Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

WAZIRI WA SHERIA NA KATIBA: Mheshimiwa Spika, na mimi nataka niungane na wale wote ambao wamewapongeza Waziri na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii kwa kuwasilisha bajeti yao. Pia niendeleze machache ya yale aliyoyasema Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, panapokuwa na sheria msingi na sheria ya zamani panakuwa na kipindi cha mpito na ni imani yangu kwamba haya yaliyotokea ni ya kipindi cha mpito. Katika kipindi cha mpito zipo changamoto za utekelezaji wa sheria na panapokuwa na changamoto kazi kubwa ya mamlaka za Serikali ni kuona ni jinsi gani kipindi hicho cha mpito kinatekelezwa na kama kuna changamoto zozote zinatatuliwa kiutawala. Kwa hiyo, nisingeenda kusema kwamba Waziri amevunja sheria, ninachoweza kusema ni kwamba kipindi cha mpito kina changamoto kati ya sheria iliyokuwepo na sheria msingi iliyokuja ili kusaidia kupata utaratibu ambao mwisho wa siku una tija kubwa.

Mheshimiwa Spika, maadam Mwanasheria Mkuu wa Serikali amesema na kwa mujibu wa Sheria ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kifungu cha 21 ushauri wake is binding. Kwa hiyo, nikiwa Waziri ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali is binding mpaka a-overcatch na maadam haja-overcatch basi huo ndio msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwenye suala hili ambalo linatugusa sisi wote nalo ni suala la mifugo inayokamatwa katika maeneo ya hifadhi. Hili kama nilivyosema ni suala nyeti, ni suala zito, ni suala ambalo huwezi kulipuuza ni lazima nikitumia lugha yako ufungue masikio mawili. Nini maana ya kufungua masikio mawili, uko upande wa sheria na uko upande wa utekelezaji wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa upande wa sheria na wewe unaifahamu hii sheria vizuri kabisa, hii sheria ni miongoni mwa sheria iliyochukua zaidi ya miaka nane kutungwa. Ilikuwa na majadiliano mengi na miongoni mwa maeneo ambayo yalizungumzwa yalikuwa eneo hili hili tunalolizungumza leo la mifugo kuingia katika maeneo ya hifadhi na kulishwa na hatua gani zichukuliwe na limeendelea kuwa hivyo. Ni kweli kabisa kifungu cha 18 cha sheria kinazuia mifugo kwenda kulishwa ndani ya maeneo ya hifadhi na kinaeleza kabisa mifugo ikikamatwa ndani ya hifadhi suala zima la kutaifishwa.

Mheshimiwa Spika, Sheria hiyo hiyo kama unakumbuka ilijadiliwa sana kwamba ziko nyakati na yako majira ambayo kweli kabisa kunakuwa na ukame uliopitiliza, malisho hayapatikani na inawezekana kabisa bila kuchukua hatua mifugo mingi ikafa. Ndio maana kwa busara ya Bunge wakati ule kwenye kifungu cha 21 kilisema; “Any person shall not serve with the written permission of the director previously solved and obtained graze any livestock in any game controlled area.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mara nyingi jambo hili limekuwa pia halijaangaliwa kwa hiyo yako mazingira kwa sababu amesema kuna maeneo watu wanaruhusiwa kuingia, kuna maeneo watu wanazuiwa. Si ajabu huko walikoruhusiwa kuingia haikuwa suala la rushwa au arbitrariness lilikuwa uwezekano mkubwa sisemi ni hivyo kwamba walipata ruhusa katika kufanya jambo hilo na ikitokea hivyo watu hao basi wametekeleza matakwa ya sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mifugo inayokamatwa kwenye kifungu cha 111 cha Sheria kinaruhusu utaifishaji wa mifugo na nisikisome kimeeleza kwa kirefu sana. Kifungu hicho hicho cha 111(4) kinaeleza wazi mifugo hii ikikamatwa inachukuliwa kuwa ni mali ya Serikali na baada ya hapo ukienda kifungu cha 114(2) kinahusu suala zima la uuzaji wa hiyo mifugo na kinasema wazi; “The value of a livestock shall be calculated on the basis of the normal price of the livestock on a sale in open market between a buyer and a seller in dependent of each other.”

