Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii niweze kuhitimisha hoja yetu ya Wizara ya Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kutumia fursa hii kukushukuru wewe mwenyewe pamoja na Mheshimiwa Mtemi John Chenge, Mbunge na Mwenyekiti wa Bunge kwa kutuongoza vyema kwenye mjadala huu toka tulipoweka mezani mapema jana. Pia nitumie fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote kwa kujadili hotuba ya Wizara yangu kwa mwaka wa fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Spika, nitumie pia nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, Mbunge na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii pamoja na Kamati yake yote kwa kuchambua, kujadili na kutoa maoni na ushauri kwenye maeneo mbalimbali yaliyohusu utekelezaji wa bajeti ya Wizara yetu kwa mwaka wa fedha 2017/2018 na pia kutoa maoni kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha 2018/2019. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango ya maandishi lakini pia kwa michango ya kusema hapa Bungeni moja kwa moja. Kimsingi Wizara yetu imepokea uchambuzi, maoni na ushauri wao. Niwahakikishie tu kwamba tutauzingatia kwa kina na kwa uzito wake katika utekelezaji wa majukumu yetu katika siku zinazokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia binafsi niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuwa kwa kweli siku mbili za kukaa hapa mbele zimekuwa ni somo kubwa sana kwangu kwenye kazi hii ya dhamana ya Wizara ya kuwa kama Waziri kwenye Wizara ambayo nimepewa na Mheshimiwa Rais niweze kuwatumikia Watanzania wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, japokuwa michango mingine nikiri ilikuwa mikali kweli kweli, lakini nilifarijika kwamba michango hii imenipika vizuri zaidi na ninaamini baada ya leo nitakuwa Waziri mzuri zaidi kuliko ilivyokuwa juzi kabla sijasimama mbele ya Bunge lako tukufu na kutoa hoja ya Wizara yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini michango ya Waheshimiwa Wabunge imenipitisha kwenye tanuru ambalo linazidi kuongeza uwezo na umahiri wangu wa kukabiliana na changamoto zilizopo kwenye sekta hii nyeti, kwenye uchumi na maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo wahenga waliwahi kusema kwamba ili dhahabu iweze kung’ara vizuri ni lazima ipite kwenye tanuru lenye moto mkali na mimi ninashukuru sana kwa fursa ya kupita mbele ya tanuru la Bunge lako tukufu ambapo nimepikwa na kuiva vizuri zaidi tayari kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo kwenye sekta hii nyeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge waliochangia kwenye Wizara yetu jumla walifika 99 kati yao waliochangia kwa kuongea moja kwa moja hapa Bungeni ni 42 na 57 walichangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie tu kwamba maoni yao tumeyapokea na pamoja na hoja ambazo zimetolewa ufafanuzi na Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria na Mheshimiwa Naibu Waziri na nyingine ambazo nitazifafanua mimi mwenyewe hapa, naomba kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba hoja nyingine tutawasilisha majibu yake kwa maandishi kwa sababu hatutaweza kufafanua maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo yaliyoguswa na Kamati yetu ni pamoja na utekelezaji wa miradi ya maendeleo, migogoro ya mipaka na ushirikishaji katika zoezi la uwekaji vigingi, ukokotoaji wa takwimu za idadi ya watalii wanaotembelea Tanzania, utozaji wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), uwindaji wa kitalii, biashara ya wanyamapori hai, utangazaji wa utalii, ukusanyaji wa mapato, mgongano wa Sheria za Uhifadhi na sheria nyingine, hali ya jumuiya za hifadhi za wanyamapori, uingizaji mifugo kwenye maeneo ya hifadhi, uharibifu wa misitu na matumizi mseto ya eneo la Hifadhi ya Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia baadhi ya hoja ambazo zimewasilishwa na Waheshimiwa Wabunge ziligusa maeneo ya biashara ya wanyamapori hai, mradi wa umeme wa Rufiji, kurejesha Wizara ya Maliasili na Utalii sehemu ya uvuvi ili kuendeleza utalii wa fukwe, migogoro ya mipaka na ushirikishaji katika zoezi la uwekaji vigingi, mgogoro wa Pori Tengefu la Loliondo, kuendeleza utalii Kusini mwa Tanzania, wanyamapori wakali na waharibifu, uwindaji wa wenyeji, ulinzi wa maeneo ya mapito, mtawanyiko na mazalia ya wanyamapori, tozo ya pango kwenye hoteli zilizopo kwenye maeneo ya hifadhi na kodi na tozo mbalimbali kwenye sekta ya utalii.

