Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DANIEL E. MTUKA: Ahsante Mheshimiwa Spika na mimi kupata nafasi hii kuchangia Wizara ya Maliasili na Utalii.

Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii, kwa kutupa uhai, lakini pia naipongeza Serikali yangu ya Jamhuri ya Tanzania hasa Mheshimiwa Rais anavyofanya kazi, wote tunaiona.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze pia Wizara hii ndugu yangu Kigwangalla, shemeji yangu, kwa maana ya Naibu Waziri Hasunga, nawaona ni vijana wanachapa kazi, wanazunguka huku na huku ukimuona Mheshimiwa Kigwangalla shemeji yangu amepiga buti zile za kijeshi ananikumbusha mbali sana wakati nikiwa kambi za jeshi huko. Kwa kweli nawapongeza sana wanafanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hayo ninayo maoni machache, mchango wangu mdogo na nikianzia, ukifungua kwenye kitabu chako ukurasa wa 19 nimekuta kuna ulinzi wa wananchi na mali zao dhidi ya wanyama pori wakali na waharibifu. Nimejaribu kupitia Sheria ya Hifadhi ya Wanyamapori (Wildlife Conservation Act) Namba 5 ya mwaka 2009.

Mheshimiwa Spika, kwenye sheria hiyo nimeenda nimeangalia zile regulations zake, kwenye regulations hizo za mwaka 2011 nimekuta kuna jedwali namba nne ambalo linaonesha viwango vya fidia wanazolipwa watu ambao wanauawa na wanyama, wanaopata ulemavu wa kudumu, wanaojeruhiwa pamoja na uharibifu wa mazao.

Mheshimiwa Spika, viwango hivi ni vidogo na vinasikitisha sana. Ukiangalia kwa mfano binaadamu anapouawa na mnyama, ukiangalia kwenye lile jedwali inasikitisha sana.

Mheshimiwa Spika, binadamu anapouawa anasema fidia ni shilingi milioni moja lakini anapopata ulemavu wa kudumu, anapata shilingi 500,000 tu. Hapana, hiki kiwango ni kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naweza nikatoa mfano mdogo siwezi kulinganisha na mwanajeshi anapouawa anapokwenda kupigania kulinda amani, kwa mfano labda Darfur kwamba ameuawa kwa bahati mbaya. Tulijibiwa hapa na Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi kwamba fidia ya huyu mtu ni karibu milioni 150.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo hata wale waliouwawa kwenye vita vya Kagera wanalipwa pesa nyingi sana mamilioni ya fedha. Nimesema siwezi kulinganisha lakini angalau ukiangalia shilingi milioni moja dhidi ya milioni 150? Haya ni maisha wote wanakuwa wamepoteza maisha wanaacha familia zinahangaika lakini shilingi milioni moja ya fidia hii haitoshi hata kidogo.

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara hii, shemeji yangu Kigwangalla naomba unisikilize, rudi, toeni mapendekezo, leteni hizi regulations, zibadilishwe viwango hivi viongezwe tafadhari; hiyo ni moja. Hata hivyo bei yake kwenye uharibifu wa mazao, nimejaribu kupekua sheria nimeangalia regulations na sheria zote zinazohusu wanyamapori kwenye fidia. Sasa hivi kwa mfano tumekuwa na shida sana manyoni sisi.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na shida sana, kwa mfano pale Manyoni. Manyoni tumepakana na Pori la…

T A A R I F A . . .

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwenye mazungumzo ya kawaida binadamu mnapokutana huwezi kuongea umekunja uso tu, unaongea maneno magumu, lazima uchombeze kidogo, naomba niendelee. Nimesema hiyo ni bei yake fidia hiyo ni ndogo. Nimesema fidia hiyo haitoshi, tafadhali sana leteni sheria zibadilishwe ili fidia hii iongezwe. Mnasema kifuta machozi, kwenye uhai sawa ni kifuta machozi, lakini famila inaachwa inaachwa hii. Shilingi milioni moja ndugu yangu ni kiwango kidogo sana hata hakiwezi kusemeka.

Mheshimiwa Spika, nimesema pia pili yake, mazao yanapoharibiwa ndani ya nyumba. Nimesema manyoni sisi kule unapakana na Mapori ya Mhesi na Kizigo, sasa wanyama wanahama, kiangazi mkulima amevuna mazao, ameweka ndani kwenye vihenge, amefungia ndani ya nyumba, tembo anatoka porini huko atokako anakuja anabomoa nyumba ananyanyua lile tembe la nyumba, anatafuta kihenge kiko wapi anakula mahindi yote kabisa yanaisha.

