Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Kumi na Moja wa Bunge

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Kumi na Moja wa Bunge

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kupata japo dakika chache kuzungumza juu ya mchango uliotolewa hapa na Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Sheria Ndogo, Mheshimiwa Mtemi Chenge. Kwa hakika nampongeza sana hasa kwa jinsi anavyotuongoza sisi, lakini pia yeye amekuwa mwenye msaada mkubwa kwa sisi wanasheria kuendelea kutusaidia kuelewa nini maana ya sheria katika uhalisia wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu waliotangulia wameeleza mengi na kwenye taarifa yetu ya Kamati tumeeleza mengi. Nataka nijikite katika mambo makuu mawili kama siyo matatu kama muda utaniruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza kabisa ni mahitaji ya kuwa na rasilimali watu ya kutosha katika Ofisi ya Attorney General. Haya yote yanayolalamikiwa hapa kama umesikiliza vizuri wengi wao wamejikita sana katika hoja kubwa ya uandishi wa sheria. Yapo maeneo mengi, tukitaka kuyaelezea hapa unaweza ukachukua muda wote uliobakia.

Naomba nizungumze kwa uchache zaidi, kwa mfano ukifungua ukurasa wa 7 na wa 17 kuna tatizo kubwa sana la uandishi unaojichanganya. Waandishi wetu wa sheria wanapenda kufanya reference ya vitu ambavyo havifanani na hizo sheria zenyewe, wameeleza hapa waliotangulia. Kwa mfano mmoja kwamba kuna mtu ameandika ana-refer Sheria ya Traffic ambayo ukiangalia sheria yenyewe kinachotambulishwa sicho ambacho kimeelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, majedwali mbalimbali ambayo wameyaweka kwa mfano katika ukurasa wa kwanza kwenye ile Sheria ya Usimamizi wa Mapato ya Gesi (Oil and Gas) unaona kabisa kwamba Waziri wa Fedha anapewa mamlaka ambayo mamlaka yale kwa utaratibu wake yalivyo hayatambuliki katika sheria inayoelezea juu ya usimamizi wa makusanyo ya mapato yanayotokana na oil and gas.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunachosema ni kwamba hapa hakuna mtu anayetaka kupambana na Serikali au kuivuta Serikali, lakini basi waandishi wetu mnapofanya nukuu hizo muwe makini katika kitu gani ambacho mnaki-refer, isije kuwa baadaye mkaonekana kama vile kwamba ni watu makanjanja ambao hamjui hata mnalolitenda. Ndani ya ukurasa wa 10 katika Sheria Ndogo ya Mining Local Content nayo pia kosa hilo linajitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo mengi sana ya kueleza, lakini siyo hilo tu pia iko shida nyingine ya kutotekeleza kwa yale ambayo tumekuwa kila siku tunaeleza. Siyo mara ya kwanza Kamati inaleta mbele yako mapendekezo juu ya kazi ambayo imekwishafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unakumbuka katika taarifa yetu iliyotolewa miezi sita iliyopita tulieleza juu ya watu wetu kutokuwa makini juu ya uchapishaji wa sheria hizi ndogo. Kama unakumbuka vizuri tulieleza hapa iko sheria ambayo inaeleza kwamba watu wa Kahama katika barabara zao au katika nyumba zao mbele waweke pavement blocks.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulieleza kwa masikitiko makubwa kwamba ziko sheria ambazo zimetungwa Dar es Salaam, wakafanya copy and paste wakazipeleka katika maeneo mengine, lakini matatizo hayo yanaonekana yanaendelea kujitokeza na bado shida imekuwa kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Sheria ya Electronic and Postal Communication Act iko lugha ambayo imeelezwa mle ndani ambayo watu wengi hata kwenye kamati tuliijadili sana juu ya kitu kinachoitwa sim swap, lakini unavyoona mpaka leo hii mambo bado yameendelea kuwa vilevile. Tunachokiomba ni kwamba Wizara au Serikali ichukulie mawazo yale kama ni mawazo sahihi na kama kuna maeneo ambayo wanatakiwa kuyaweka sawa basi ni vyema tukaelezana katika mikutano ya Kamati inapokutana na Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo, yako mambo mengine ambayo nayaona ni kwamba kwa tafsiri yangu ni mambo ya kutozingatia weledi tu, yako mambo ambayo yanaweza yakarekebishwa hata ndani ya ofisi. Ameeleza hapa Mheshimiwa Halima Mdee, lakini pia wameeleza waliotangulia hasa juu ya uandishi mbovu wa kutojua kupangilia vipengele na vifungu vya kisheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi yangu naiomba sana Serikali iendelee kuamini kwamba wanao muda wa kutulia na kujipanga vizuri na wakatengeneza kitu ambacho kitakapokuja kwetu sisi tuwe na sehemu ndogo ya kuongezea nyama na siyo kufikia sehemu ya kuonesha kabisa kwamba hakuna kitu kilichofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza mwanzo, mengi yameelezwa na wenzangu, lakini pia katika hotuba yetu ya Kamati tumejaribu kuchambua kwa undani zaidi na kueleza yale ambayo tumeweza kuyafikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nitumie nafasi hii kupongeza tena Kamati yetu, lakini pia kuendelea kuwatia moyo Serikali waendelee kuchukua yale ambayo Kamati inafanyia kazi kwa sababu sisi Kamati inafanya kazi kwa niaba ya Bunge na unaposema kwa niaba ya Bunge tunamaanisha kwa niaba ya wananchi wote wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja tuliyotoa, lakini pia naendelea kuunga mkono hoja zote zinazotolewa. Ahsante sana.