Mheshimiwa Spika, nyingine ni kubaini na kuendeleza vivutio vya utalii, ushirikishaji kwenye uhifadhi wa maliasili, malikale na utalii, biashara ya mazao ya misitu, uwezo wa kusimamia uhifadhi wa maliasili, malikale na utalii, matumizi ya nishati ya kuni na mkaa, utangazaji utalii, maeneo ya hifadhi yaliyopoteza sifa kwa mfano Pori Tengefu la Wembele, uingizaji mifugo kwenye maeneo ya hifadhi, uendelezaji wa maeneo ya malikale na historia ya utamaduni wa makabila mbalimbali, kuimarisha mikakati ya uhifadhi wa vyanzo vikuu vya maji kwenye Mto Ruaha na mito mingine, matumizi mseto eneo la Hifadhi ya Ngorongoro na changamoto ya utawala bora.

Mheshimiwa Spika, nitaomba nitumie fursa hii sasa kutoa ufafanuzi kwenye baadhi ya maeneo mahususi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mchungaji Peter Msigwa, rafiki yangu na mtani wangu alinipiga sana hapa jana. Napenda kutumia sehemu moja kuanza kufafanua kwenye hoja yangu kwamba mimi ni kiongozi kijana, ningepaswa kuwa visionary zaidi, lakini yeye alikuwa anasema mpaka jana alikuwa hajaona chochote kipya ambacho kimeletwa na Waziri huyu kijana. Kwanza mimi sio kijana, labda nina sura tu ya ujana, lakini nilishavuka ujana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuleta kwenye attention ya Mheshimiwa Msigwa pamoja na Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote mambo machache kadhaa ambayo katika kipindi hiki cha miezi nane tumeweza kuyabuni ya kuyaanzisha na mengi yapo katika hatua mbalimbali. Pengine ndiyo maana watu wengi sana wamekuwa wakishangaa hata Mawaziri wenzangu kwamba mbona Wizara ya Maliasili safari hii inapita taratibu fulani hivi ukilinganisha na miaka takribani mitatu mfululizo iliyopita?

Mheshimiwa Spika, ukweli ni kwamba tumebadilisha sana namna ambavyo tuna-approach mambo kwenye Wizara hii toka tulipoteuliwa na zaidi tunatumia mbinu ya ku- engage wadau. Mbinu ya kushirikisha wadau pamoja na waathirika wa maamuzi mbalimbali ambayo tumekuwa tukiyafanya (multisectoral stakeholders engagement). Tunafanya sana mambo yetu kwa kushirikisha wadau.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya mambo ambayo tumeanza kuyafanya ni pamoja na kubuni Tamasha la Urithi wa Mtanzania ambalo litafanyika kila mwaka hapa nchini na kwenye maeneo yote yale ambapo Watanzania ama marafiki zetu wanaweza kupenda kufanya ambapo litafanyika mwezi Septemba wa kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, Tamasha hilo tumelipa jina la Urithi Festival. Tuliteua Kamati ya wadau mbalimbali wa media, tasnia za utamaduni, mambo ya urithi na utalii na kuwashirikisha kubuni wazo la kuwa na tamasha ambalo litautambulisha utamaduni wetu sisi kama Watanzania kwamba tuna lugha yetu ya Kiswahili, lugha zetu za asili za makabila zaidi ya 120 tuliyonayo, mila na desturi zetu, historia yetu kama Taifa na Muungano wetu wa kipekee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mambo mengi ambayo tunaweza tukaelezea kuhusu Tanzania zaidi ya kuwa na aina moja tu ya urithi ambao ni urithi wa asilia, kibailojia (natural heritage) ambayo ni ya wanyamapori, uoto na uwanda, tunaweza tukazungumza pia kuhusu utamaduni wetu kuhusu mila na desturi, historia yetu na mambo kama hayo. Kwa hiyo, tumeamua ku-designate na kuutambua mwezi Septemba kama Mwezi wa Urithi wa Mtanzania na kilele chake itakuwa ni Tamasha la Urithi Festival ambalo litafanyika kila mwaka na tutaanza kulitekeleza mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mwezi huu, mambo mengi yatafanyika ikiwemo matamasha ya ngoma za jadi, michezo ya kuigiza, matamasha ya muziki wa kizazi kipya, matamasha ya muziki wa dansi, matamasha ya filamu, matamasha ya hotuba, ngonjera na vitu vingine mbalimbali ambavyo tumekuwa tukivifanya kama Watanzania.

