa mpango ambao utawezesha chanjo kupatikana kiurahisi, lakini vilevile uogeshaji wa mifugo kuwezekana kwa urahisi na vilevile kwa bei ambazo wafugaji wetu watazimudu. Kwa hiyo, jukumu hilo linafanyika na mpango huo tutahakikisha kwamba, wafugaji wote, halmashauri zote zinashirikishwa katika kuutekeleza.

Mheshimiwa Spika, kuna suala lingine la pili liliwahi kuzungumzwa hapa Bungeni kuwa ni suala la uzalishaji wa maziwa hapa nchini na hasa ikilinganishwa nchi yetu na nchi ya Kenya kwamba, sisi tunazalisha mpaka sasa hivi lita za maziwa bilioni 2.4 wakati Kenya wanazalisha bilioni 5.2.

Mheshimiwa Spika, katika ulinganifu huo ni kweli kabisa, lakini nataka kuwa-assure Waheshimiwa Wabunge kwamba, kutangulia si kufika, tumejipanga vizuri katika kuhakikisha kwamba, tunakuja na uzalishaji mkubwa wa maziwa hapa nchini. Sisi hatuwezi kushindana na Kenya, hatuwezi kushindana na nchi yeyote ile ya Afrika kwa sababu, sisi kama ninavyosema, ni nchi ya pili tu kuwa na mifugo mingi hapa Afrika ikiwa nchi ya kwanza inayoongoza mpaka sasa hivi ni Ethiopia.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, sisi tuna malisho mazuri kuliko mtu yeyote, tuna maji bora kuliko mtu yeyote pamoja na kwamba, ng’ombe wa maziwa sasa hivi ni 789,000 tu, lakini mpango tulioanzisha sasa hivi wa kuhimilisha mifugo yetu ambao tunaita this is a massive artificial insemination ambapo tutahimilisha kila mwaka kutafuta mitamba milioni moja kwa mwaka, kwa miaka mitatu tutakuwa na mitamba milioni tatu na tutaweza ku-compete na yeyote na tutaweza kuzalisha maziwa mengi kuliko mtu yeyote. Tuna mifugo, tuna maeneo mazuri na swali hili limenifurahisha na liliulizwa na Mheshimiwa Jesca. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niseme kwamba, Kituo chetu cha Taifa cha Uhimilishaji (NAIC) tumekifanyia ukarabati mkubwa sana ambao utawezeasha kuzalisha mbegu nyingi za kutosha. Tumenunua madume bora 11, kuna mtu mmoja aliwahi kuchangia hapa Bungeni akasema kwamba, madume hayo 11 hayawezi kutosheleza na kwamba, ni kidogo mno na kwamba, Serikali haiko serious.

Mheshimiwa Spika, niwaambieni kwamba, haya madume 11 yanaweza kuhimilisha ng’ombe zote wa Afrika Mashariki. Mbegu zinazozalishwa na madume 11 zinaweza kuhimilisha mahitaji yote ya uhimilishaji katika nchi za Afrika Mashariki. Kwa hiyo, tumejipanga vizuri na tutakuwa na maziwa mengi ya kutosha katika nchi yetu.