Mheshimiwa Spika, lakini nimeangalia sheria hakuna fidia. Ni bora hata yawe yameliwa porini, hiyo naweza nikasema sawa angalau, lakini mtu ameyavuna ameyaweka ndani tembo anakuja atokako anakula mahindi halafu hakuna fidia. Naomba pia turudi kwenye sheria, naomba turekebishe kipengele hicho. Kama mnyama ameingia, ameumiza mtu, amekula mazao pia hicho kipengele cha fidia kiwepo.

Mheshimiwa Spika, nisemee tatizo la mipaka kwa ufupi sana. Sisi Manyoni tumepakana na mapori mawili ya Hifadhi ya Mhesi na Kizigo kama nilivyosema. Mwaka 1994 Mhesi Game Reserve ilianzishwa, ni moja ya reserve changa kabisa ambayo ina ukubwa wa kilometa za mraba 2000. Ujio wa Mhesi imeleta kilio kikubwa sana kwa watu wa Manyoni kwa sababu kama ambavyo wenzangu wamelalamika, imeua vijiji na vitongoji vingi sana. Kwa mfano tulikuwa na vitongoji vya Chisola, Msisi, Ilowelo, Machochoroni, Mkindiria, chigugu, Ngongolelo, Chibwee na Iluma.

Mheshimiwa Spika, vijiji hivi tulikuwa tunavitumia kwa kilimo, machimbo ya dhahabu, kwa mfano Iluma pale. Ukichukua taarifa ya benki ya mwaka 1992 dhahabu inayotoka iluma ni dhahabu inayoitwa alluvial ambayo haijawahi kuchimbwa mahala popote duniani. Machimbo ya dhahabu tunajua huwa wanasaga kwenye mawe, wanatumia madawa makali, zebaki lakini ile unachimba tu unapuliza puliza lile vumbi basi unauza imeshajiunda tayari imeshaji-mould tayari, angalieni tarifa za benki za mwaka 92. Wameweka mipaka, wamezuia yale machimbo, ilikuwa ni neema kwa watu wa Manyoni. Jamani, hii mipaka hii, tuangalie upya mipaka hii ndugu zangu.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nizungumzie suala la uwekaji wa mipaka, wenzangu wamelalamika pia. Uwekaji wa mipaka tunaviziana, uwekaji wa mipaka si shirikishi kwa wananchi. Wanakuja huko watokako tunaona watu wanachimbia mambo wanaondoka, baadae inatolewa taarifa kwamba ninyi hapa mnatakiwa msiwepo maeneo haya. Jambo hili ni baya sana na limeleta mateso kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, lakini pia pili, mipaka hii haionekani. Unaenda kuchunga ng’ombe hujui mpaka uko wapi, kumbe umeshavuka uko ndani ya hifadhi yao. Kipigo kinachofata hapo kwa wananchi wetu ni kikubwa mno ndugu zangu. Manyoni haisemwi sana sijui kwa nini, lakini Manyoni kuna watu wanateseka sana kwenye hii Mhesi na Kizigo.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2016 nakumbuka ulikuja msafara wa wananchi kutoka Manyoni. Nina vijiji 12 vinavyogusana na mpaka wa Manyoni kule Mhesi na Kizigo, nakumbuka sana, ilikuwa tarehe 25 Mei, na mimi mwenyewe niliwaongoza; walikutana na aliyekuwa Naibu Waziri kipindi kile Mheshimiwa Ramo Makani, kwenye Maliasili na Utalii. Vile vile walikutana na ndugu yangu Mheshimiwa William Tate Ole-Nasha akiwa Naibu Waziri wa Kilimo na Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, tuliongea kwa muda mrefu, tukapewa ahadi ndugu zangu mwaka 2016. Hata hivyo hata ile Kamati iliyoundwa kwenda kutatua migogoro ya kitaifa ile Manyoni hata hawakugusa, sijui ni dharau, sijui ni kitu gani? Watu wametekesa sana, wamekuja kwa utiifu wao, wamekutana na Mawaziri wametoa wito na wameahidiwa kwamba Wizara itakwenda. Kamati imeenda hata hawakupita Manyoni kwamba yaani wale hata hakuna kitu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja lakini tafadhali sana, naomba sana wananchi wangu wanapigwa sana kule Manyoni, njooni tutatue tatizo la mipaka. Ahsante sana.