Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru Mungu wangu kwa neema yake ya siku ya leo ya kuzungumza katika Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naamini kwamba Serikali inafanya kazi kubwa na Mheshimiwa Waziri Dkt. Kigwangalla pamoja na Mheshimiwa Hasunga mmezunguka nchi nzima kuangalia changamoto ambazo zinaelezwa na Waheshimiwa Wabunge. Najua utakaposimama kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge mtazungumzia changamoto hizo kwa sababu mnazijua. Pia najua kwamba mmezikabidhi changamoto na kero hizi kwa wataalam wenu ili wazishughulikie na tunaamini sasa zitafanyiwa kazi. Tunakuamini Waziri na hukuzunguka bure na wataalam wako pia tayari kukusaidia na pale ambapo unaona hupati msaada najua utachukua hatua zinazostahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka mmea wako uzae matunda lazima uutunze, lakini lazima uweke mbolea na maji na upige dawa. Ukitaka mifugo yako upate mazao mazuri lazima uilishe, wapate chanjo na wapate maji na malisho mazuri. Wizara hii ya Maliasili na Utalii inafanya kazi kubwa, inachangia asilimia 17.6 ya pato la Taifa. Wizara hii ndiyo Wizara inayoingiza fedha nyingi za kigeni, Wizara hii ndiyo inayoingiza asilimia 25 ya fedha zote za kigeni na Wizara hii ndiyo inayoingiza fedha za kigeni dola bilioni 2.3 kwa mwaka. Kwa hiyo, lazima Wizara hii ipate fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia bajeti tunayomaliza Wizara hii ilipata asilimia 33.5 tu fedha za maendeleo, fedha ambazo haziwezi kuimarisha Wizara ya Maliasili na Utalii. Tunalalamika kwamba watalii hawaji kama wanavyokwenda katika nchi jirani, hawawezi kuja kwa sababu fedha za maendeleo hatuna, hatuwezi kuimarisha barabara zetu, huduma zetu haziwezi kupendeza kama fedha hazipo za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Utalii inafanya biashara na watu binafsi na bajeti iliyopita walisimamisha biashara ya wanyama hai kusafirishwa nje ya nchi. Serikali ikaahidi kabisa kwamba hawa watu watalipwa fidia na tulitegemea kwamba mpaka leo bajeti nyingine imeingia, Wizara au Serikali itakuwa imekwishalipa fidia. Hawa watu walikopa fedha kwenye benki, hawa watu walitumia fedha zao lakini mpaka leo Serikali haijalipa fidia kwa watu hawa.

Mheshimiwa Spika, nategemea Waziri utakaposimama utasema kitu kwamba hawa watu watalipwa fidia kipindi gani kwa sababu interest inaendelea kukua kule benki, lakini Serikali haijawalipa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nirudi nyumbani, kule kwetu Mkungunero - Kondoa tumeshawapeleka zaidi ya Mawaziri watano. Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla ulikwenda, Mheshimiwa Hasunga alikwenda, tukaitisha mkutano mkubwa, ukawahutubia wananchi, ukaenda na Mbunge wa pale Mheshimiwa Dkt. Ashatu, wananchi wakapata matumaini, lakini mpaka leo hakuna kinachoendelea kati ya wananchi wa vijiji vya kule na hifadhi ya Mkungunero.

Mheshimiwa Spika, askari watatu waliwahi kuuawa kule, wananchi wanalima kule mazao yao yanafyekwa, ng’ombe wakiingia eneo lile la eka 50 tu wanachukuliwa, harudishwi kwa wenyewe na wenyewe wanatozwa faini, na ni mgogoro wa muda mrefu sana. Mheshimiwa Waziri ulipokwenda ulitoa ahadi nzuri na wananchi wakapata imani na wewe, kijana ulipokwenda na morale walikupigia makofi, wakapata imani kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasikitika, natamani kulia kwa sababu kila ninaposimama katika Wizara hili nalizungumza suala la Mkungunero. Mheshimiwa Rais alipompa Mheshimiwa Dkt. Ashatu nafasi ya Naibu Waziri, wananchi wa eneo lile la Mkungunero vijiji vile 12 walipata amani, kwamba sasa suala lao litaisha, lakini mpaka leo mwaka wa tatu sasa tumeanza, suala la Mkungunero bado liko pale pale. Ninakusihi hebu fanya kitu, ninakusihi wale wananchi shida yao sasa ikashughulikiwe.