Mheshimiwa Spika, pia katika mwezi huu kutapikwa vyakula vya Kitanzania, menu maalum ya vyakula vya asili vya Mtanzania kwenye mahoteli yote ya kitalii. Kwa hiyo, ndiyo maana tumesema tuna-engage wadau wa sekta hii ili waweze ku-absorb na kukubaliana na mawazo haya, waweze kushiriki kwenye tamasha hili kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika mwezi huu mavazi yatakuwa ni ya Kitanzania, kama utapenda kuvaa vazi la asili ya kimwambao, vazi la Kiswahili kama alivyopendeza Mheshimiwa Mtolea na Mheshimiwa Masoud, basi utavaa hivyo na kwenye mahoteli wanaweza wakavaa hivyo. Kama utapenda kuvaa vazi la Kimasai, utavaa hilo; kama utapenda kuvaa vazi la vitenge (African prints) utavaa vitenge ama khanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, basi kwenye mahoteli yote ya kitalii, Balozi zetu, Ofisi za Serikali kutakuwa kuna mavazi ya aina hiyo kuanzia tarehe moja Septemba na lengo ni kuutambulisha utamaduni wetu, lakini pia tutapamba maeneo mbalimbali ya nchi na taswira mbalimbali za Utanzania wetu. Lengo ni kusherehekea Urithi wa Mtanzania na mwezi Septemba tumeamua kufanya hivyo. Hili ni katika mojawapo ya mawazo tuliyokujanayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia lengo letu kufanya hivi, ni kuhakikisha tunaweka fungamanisho (linkage) la utalii wa wanyamapori (wildlife), maeneo asilia na utalii wa utamaduni. Lengo ni kuongeza mazao ya utalii ili watalii wawe na shughuli nyingi wanazoweza kuja kuzishuhudia Tanzania. Matamasha ya namna hii yanafanyika South Africa na Brazil.

