Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati

Hon. Jamal Kassim Ali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Magomeni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati

MHE. JAMAL KASSIM ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Awali ya yote niungane na wenzangu kuipongeza Serikali na hususani Wizara yetu hii kwa jitihada kubwa ambayo wanaifanya katika kuhakikisha nchi yetu inapata umeme wa kutosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika hotuba leo nitachangia maeneo mawili. Eneo la kwanza nitaanza kuchangia suala la TAENESCO. Kusema ukweli kwa takribani kipindi cha miaka 10 sasa Shirika letu la Umeme la TANESCO halifanya vizuri kifedha. Ukiangalia hesabu zake za fedha kwa takribani miaka 10 shirika letu hili lilikuwa linajiendesha kwa hasara. Hii nini maana yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwamba tutoke kwenye kuwa Taifa la chini kwenda kuwa Taifa lenye uchumi wa kati na hatuwezi kuwa Taifa la uchumi wa kati kama hatuna viwanda na hatuwezi kuwa na viwanda kama hatuna umeme wenye kutosheleza na uhakika. Hatuwezi kuwa na umeme wa uhakika na wa kutosheleza kama hatuna Shirika la Umeme imara kifedha na kiufanisi. Ukiangalia hesabu zetu hizi za TANESCO inaonesha kabisa ipo haja ya kufanya mabadiliko makubwa ya kiutendaji ndani ya shirika letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hili limeongelewa sana. Mwaka 2002, Mercado Energético Company ya Argentina ilifanya stadi ya Shirika la Umeme la TANESCO na mapendekezo yake yakawa ili shirika hili liwe la ufanisi lazima unbundling ifanyike, tuwe na kampuni ya generation, tuwe na kampuni ambayo itasimamia masuala ya transmission na tuwe na kampuni ambayo itasimamia masuala ya distribution. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, mwaka 2003 Consultancy Company ya Marekani nao walifanya utafiti wa Shirika la TANESCO wakaja na mapendekezo hayo hayo. Sio hayo tu, mwaka 2005 iliundwa Presidential Team on Privatization Review of Utility ikiongozwa na Profesa Chijoriga nao walipendekeza hayo hayo. Mwaka 2014, Price Waterhouse Coopers waliajiriwa wafanye study ya Shirika la TANESCO nao walipendekeza hayo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niishauri Serikali baada ya mapendekezo ya Price Waterhouse Coopers wakaja na mpango wa miaka 11 wa Electricity Supply Industry Reform Strategy Roadmap ambao ulikuwa ni mzuri kabisa ulitafsiri mapendekezo yote ambayo washauri elekezi na hizi timu ambazo ziliundwa kuyaingiza katika utekelezaji lakini mpaka leo hii kimya. Ukiangalia taarifa za CAG za hesabu za TANESCO kuanzia mwaka 2010 TANESCO ilipata hasara ya shilingi bilioni 47, mwaka 2011 ilipata hasara ya shilingi bilioni 43, mwaka 2012 ilipata hasara ya shilingi bilioni 178, mwaka 2013 ilipata hasara ya shilingi bilioni 467, mwaka 2014/2015 ilipata hasara ya shilingi bilioni 124.5, mwaka 2015/2016 imepata hasara ya shilingi bilioni 346. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi reform sio sisi wa kwanza wenzetu wa Kenya na Uganda walifanya. Mwaka 1996 Kenya walikabiliwa na changamoto kama zetu, Shirika la Umeme la Kenya lilikuwa moja tu mwaka 1996 wakali-unbundling wakawa na shirika ambalo linasimamia masuala ya uzalishaji, shirika linalosimamia transmission na shirika ambalo linasimamia masuala ya distribution. Nini hatima yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Kenya leo hii wana- realize matunda ya reform yao. Mwaka 2015 taarifa za ukaguzi wa Shirika la Umeme la Kenya (KPLC) zimeripoti faida ya Kenya shilingi 7.56 bilioni, mwaka 2016 faida ya 7.2 bilion Kenya shilingi, mwaka 2017 faida ya 7.27 bilioni Kenya shilingi na miaka yote wamekuwa wanagawa gawio kwa Serikali. Mwaka jana wameweza kugawa gawio la jumla ya shilingi milioni 493 Kenya shilingi kwa Serikali lakini leo hii Shirika letu la Umeme la TANESCO bado linategemea lipewe pesa na Serikali kijiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika na Uganda hivyo hivyo. Uganda mwaka 1999 walikuwa na hali mbaya zaidi kuliko ya kwetu lakini wakafanya reform. Leo hii ni aibu Uganda walitoka kwenye vita miundombinu yote ya umeme ilikufa lakini leo hii Shirika lao la Umeme linazalisha faida. Mwaka jana tu waliweza kuzalisha faida shilingi bilioni 100 za Uganda na kugawa gawio bilioni 57.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Wizara iniambie kwa vile ina mpango, huu mpango upo na ni mpago wa Wizara kabisa ina kugugumizi gani kuufuata? Mwaka huu katika ule mpango ilikuwa Shirika letu la Umeme la TANESCO liwe unbundling tuanze hizo reform. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up aje aeleze tatizo ni nini, kwa nini hatuendi kwenye mpango ambao tayari Serikali iliukubali na kuupitisha na kwa nini mpaka leo haujatekelezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka kuchangia ni suala la mauziano ya umeme baina ya TANESCO na Zanzibar. Kusema ukweli kwa kipindi kirefu sasa hili suala limekuwa vuta nikuvute.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakubaliana nami kwamba kuna tatizo kubwa baina ya biashara hii ya umeme kati ya TANESCO na upande wa Zanzibar yaani ZECO, muda mrefu sana wamekuwa wakirumbana kuhusu bei stahiki ya kuuziwa umeme na muda mrefu sana hili suala halijapatiwa ufumbuzi. Nimshauri Mheshimiwa Waziri, theory zote za upangaji bei ya umeme zinaelekeza kwamba jambo la kwanza bei ya umeme itapangwa kwa kuzingatia gharama za kuufikisha umeme kwa ngazi ya mteja husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar inachukua umeme katika level ya transimision line 132Kv. Gharama za kuufikisha umeme katika 132Kv ni ndogo kuliko kufikisha umeme katika medium voltage na low voltage. Ukiangalia bei ya umeme ambayo Zanzibar imekuwa inauziwa haiwiani kabisa, kwanza Zanzibar ni bulk purchaser lazima preferential treatment ambayo ipo, ukienda South Africa kuna bulk purchaser ambao wao wanapewa preferential treatment na sehemu nyingine mbalimbali duniani ukiachilia mbali suala la kwamba gharama za kuufikisha umeme katika 132Kv ni ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia bei ambayo Zan- zibar inanunua umeme, naomba nisome, unity moja ya KVA Zanzibar inanunua kwa Sh.16,550, wakati wateja ambao wapo katika media voltage ambapo gharama ya kupeleka umeme katika media voltage ni kubwa wanauziwa na TANESCO hiyo hiyo unity moja kwa Sh.13,200. Hili si sawa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua Kenya, nadhani nichukue na Kenya Mheshimiwa Waziri aone mteja wa high voltage anachajiwa Sh.4,900 za Kenya wakati mteja wa low voltage anachajiwa Sh.6,000, umeona? Kwa hiyo, hapa suala la umeme na bei inayouziwa Zanzibar si sawa na haya madeni hayatokaa yalipike kwa sababu hili tatizo la bei ni kubwa ambalo linaathiri Shirika la Umeme la Zanzibar kulipa madeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru kwa kunipa nafasi.