Mheshimiwa Spika, lakini tena tuna suala la pori la Swagaswaga. Mpaka wa pori la Swagaswaga na Vijiji vya Handa na Lahoda ni tatizo kubwa. Mpaka upo lakini maafisa wako Mheshimiwa Waziri hawataki kufuata mpaka uliopo pale. Ninakusihi sasa ukashughulikie mipaka kwa sababu kila Mbunge anayesimama anazungumza suala la mipaka. Sisi Dodoma hatutaki migogoro na Serikali yetu, lakini kama migogoro haitatuliwi mapema wananchi hawawezi wakakubali, kama migogoro haishughulikiwi kwa wakati wananchi wataendelea kulalamika, Mheshimiwa Waziri naomba sasa suala hili likashughulikiwe haraka inavyowezekana.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie tena suala la tozo inayotozwa kwa TANAPA na Ngorogoro. Mashirika haya yanafanya kazi nzuri sana na hata fedha tunazopata yanatokana na mashirika haya. Na masharika haya nikubaliane na kamati kwamba wanatoa asilimia 15 ya mapato ghafi kwa Mfuko Mkuu wa Serikali. Halafu wanatoa asilimia tatu kwenda Mfuko wa Uendelezaji wa Utalii, na fedha hizi zinakwenda Serikalini.

Mheshimiwa Spika, lakini bado wanatakiwa kulipa VAT, na bado wanalipa kodi. Ninadhani tozo hizi na gharama hizo ambazo mashirika haya yanaingia ndio maana unakuta gharama zetu ni kubwa kuliko nchi ya Kenya, gharama zetu ni kubwa kuliko nchi za jirani. Serikali inaona nini? Masharika haya ni Serikali, fedha zao hawatii mfukoni, fedha zao zinaingia Serikalini na fedha hizi ndizo zinazowasaidia kutengeneza miundombinu na watalii wanapokuja wanakuta kwamba kuna miundombinu mizuri. Ninaomba sasa Serikali ione namna kuacha VAT kwa fedha hizi ambazo kwa hakika zinakwenda Serikalini.

Mheshimiwa Spika, mashirika haya yamefanya vizuri kipindi chote, na hata tunapoongea asilimia 17.6 ya Pato la Taifa mashirika haya yanahusika. Hata utalii wa picha kwenye mapori yetu yanahusika, lakini bado wanatozwa kodi hiyo.

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumze suala la ushikaji wa wanyama au ng’ombe au mifugo katika mapori yetu. Serikali inaweza ikaongea na hao wafugaji, wakaweka utaratibu, kwamba wanaposhika ng’ombe wakaandikishane kijijini na wenye mifugo na Serikali iwe na RB kwamba nimeshika ng’ombe wa Mama Bura 400 na sasa kesi iendelee mahakamani ili huyu mtu aendelee kulima na aendeleze kufanya mambo ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mifugo umechukua, halafu unakuja kumtoza faini shilingi milioni 50, anatoa wapi? Serikali yetu ni Serikali ya wanyonge, mkulima akishikiwa mifugo yake waandikishane kwa Mwenyekiti wa Kijiji exhibit itabaki kwa mwenye mifugo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, inasikitisha na kuhuzunisha, lakini niishauri Serikali yangu, watafute utaratibu mzuri ila haya malalamiko yanayotokea kwa wafugaji yatoke, naunga mkono hoja.