Mheshimiwa Spika, kuna watu wanafahamu Tamasha la Samba huko kwenye nchi za kule Amerika ya Kusini, ni maarufu sana duniani na watu wanakwenda kule kipindi hicho cha tamasha hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kusudio la kuwa na tamasha hili ni kitu kama hicho ambacho kinafanyika nchi kama za Brazil na Mexico ambapo kuna mwezi wa urithi wa nchi zao kama huu tunaozungumza hapa. Hili ni katika mojawapo ya mawazo tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, tumekuja na wazo la kuhuisha mifumo ya kukusanya mapato na mifumo ya taarifa katika Wizara ya Maliasili. Tunatengeneza mfumo mmoja unaojulikana kama MNRT Portal ambapo ifikapo Julai Mosi mfumo huu utaanza kutumika. Malengo ni kukidhi matakwa ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi lakini pia kukidhi matakwa ya maagizo mbalimbali ya viongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais hapa alipokuwa anazindua Bunge hili alisema ni lazima tubuni mbinu ya kukusanya mapato kisasa ili kuhakikisha mapato hayavuji katika sekta ya utalii. Pia ni kukidhi matakwa ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano tulioupitisha hapa mwaka 2016 kwamba tutumie mifumo ya kielektroniki kukusanya mapato ili kuongeza tija katika ukusanyaji, lakini pia ili kuongeza urahisi wa mtu kufanya malipo ndani ya Serikali hususan sisi kwenye sekta yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumetengeneza mfumo mmoja ambao ndiyo walikuwa wanauzungumza Waheshimiwa Wabunge hapa, hata leo alizungumza Mheshimiwa dada yangu na shemeji yangu, Mheshimiwa Lucy Owenya kwamba kuwe kuna dirisha moja. Sasa dirisha tunalolitengeneza ndiyo huu mfumo wa kielektroniki. Kwa hiyo, ukitaka kulipa chochote kile kwenye sekta ya utalii, kila Idara ya Serikali tutakuwa tumetengeneza fungamanisho ambapo unaweza ukalipa kupitia kwetu na wao wakapata pesa zao ili kuongeza urahisi wa kufanya biashara kwenye sekta ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kumekuwa kuna malalamiko mengi kwamba watalii wanalipa kwa mawakala huko nje ya nchi na sisi hapa pesa haziingii, lakini mtalii anakuja, alishalipia kule, hapa anahudumiwa na pesa inabaki kule nje. Ili kuondoa hiyo, tuliona tukitengeneza mfumo mmoja wa malipo wa kielektroniki ambao pia utakuwa una applications mbalimbali zikiwemo za kwenye simu, zikiwemo za kwenye mtandao tunaweza ku-capture malipo yanayofanyika nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, pia tutaweza ku-capture taarifa, Kamati yetu ilizungumzia suala la taarifa, tutaweza ku- capture taarifa kwa sababu mfumo huu tutaufungamanisha na mifumo ya Uhamiaji.

Mheshimiwa Spika, nafikiri kila mtu anafahamu jitihada zinazoendelea kule Wizara ya Mambo ya Ndani kutengeneza e-visa na e-migration systems ambazo zitakuwa zimefungwa kule, lakini sisi tutazifungamanisha na mfumo wetu ili tuweze kukusanya taarifa sahihi na kwa wakati katika sekta ya utalii. Kwa hiyo, tunakoenda, changamoto kama hizi za takwimu kutokuwa sahihi hazitakuwepo tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo tumefanya na tunaendelea kulishughulikia ni suala la kuhuisha maeneo ya makumbusho pamoja na maeneo ya mambo ya kale kwani yamekuwa katika hali duni. Tumeona mfano mzuri wa utekelezaji wa mpango huu kwenye eneo la Oldivai Gorge ambapo Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro imeingia ubia na Idara ya Mambo ya Kale, pamoja Taasisi ya Makumbusho, wamejenga kituo kizuri sana cha makumbusho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, model hii tumeona tu- amplify kwa sababu Idara ya Mambo ya Kale inapata bajeti ndogo, lakini ina maeneo nyeti yenye thamani kubwa sana kidunia ya kiutalii, tumeona tuwaunganishe na taasisi zetu nyingine ambazo zinafanya shughuli mbalimbali na zinaingiza kipato kikubwa ili waweze kuyaboresha yale maeneo ya mambo ya kale na maeneo ya makumbusho kwa ubia na hatimaye tuweze kuyatangaza kwa pamoja ukilinganisha na maeneo ya Hifadhi za Taifa za maeneo ya Mapori ya Akiba na Mapori Tengefu ili tuweze kupata wageni wengi zaidi watakaokuwa wanatembelea maeneo ya mambo ya kale na maeneo ya makumbusho.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri mkakati huu uko vizuri na tumeingiza kwenye bajeti hii. Kwa hiyo, kuanzia mwezi wa Saba, taasisi hizi ambazo zinauwezo mkubwa wa kipesa, zitaanza kufanya uendelezaji kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, eneo la makumbusho pia litaboreka na lengo ni kuongeza product za utalii (tourism products), mazao ya utalii, kwa sababu sasa hivi utalii kwa zaidi ya asilimia 80 umejikita zaidi kwenye utalii wa mambo ya wanyamapori. Sasa tunavyotanua wigo kufanya matamasha, lakini pia kuongeza makumbusho na kuboresha maeneo ya mambo ya kale, maana yake tunaongeza mazao ya utalii. Lengo letu tunapoongeza mazao ya utalii ni kumtaka mtalii anapoingia nchini akae muda mrefu zaidi.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi wastani wa mtalii kukaa hapa nchini ni kati ya siku tisa mpaka kumi. Tunataka tunavyoongeza hizi tourism products mtalii a-spend muda zaidi. Kadri anavyozidi kukaa hapa nchini ndivyo anavyozidi kutumia zaidi dola zake na ndivyo anavyozidi kuacha pesa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaongeza mazao haya ili kuongeza kipato cha Serikali. Pia kadri maeneo ya vivutio yanavyoongezeka, wananchi pia wanaoishi jirani na maeneo haya nao wanapata shughuli za kufanya, watauza baadhi ya vifaa, watauza souvenirs wataweza na wenyewe kushiriki katika uchumi mpana wa utalii.

