Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu katika Wizara hii muhimu ambayo ni kioo cha nchi yetu katika uso wa kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema na ukarimu kwa kuendelea kutupa ruhusa ya kupumua pamoja na maudhi tunayomfanyia kama binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo naanza na mchango wangu kwa kujielekeza hasa katika ukurasa wa 14; kuhusu Diplomasia ya Uchumi. Tanzania tunategemea kilimo kwa chakula, ajira, biashara na malighafi, lakini tatizo kubwa ni masoko ya uhakika na yenye bei nzuri na tija kwa wakulima wetu. Kwa mfano, zao la mbaazi kukosa soko mwaka jana 2017/2018 na bei yake kuanguka kutoka 2,000 ya mwaka 2016/2017 na kufikia 150 kwa kilo moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii imeathiri uchumi wa Taifa na kipato cha wakulima wetu na kusababisha hasara kubwa. Pia imeleta madeni katika taasisi za fedha zikiwemo benki na SACCOS ambako waliwalichukua mikopo kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa mbaazi kuzingatia bei nzuri na ushindani wa soko kwa msimu wa mwaka uliopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ina ardhi kubwa na faida ya kijiografia katika mikoa mingi katika uzalishaji wa mbaazi ikiwemo Morogoro, hasa Morogoro Vijijini, Kilosa, Turiani na Ifakara na mikoa mingine kama Arusha, Manyara, Shinyanga, Pwani, Lindi na Mtwara ambayo ilikuwa inatoa ajira, chakula na kuongeza vipato vya watu wetu; ukizingatia kwamba zao hili la mbaazi kilimo chake hakina gharama kubwa na usumbufu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao hili si la kupuuza na kuliacha kwa sababu lina fursa nyingi za kiuchumi, lakini tatizo kubwa ni soko lake, kwamba linategemea jamii moja tu na sehemu moja ambayo ni India. Kutokana na kutegemea soko moja wakulima wetu wanaathirika zaidi kwa sababu mabadiliko yoyote ya sera ya soko hilo au uzalishaji mzuri wa mbaazi wa India kunaathiri soko la mbaazi la wakulima wetu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina ushauri katika Wizara hii katika Diplomasia ya Uchumi kutafuta soko la mbaazi kabla ya msimu kuanza katika nchi ya India na hasa mnunuzi mkuu ambaye ni Serikai ya India ili kuwa na uhakika wa soko na bei nzuri kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuishauri Serikali kuingia mkataba wa ununuzi na Serikali ya India kutoka kwetu kwa bei ya kiasi ili kutumia vizuri Diplomasia ya Uchumi na kuongeza fedha za kigeni na kipato kwa wakulima na kuepuka hasara kama mwaka jana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.