Mheshimiwa Spika, lazima tukiri, eneo hili ni miongoni mwa maeneo ambayo yametatiza sana na yamewakera watu wengi kwamba mifugo imekamatwa, lakini kwenye mnada kumekuwa na mazingira yanayoonesha ama bei ilipangwa au imeuzwa kwa bei ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa kulizingatia hilo nipende kulieleza Bunge hili kwamba Serikali jambo hili imelisikia na imelizingatia. Kesi nyingi hizi ziko tayari kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ambaye kwa mujibu wa Katiba ana mamlaka ya mwisho kuhusu uendeshaji wa kesi hizi, lakini alipokea malalamiko na bango kitita ninalo la kesi moja moja. Baada ya kuzichambua kesi zote amechukua hatua zifuatazo:-

Mheshimiwa Spika, hatua ya kwanza kama nilivyoeleza kwenye bajeti ya uvuvi, ameachia jumla ya ng’ombe 553 wanaomilikiwa na wafugaji wanne na mifugo hiyo imekwisharejeshwa, na hizo kesi nne baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka kuzipitia ameamua kutokukata rufaa. Hakuona kama kuna sababu ya kukata rufaa na mara moja mifugo hiyo imeachiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jumla ya kesi tano zina rufaa katika Mahakama ya Rufani ambapo Mkurugenzi wa Mashtaka amekata rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu na nimemuomba Mkurugenzi wa Mashtaka nielewe ni kwa nini katika hizi kesi tano amekata rufaa/amekwenda Mahakama ya Rufani. Tatizo hapa siyo suala la ng’ombe, ni suala la tafsiri ya sheria iliyotolewa na Mahakama Kuu ambayo Mkurugenzi wa Mashtaka anaamini ikibaki ilivyo inaweza kuwa na madhara makubwa baadae kwa uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, pia ziko kesi nne ambazo washtakiwa wenyewe wamekata rufaa Mahakama Kuu kupinga uamuzi wa Mahakama ya Wilaya kuwatia hatiani na kutaifisha mifugo. Katika eneo hili Mkurugenzi wa Mashtaka ameahidi kukutana na watu hao na kuhakikisha kwamba rufaa zao zinasikilizwa mapema ili kuhakikisha kwamba wakishinda na kama yeye hatakuwa na sababu ya kukata rufaa mifugo hiyo pia iachiwe. Kesi hizo moja itatajwa kesho tarehe 23/5 na nyingine tarehe 30 Mei.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naamini kabisa tarehe 23/5 na 30/5 kesi hizi nne za rufaa zitakuwa zimepatiwa ufumbuzi ambao ama unaweza ukaelekea mifugo hiyo kuachiwa kama wale wenye kesi wataelewana kwamba rufaa hiyo isiendelee na Mkurugenzi wa Mashtaka akiona hana sababu ya yeye pia kukata rufaa. Kwa hiyo, ningesihi tu tusubiri hiyo kesho na tarehe 30 Mei tuone hizo rufaa nyingine nne zimekwendaje.

Mheshimiwa Spika, pia zipo jumla ya kesi 23 kati ya 27 ambazo watuhumiwa walilipa faini bila kupelekwa mahakamani na wakarejeshewa mifugo yao. Pamoja na kulipa faini ambayo ni kati ya shilingi 10,000 mpaka 300,000 lakini hata katika kesi hizo kumekuwa na malalamiko. Malalamiko hayo hatukuyapuuza na moja ya kesi iliyolalamikiwa ambayo ilielezwa kwamba mke wa mfugaji huyo alipigwa risasi na askari pori kisa alikuwa anafuatilia maeneo ya malisho na kwamba hakuna hatua iliyochukuliwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya uchunguzi uliofanyika na kupata majibu jana, taarifa hizi si za kweli kwani mama huyu alipigwa risasi na mtu ambaye sitaki kumtaja jina ambaye si askari na amefunguliwa kesi ya mauaji namba 27 ya mwaka 2017. Natoa huu mfano tu kuonesha kwamba ni lazima tufanye uhakiki wa kina ili tusimuonee mtu, lakini pia tusilee uzembe ambao unaweza kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hatua nyingine ambayo kwa kuzingatia unyeti wa jambo hili ambalo tumeona kama Serikali tulichukue ni kuhakikisha kwamba tunakutanisha wadau wote, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ofisi ya Mashtaka ya Taifa na Ofisi ya Rais TAMISEMI ili kuandaa mwongozo maalum ambao utakaotumika katika masuala yote yanayohusu mifugo inayoingia ndani ya hifadhi. Ni jinsi gani ukamataji ufanywe, ni jinsi gani mifugo hao watunzwe na jinsi gani ya kuharakisha kesi na baada ya kesi nini kitokee.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tumebaini kwamba mara nyingi mambo haya yanapofanywa kwa mtindo wa operation yanapokosa mwongozo wakati mwingine hutokea hitilafu, na hitilafu hizo ili tuzitatue basi vyombo vyote hivi vitakutana kwa pamoja na baada ya hapo tutakuwa na standard operating procedure na standard operating manual ambayo itaongoza shughuli zote zinazohusu mifugo kuingia ndani ya hifadhi na kulisha.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la ushahidi, kwa sababu moja ya sababu ambazo zimekuwa zinapelekea mifugo hii kukamatwa na kubakizwa ni ili zitumike kama ushahidi mahakamani. Naomba niliahidi Bunge lako kwamba nitatafuta mimi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuonana na Jaji Mkuu ili tuone utaratibu mwingine unaoweza kutumika katika ukusanyaji wa ushahidi na utunzaji wa ushahidi ili baadaye uweze kutumika Mahakamani bila kuvunja sheria za nchi ili tusilazimike labda wakati wote kuwa na mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkurugenzi wa Mashtaka anasema alipeleka shauri hili Mahakama ya Rufaa kuiomba Mahakama ya Rufaa iruhusu mifugo ikikamatwa na kama kesi itachukua muda mrefu iuzwe, ile fedha itunzwe ili wafugaji wakishinda warudishiwe fedha lakini wale wafugaji waliohusika walipinga utaratibu huo kwamba wangependa wabaki na wale ng’ombe wao wenyewe na sio fedha, lakini hilo nalo pia tutalijadili na mamlaka husika.