Mheshimiwa Spika, kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano tulioupitisha mwaka 2016 palizungumzwa kutokuwepo kwa linkage kati ya sekta ya utalii na maendeleo ya watu; na ndiyo maana pengine malalamiko yanakuwa mengi dhidi ya sekta hii kwa sababu pengine kuna baadhi ya jamii zinazozunguka maeneo yaliyohifadhiwa hazioni faida ya moja kwa moja ya uwepo wa maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kadri tunavyozidi kufungamanisha sekta ya utalii na maendeleo ya watu ndivyo ambavyo hata hii migogoro ambayo inajitokeza sasa tunarajia itazidi kupungua. Pamoja na mambo mengine mengi ambayo ningeweza kuyasema, lakini kwa faida ya muda nisiyaeleze yote kwa upana, naona muda nao unanitupa mkono, inatosha tu kutaja maeneo ya misitu ya asili ambayo ilipoteza hadhi kwenye Halmashauri, kwenye vijiji tumeiwekea mkakati wa kuifufua, mkakati wa kuitengea maeneo kwa ajili ya mkaa, Mheshimiwa Naibu Waziri amefafanua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tumeanzisha utaratibu mpya wa kutengeza utambulisho wa Mtanzania (destination branding) ambapo tumetengeneza slogan ya Tanzania Unforgettable kwa kutumia wadau mbalimbali waliobobea katika eneo hili la kufanya branding. Bila shaka mmeona hata kwenye mabegi tumewapa ndiyo tunaanza hivyo kuitangaza brand yetu. Pia tutatoa print materials mbalimbali, tutatumia mitandao kuitangaza brand yetu kuanzia sasa na Tanzania kwa kweli kwa jinsi ilivyo na vivutio ambavyo ni unmatched au unparalleled, kwa hakika mtu akija hapa ataondoka na unforgettable experience. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunakusudia kuanzisha Mamlaka ya Utalii wa Fukwe, limezungumzwa hapa suala la fukwe, ni katika mambo mapya ambayo tunakusudia kuyafanya na hivyo tuta- harmonize mahusiano yetu kwenye ku-manage hizi fukwe pamoja na zile marine parks ambazo kwa sasa ziko chini ya Idara ya Fisheries iliyopo Wizara ya Mifugo ili iwe package moja kwenye hiyo sheria mpya ambayo pengine tutaileta hapa Bunge siku za usoni.

Mheshimiwa Spika, pia tuanzishe Jeshi Usu ili kuimarisha ulinzi wa maliasili zetu, lakini pia kuhuisha sheria za TAWA, TFS na kutunga kanuni mbalimbali kama kanuni za shoroba, kanuni za buffer zone, kanuni za maeneo ya mtawanyiko wa wanyamapori, lakini pia kufanya mabadiliko makubwa kwenye Kanuni za Jumuiya za Hifadhi ya Wanyama Pori (WMAs). Yote haya ni mambo ambayo tunayafanyia kazi; na tunayafanyia kazi kwa speed kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo tunalifanya kwa sasa ni kufungua corridor ya Kusini. Tunakusudia kwa kweli kufungua corridor ya Kusini na mikakati mwezangu ameigusia kidogo, nisiirudie kuelezea jambo hili.

