Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Waziri, Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Suzan Kolimba na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuendelea kuiweka Tanzania katika ramani ya dunia kwa masuala ya uhusiano wa Kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, napenda kuendelea kuipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa kazi nzuri na kubwa ya kuijenga Tanzania ya viwanda na maendeleo ya uchumi wa kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi naomba sasa nichangie hoja ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ipatie kipaumbele haja ya kurekebisha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuruhusu raia wake kuweza kuwa na uraia pacha (Dual Citizenship). Nionavyo kuna faida kubwa kuliko hasara kama Watanzania wanaopenda kuwa na uraia wa nchi mbili watahalalishwa kufanya hivyo, kwani kwa kufanya hivyo, tunajiongezea fursa za kiuchumi na kijamii, hasa kwa Watanzania wenzetu wanaoishi na kufanya kazi nchi za nje (The Diaspora Community).

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Itifaki ya Soko la Pamoja la Afrika ya Mashariki. Ingawa hotuba ya Waziri inatamka bayana katika ukurasa wa 28, aya ya mwisho kuwa, wananchi na hasa vijana washiriki katika kuchangamkia fursa zilizoko kwenye soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki, hali ilivyo sasa kwa wasafiri wanaotumia Hati za Dharura za kusafiria siyo rafiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, zamani Hati za Dharura za Kusafiria zilikuwa zinatolewa kwa kuruhusu kutumika kwa multiple entries kwa muda wa mwaka mmoja, lakini kwa sasa na kwa sababu ambazo wananchi wanaosafiri mara kwa mara kwenda na kurudi katika nchi jirani zetu Afrika Mashariki hupewa hati za dharura ambazo zinaruhusu single entry visa tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kumaanisha kuwa, mara msafiri anapopita kwenda nchi ya jirani, mfano Kenya, kwa wajasiriamali wa mpaka wa Kenya na Tanzania, Namanga, ambao hufanya biashara katika masoko ya nchi jirani kila wiki hulazimika kukata hati mpya ya dharura ya kusafiria kila trip hata kama atasafiri kwenda na kurudi kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili siyo rafiki kwa uchumi wa wananchi na vijana wanyonge ambao Itifaki ya Soko la Pamoja ililenga kuwasaidia. Gharama ya hati kwa kila safari ni wastani wa Sh.20,000/= na kama msafiri atahitaji kwenda Kenya mara tano kwa mwezi, kwa mfano, atalazimika kutumia hadi Sh.100,000/= kwa hati ya kusafiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri na kuiomba Serikali watengeneze mazingira rafiki ya ama kurejesha Hati za Dharura ambazo ni valid for multiple entries for one year au utoaji wa Pasi za Afrika Mashariki urahisishwe na kuwezekana kutolewa mpakani tofauti na sasa ambapo ni mpaka maombi yapelekwe Dar-es-Salaam na kuchukua zaidi ya miezi sita mpaka msafiri apate pasi hiyo, au ikubalike sasa kuwa, Watanzania waruhusiwe kusafiri nchi za Jumuiya yetu kwa kutumia vitambulisho vyao vya Kitaifa tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.