Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Spika, nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa jitihada kubwa anazofanya za kutuletea maendeleo nchini.

Mheshimiwa Spika, sekta ya maliasili na utalii ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu. Ni vyema Serikali ikaweka mipango yake vyema ili kuhakikisha wananchi wote wananufaika kutokana na maliasili zilizopo nchini.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Morogoro Kusini lina mchango mkubwa katika kulinda na uhifadhi wa maliasili kama vile misitu ya asili, wanyamapori, hifadhi za taifa hususani Selous Game Reserve upande wa Kata ya Kisaki, mito ya maji na kadhalika. Yapo malalamiko makubwa ya baadhi ya wananchi wa Jimbo la Morogoro Kusini ambao kwa masikitiko makubwa mimea yao ya mpunga waliyolima kwenye maeneo ambayo baadae yametambulika kuwa ni ya hifadhi ya Taifa iliharibiwa kwa makusudi. Wananchi hawa waliomba waachiwe ili waweze kuvuna mpunga wao na baada ya hapo wasingelima tena maeneo hayo ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, wakati mwingine wananchi waelekezwe na kuwasaidia wanapokosea. Pia yapo malalamiko ya mifugo ya ng’ombe kuteketezwa na askari wa hifadhi. Yupo mwananchi anayedai ng’ombe wake zaidi ya 200 kuteketezwa. Barua yake ya kukumbushia malalamiko hayo ya tukio lililodaiwa kutokea mwezi Aprili, 2015 nimeletewa nakala yake ambayo nimeikabidhi kwa Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii hapa Bungeni jana tarehe 21 Mei, 2018. Naomba Mheshimiwa Waziri aweze kushughulikia malalamiko hayo na muhusika ajibiwe ipasavyo, kuendelea kukaa kimya si sahihi.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Morogoro Kusini lina maeneo mengi ya vivutio ambavyo vinaweza kutumika kuvutia watalii. Jiwe lenye umbo la matiti makubwa ya mama kwa lugha ya Kiluguru tunaita Matombo, jiwe hilo ndilo lililopelekea Tarafa nzima iitwe Matombo. Jiwe lile lipo, ninasikia ziwa lake moja limekatwa na mgeni mmoja aliyekuwa anakata mawe. Hii ni sehemu ya utamaduni na utalii, tuhakikishe historia kama hii inatunzwa na kutumika kuvutia watalii.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Bwakila Juu ipo nyumba aliyoishi chifu wa zamani wa Waluguru. Nyumba ile ingeweza kuwaleta watalii na wenye kufuatilia historia kuja na kuandika zaidi kuhusu taarifa za maisha ya chifu huyo. Barabara kutoka Bigwa hadi Kisaki ndiyo hiyo inayotumika na watalii kwenda kwenye Hifadhi ya Selous kupitia Morogoro. Miundombinu ya barabara hii si mizuri. Lazima tutambue umuhimu wa kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, TANAPA ni shirika muhimu katika kukuza na kuendeleza sekta hii ya maliasili na utalii. Misaada ya TANAPA kwa Jimbo la Morogoro Kusini bado inahitajika na kwa kweli bado haijaonekana kwa kiwango cha juu. Eneo lote la Kisaki, Sesenga na kadhalika TANAPA ingeweza kusaidia miradi yao ya maendeleo, maji, shule, barabara na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, mahusiano kati ya wananchi na askari wa hifadhi sharti yawe mazuri kwa ustawi mzuri wa nchi yetu. Naomba Serikali isimamie ili kuhakikisha wananchi wanatendewa haki.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.