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuridhia maombi yetu kadhaa ambayo tumempelekea ya kutaka kupandisha hadhi baadhi ya maeneo ili tukae kimkakati zaidi katika kufungua corridor nyingine kiutalii. Alizungumza Mheshimiwa Mbatia hapa. Kwa sababu tunakusudia kufikia hao watalii 8,000,000 katika miaka takribani saba iliyobakia ili tuweze kufikia malengo ya kukusanya mapato ya dola za Marekani bilioni 16 kufikia mwaka 2025, ni lazima pia tufungue maeneo mapya ya utalii. Kwa sababu maeneo ya Kaskazini yameanza kuwa exhausted, watalii wamekuwa wengi sana kiasi kwamba hata maintenance ya barabara inakuwa ngumu, kila baada ya mwezi inabidi mfanye repair ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wakati tuna vivutio vingi na vyote vina wanyama wale wale, kwa hiyo, tunafungua maeneo mengine. Hapa nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kukubali kupandisha hadhi mapori ya akiba ya Burigi, Biharamulo, Kimisi, Ibanda na Chifu Rumanyika badala ya kuwa na Mapori ya Akiba, sasa tunaanzisha mchakato rasmi wa kuyapandisha hadhi ili yaende yakawe National Parks. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, watu wa Kanda ya Kaskazini Magharibi, mama yangu Mheshimiwa Profesa Tibaijuka na mdogo wangu Mheshimiwa Innocent Bashungwa, wakae mkao wa kula, utalii unakuja Ukanda wao. Tuna-take advantage ya kiwanja cha ndege cha Chato, lakini pia kwenye bajeti hii tumeweka mkakati wa kuchonga barabara zinazoingia kwenye mapori haya ya akiba ambayo sasa tunaanzisha mchakato wa kuyapandisha hadhi yaende yakawe National Parks ili tuifungue corridor hii ya Kaskazini Magharibi kiutalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunasubiri majibu mengine kama Mheshimiwa Rais ataridhia kupandisha hadhi baadhi ya mapori yaliyopo Ukanda wa Kati na Magharibi ili tuifungue corridor ya kati Magharibi kwa maana ya kutokea hapa Dodoma kwenda Tabora kupita Katavi tuunganishe na Kigoma iwe nayo ni circuit nyingine ya kiutatalii. Mapori ninayoyazungumzia ni mapori kama Swagaswaga, Mkungunero, Rungwa, Mhesi lakini pia mapori ya Ugala kwenda mpaka mapori ya Kigosi Moyomosi ili nayo tuchague baadhi yake tuyapandishe hadhi yawe National Parks ili tuyajengee miundombinu na yenyewe yaweze kuanza kutumika kwa kasi zaidi kwa shughuli mbalimbali za utalii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nachukua fursa hii adhimu kwa kweli kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutujibu maombi yetu hayo na bahati nzuri majibu yamekuja kwa wakati muafaka, barua nimeipokea jana kwamba Mheshimiwa Rais ameridhia tuanze mchako wa kuyapandisha hadhi mapori hayo ya akiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine jipya ambalo tumekuja nalo ni kushirikisha jamii. Sisi tuna falsafa kwenye Wizara yetu kwa sasa kwamba uhifadhi endelevu ni uhifadhi shirikishi jamii na hapa tunamaanisha kwamba kwenye kila changamoto ni lazima tuzungumze na jamii na ndiyo maana nilikuwa tayari kuzungumza na wananchi wa Momela kwa mdogo wangu, rafiki yangu Mheshimiwa Joshua Nassari, lakini pia nilizungumza na Mheshimiwa John Heche.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya sana, Waheshimiwa Wabunge hata ukiwatendea wema namna gani, wakija hapa ndani wanakupiga tu. Hawazungumzi yale mema dhidi ya watu wao. Kwa mfano, Mheshimiwa Heche juzi tu hapa watu wake zaidi ya 100 walikuwa wamekamatwa wamewekwa ndani kwenye operation ambayo ilikuwa inaendelea kule. Sisemi operation ilikuwa haramu, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, operesheni ilikuwa halali, imefanyika vizuri, wananchi wameshirikishwa, ushahidi upo, kuna ushahidi wa picha, kuna ushahidi wa video, kuna ushahidi wa mihutasari ya mikutano ya kushirikisha wananchi. Katika vigingi ambavyo vilifikia idadi ya 147 kwa plan iliyokuwepo, siku wananchi wake wanafanya mgomo zoezi lisiendelee pale Kegonga, kulikuwa kumeshawekwa beacons zaidi ya asilimia 90.