Mheshimiwa Spika, ni kweli mifugo inapobaki kwa muda mrefu ili itumike kama ushahidi, mingi inakufa na hata kesi inaposikilizwa, mifugo hiyo inakuwa imekufa na ikishinda, Serikali yenyewe inakuwa haina mifugo na wale wafugaji wanakuwa hawana mifugo. Lakini kwa sababu ni suala la Mahakama, mniruhusu tu ili mimi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali tukae tumwombe Jaji Mkuu aone ni utaratibu gani mpya unaoweza kutumika katika kutunza ushahidi bila kuwashikilia ng’ombe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni jambo ambalo lipo mikononi mwa Jaji Mkuu, siwezi kulisemea. Ninachoweza kusema ni kwamba tutakwenda kushauriana naye halafu yeye atoe maamuzi ili ikiwezekana pasiwe na ulazima wa ng’ombe kukaa hata miaka miwili wakati wanasubiri kesi ili njia nyingine itumike. Pia huwa kuna mtindo wa kuhakikisha iwapo mfugaji atashindwa ni jinsi gani Serikali ina-recover na iwapo mfugaji atashinda ni namna gani anarudishiwa fedha.

Mheshimiwa Spika, nimechukua muda mrefu kidogo kulieleza hili kwa sababu ni suala ambalo linagusa maisha ya watu, livelihood yao na ustawi wao na Serikali haiwezi kulifumbia macho, lakini kwa mujibu wa sheria ilivyo, hivi ndivyo inavyotakiwa kuwa lakini tutachukua hatua zinazostahili ili kuzikamilisha. Mara kila kesi tukayoshindwa Serikali na ambapo hatutakata rufaa, mifugo hiyo itaachiwa mara moja na pale tutakapolazimika kukata rufaa, basi tutajiridhisha kwamba zipo sababu compelling za sisi kukata rufaa ili kuhakikisha tunafanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa wafugaji, ningerudia tena kuwasihi wafugaji wasiingize mifugo katika maeneo ya hifadhi na wanapolazimika kufanya hivyo kwa sababu ya ukame uliopitiliza, basi watumie utaratibu wa sheria wa kuomba kibali na wakipata kibali hicho na masharti maalum wanaweza kulisha mifugo yao mpaka hali hiyo ya ukame inapoweza kuwa imebadilika.

Mheshimiwa Spika, mimi mwenyewe natoka kwenye kundi la wafugaji na labda ndiyo maana naweza kuonekana naongea hivi, lakini Watanzania waelewe kwamba sifanyi hivyo kwa sababu pia natoka kwenye jamii inayofuga, lakini tunajua kwamba mifugo ni muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kama wewe ni wahifadhi, maana yake pia tunajali hifadhi zilizopo kwa sababu na zenyewe ni sehemu ya maendeleo yetu. Kwa hiyo, ni lazima tuwe na uwiano kati ya uhifadhi ambao ni muhimu sana lakini pia kuendeleza sekta ya ufugaji. Nawasihi sana wafugaji kwa kiasi kikubwa kabisa wa-comply na sheria. Na sisi upande wa Serikali tutajitahidi kabisa kuhakikisha kwamba sheria iliyopo haitumiki kwa namna ambayo inaleta madhara yasiyostahili na pale kwenye vitendo vya rushwa au uzembe, tutachukua hatua haraka na tuwaombe watu watoe taarifa ili PCCB na mamlaka nyingine zichukue hatua inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.