Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri pamoja na timu yake kwa kazi kubwa wanayoifanya. Suala zima la upandaji miti katika maeneo yetu yaliyo wazi pamoja na maeneo yaliyoungua. Niishauri Serikali yangu kuwa na mpango mkakati wa kuhakikisha miti inapandwa kwa wingi na si kupanda tu pamoja na kuitunza mpaka ikue pamoja na kuwapa miche bure. Pia kuna misitu iliyoungua katika maeneo mbalimbali ya nchi ikiwemo Lushoto.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali ikapande miti katika maeneo hayo hasa Lushoto katika Misitu ya Magamba, Shume, Gara, Irente; maeneo yote yameungua tangu mwaka 2004 mpaka sasa kumeota tu majani bila miti. Kwa hiyo maeneo haya ni muhimu sana yarudishiwe miti ya asili ili kurudisha mandhari na uoto wa asili uliopotea. Wananchi wa Lushoto wapo tayari kupanda miti isipokuwa hawana uwezo wa kununua miche hiyo. Hivyo basi niiombe Serikali itenge mafungu ya kununua miche ya miti ili kuwapa wananchi hao.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la kuungua kwa misitu hii inatokea kila wakati lakini uzimaji wa moto unategemea wananchi. Kwa hiyo, niiombe Serikali inunue ma-grader ili yakachimbe barabara maeneo ya msituni ili janga la moto linapotokea iwe rahisi kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Spika, katika zao la misitu kuna tozo zaidi ya 32. Tozo hizi zimewaathiri sana wafanyabiashara kiasi kwamba mpaka sasa mgao wanaopewa umesimama kwa sababu gharama zenyewe zimepanda, ambapo kwa square meter 100 ni shilingi 10,000,000 tofauti na mwaka 2016 – 2017 ilikuwa square meter shilingi 6,000,000 ukichanganya na hizo tozo gharama inakuwa kubwa sana ambayo haiendani na bei ya soko.

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali, zao la misitu ni sawa na mazao mengine, kwa hiyo tozo hizi zipungue kama mazao mengine ya kahawa, pamba, korosho na tumbaku kwa sababu hii imesababisha wafanyabiashara hao kununua miti kwa watu binafsi kwani huko bei ni nzuri. Changamoto yake ni kwamba wanauza miti ambayo haijakomaa na hii itasababisha nyumba zetu hatimaye kwenda na upepo maana mbao zilizoezekea si imara.

Mheshimiwa Spika, niishukuru Serikali kwa kuziacha hizi mashine ndogo za kuchania mbao ziendelee mpaka hapo zitakapoisha zenyewe. Hivyo basi nikuombe Waziri wetu utakaposimama na kujibu hoja naomba hili ulisemee kwani kuna watu wengine wamezisimamisha na kazi zao kusimama. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba tamko juu ya hili. Mashine hizo zinaitwa Dindon.

Mheshimiwa Spika, pia wafanyabiashara hao wana group lao la LMDA, hili linatoa pesa kwa ajili ya kupanda miti lakini cha kushangaza mchango huu hautambuliwi.

Wadau hawa ni watu muhimu na wanastahili kupunguziwa pamoja na kuwaangalia kwa maslahi mapana ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, niunge mkono ushauri wa Kamati kuhusu kuweka miundombinu ya barabara katika mapori ya Biharamulo, Burigi na Kimisi pamoja na vifaa vya kazi, magari, wafanyakazi pamoja na nyumba za wafanyakazi bila kusahau kuweka mazingira mazuri kwa ujumla ili kuweza kuvutia watalii wetu watakaokuja. Hivyo basi niishauri Serikali iharakishe kazi hii ili Serikali iweze kuongeza pato la Taifa kupitia mapori hayo. Pia imekuwa ni jambo la furaha sana na la kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa kujenga Uwanja wa Ndege wa Chato, uwanja huu utakuwa umepandisha hadhi mapori haya matatu, Mwenyezi Mungu ambariki sana Rais wetu kwani kazi anayoifanya ya kuwatumikia Watanzania inaonekana dhahiri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Mungu ibariki Tanzania, Mungu mbariki Rais wetu pamoja na Watanzania wote. Amen