Mheshimiwa Spika, zilibaki beacons 13 tu katika beacons 147. Kama kweli zoezi halikuwa shirikishi toka mwanzo, vijiji vingine vyote zaidi ya kumi vingekataa. Kilikataa kijiji kimoja tu cha Kegonga kwenye Kata hiyo ya Nyandugu ambapo wao walitaka kufanya vurugu na walidhani kwamba kulikuwa hakuna ushirikishwaji na kuna mtu mmoja pale alihamasisha vurugu hizo kutokea.

Mheshimiwa Spika, mimi pamoja na kufuatilia na kupata ukweli wa jambo lenyewe, nikatumia busara, nikasema kwamba ni vema hawa watu nitumie busara ya kuzungumza na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Spika, wewe kiongozi mzoefu unafahamu changamoto ninayoweza kuipata katika mazingira kama hayo, wakati Mkuu wa Wilaya na Kamati yake ya Ulinzi na Usalama inaendesha operation, Mkuu wa Mkoa amefanya ziara, amebariki operation iendelee, kuna timu nzima pale ya vyombo vya Ulinzi na Usalama vipo pale vinaendesha operation, halafu mimi Waziri ambaye ninashikiria sheria ambao inasimamiwa sasa na Serikali yetu kule kwenye Local Government, ninapofanya uamuzi wa kumwambia Mkuu wa Wilaya sitisha hiyo operation yako, siyo katika maslahi ya umma, na mimi Waziri mwenye sheria, naona kwa sasa haiendi sawa. Hebu sitisha mpaka nije mimi mwenyewe. Ni mazingira magumu sana.

Mheshimiwa Spika, nilikwenda extra mile kwa sababu ya urafiki wangu mimi na Mheshimiwa John Heche kwamba amenieleza hili jambo kwa hisia kali, na mimi ni Waziri, na mimi ni Mbunge mwenzake, hebu ngoja intervene kusimamisha hiyo operation na hatimaye tutatafuta suluhu mimi mwenyewe nikienda site. Nikasitisha zoezi lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikamwomba zaidi Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ambapo tayari charge sheets zilikuwa zimeandikwa kwa watu wale zaidi ya 100 na wako ndani kwamba Mheshimiwa naomba hao watu hebu watoe ili nijenge mahusiano mema na hao watu, nitakapokuja niweze kuzungumza nao vizuri wakiwa hawana kesi. Nikamshawishi Mkuu wa Wilaya na akaacha kufungua hizo kesi na waendesha mashitaka walikuwa njiani wanatoka Mkoani kwenda pale na wako kambi pale wanaendelea kuandika hayo mashtaka ili wawapeleke Mahakamani, lakini nikasitisha na zoezi la kwenda Mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado ukiwa Waziri wa Wizara hii, utapata lawama sana. Watu watasema beacon imechimbiwa chini ya uvungu, beacon imechimbiwa kanisani, imechimbiwa msikitini. Mambo mengi haya yanayosemwa kwa kweli nimekuwa nikiyafuatilia toka nimekaa kwenye kiti hiki, mengi nimekuwa nikiona siyo ya kweli.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, beacon yenye urefu wa kunishinda mimi, zaidi 6.4 feet haiwezi kukaa kwenye uvungu wa kitanda. Hizo ni beacon ndefu, lakini pia ziko beacon fupi ambazo zinanifika mimi hapa. Kwenye picha zilizokuwa zinarushwa hapa nafikiri mliona, beacons zote nilizozitembelea zinanifika hapa. Haiwezi kukaa chini ya uvungu wa kitanda. Hicho kitanda labla ni double decker ambacho chini hakina kitanda. Kwa vitanda vya ndugu zetu huko vijijini tunakotoka, ni vifupi chini. Kwa hiyo, maneno mengi yanasemwa ili kujenga hoja kwamba Wizara ya Maliasili na Askari ambao ni barbaric kweli kweli, ambao hawajali masilahi ya watu.

Mheshimiwa Spika, naomba kwanza niseme falsafa hiyo sasa tumeifuta kwenye Wizara hii. Tunashirikiana vizuri na wananchi, na mimi kama kiongozi mkuu kwenye Wizara hii napenda kushirikisha wananchi, napenda kuwa-engage wadau. Hata Mheshimiwa Heche huna haja ya kusema hapa kwa sababu kwanza nimeshakuhakikishia kwamba tutakwenda kule kwenye Jimbo lako tukaone hali halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia wewe umesema maneno mazito hapa kwamba Gibaso, boundary ile ni hard line, wananchi hapa, hifadhi hapa. Huwezi kuweka buffer zone kwenye eneo la wananchi, ni simple logic! Nikienda nikikuta hali iko hivyo, niko radhi kumshawishi Mheshimiwa Rais tufanye variation ya mipaka, niko radhi kufanya hivyo.

Kwa hiyo, mambo ya namna hiyo hayapaswi kuzua mjadala hapa kwa sababu mimi mwenyewe nitayafanya kwa mikono yangu. Nitafika maeneo husika na nitahakikisha tunaweka sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tumeanzisha pale TTB studio ya TEHAMA ambayo itaenda kutumika kwa ajili ya ku-monitor mawasiliano kila mahali kwenye mtandao neno Tanzania litakapotokea kwenye mjadala. Lengo letu ni kukusanya takwimu na kuwajua watu wanaozungumzia kuhusu Tanzania wanapatikana wapi, ni wa umri gani na tufanye nini ili kuweza kuwavutia kuja kutalii katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze la vigingi dakika mbili tu. Naomba sana Bunge lako tukufu lisisitishe zoezi hili. Nasema kwa sababu ifuatayo kubwa moja.

Mheshimiwa Spika, tunaweka vigingi ili tujue nani na nani wameingia ndani ya eneo la hifadhi. Kama ni hifadhi imeingia ndani ya eneo la wananchi tujue. Halafu mahali palipo na mgogoro tunatatua. Kwa mfano nilikwenda Kimotorok kwa ndugu yangu Mheshimiwa Millya, nikafika pale, nikajionea, kweli kuna vigingi, kuna makanisa yako ndani ya hifadhi na kituo cha afya kimo ndani ya hifadhi. Katika maeneo kama haya, mimi binafsi niko radhi kumshawishi Mheshimiwa Rais turekebishe mipaka, vitu kama hivi vitoke. Kwa sababu ni eneo ukakuta labla ni la kilometa moja, ni eneo dogo tu ambalo tunaweza tuka-coincide tukasema hili tulirudishe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mchakato wake utaanza, lakini ni lazima Waziri uanzishe huo mchakato. Kama mipaka haijawekwa au vigingi havijawekwa nitajua kipi na kipi kimeingia na kipi kipo ndani na kipi kipo nje? Kwa hiyo, zoezi liendelee, Waheshimiwa Wabunge mtupe ushirikiano na wananchi wenzetu watupe ushirikiano tukamilishe zoezi la kuweka vigingi, lakini tukijua kwamba hiyo siyo final, hiyo siyo hatua ya mwisho.

Mheshimiwa Spika, askari wanaolinda hizi hifadhi wasisumbue wananchi wala wasitumie nguvu kulazimisha vigingi kuwekwa ama kuwaondoa katika hatua hii ya kwanza. Wananchi wabaki katika maeneo hayo, tutatatua mgogoro mmoja baada ya mwingine kwa kufuata harama za vigingi ambazo zitakuwa zimeshawekwa. Naomba hili pia niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo bila kuchukua sana muda wako, nitakwenda Arumeru mimi mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.