Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kutoa mchango wangu kuhusiana na hoja hii iliyoko mbele yetu.

Kwanza kabisa napenda niwapongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wanafanya kwenye Wizara hii ya Fedha. Nimegundua kwamba Waziri wa Fedha kwenye nchi kama ya kwetu ni kazi kweli kweli lakini Mheshimiwa Waziri na Naibu wake pamoja na watalaam wake wanajitahidi sana kufanya kazi ili kuonesha kwamba Taifa hili na nchi hii tunataka kwenda mahali, hongereni sana Mheshimiwa Waziri. Utapata majina mengi sana, bahili, msimamo mkali na mambo mbalimbali, lakini ninavyojua Waziri wa Fedha lazima awe bahili na lazima awe na msimamo vinginevyo mambo hayatakwenda. Hawezi kuwa Waziri wa Fedha ambaye ni Waziri anayegawa gawa tu, Waziri anayetewanywa tu, haiwezekani. Kwa hiyo, hongereni sana na endeleeni kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja iliyo mbele yetu ambayo naiunga mkono, nilikuwa najaribu kuangalia mambo ambayo yameandikwa humu, nataka nizungumze mambo machache tu.

Mheshimiwa Spika, kipengele cha kwanza ambacho nakiona ni nakisi ya bajeti yetu. Kwenye kitabu chako Mheshimiwa Waziri umesema mwaka 2016/2017 nakisi ya bajeti yetu ilikuwa asilimia 1.5, lakini mwaka 2017/2018 nakisi ya bajeti yetu imeongezeka imefika aslimia 2.1. Sasa kuongezeka kwa nakisi hii siyo kuzuri sana, labda niseme tu kwamba nakisi ya bajeti inapoongezeka maana yake ni kwamba matumizi ya Serikali ni makubwa kuliko kipato chake maana yake tuna kipato kidogo, matumizi yetu ni makubwa.

Mheshimiwa Spika, sasa kama matumizi ni makubwa maana yake Serikali, lazima itafute namna ya kufidia pesa zilizopungua na namna mojawapo ambayo Serikali huwa wanafanya ili kufidia pesa zilizopungua ni kukopa kwenye benki zetu. Sasa nakisi ikiwa kubwa maana yake Serikali italazimika kukopa kwenye mabenki au maeneo mengine lakini hasa kwenye benki. Sasa Serikali ikienda kukopa kwenye benki maana yake inaanza kushindana na sekta binafsi kukopa na wakishinadana hawa watu tunajua matokeo yake.

Mheshimiwa Spika, riba ya benki itapanda lakini pia kwa sababu Serikali ni mkopaji mzuri, kuna uwezekano mkubwa kabisa sekta binafsi ikapata pesa kidogo za kukopa kutoka kwenye benki. Sasa kama engine ya uchumi wetu ni sekta binafsi na Serikali inakopa kiasi kikubwa kutoka kwenye benki. Utakuta kwamba mitaji ya sekta binafsi itapungua kwa hiyo, uwekezaji kwa ujumla utapungua kwa sababu watu binafsi hawawezi kukopa kutoka benki zetu kwa sababu wanashindana na Serikali iliyo na urahisi wa kukopa kwa sababu inaaminika zaidi.

Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana kwamba suala la nakisi ya bajeti yetu Mheshimiwa Waziri uliangalie namna linavyokuwa na inawezekana kwa viwango inavyotakiwa haijawa kubwa sana lakini kama litaendelea kukua, nakisi hii itaendelea kukua, italeta shida huko baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la Ofisi ya Mipango ambalo limezungumziwa pia na wenzangu wengine. Ofisi ya Mipango ni ya muhimu sana kwenye Wizara ya Fedha lakini wenzangu na sisi kwenye Kamati tumependekeza ni vizuri ikiwa chini ya Rais. Ninavyojua ni kwamba mipango inatangulia haya mambo ya bajeti kwa sababu bajeti maana yake unaweka pesa kwenye mipango sasa kama mipango tutaipa kisogo, nashindwa kuelewa kama tunaweza kuwa na bajeti zilizo nzuri au zilizo sawa sawa. Kwa hiyo, ninasihi kabisa kwamba Ofisi ya Mipango na lile Fungu la Mipango Namba 66 ni vizuri likarudishwa, ili ya kwamba tuwe na Ofisi ya Mipango iliyo imara, Ofisi ya mipango ambayo ni forward looking itakuwa inaona mambo kwa mbali ya nchi yetu kuliko tukiwa tu na kaofisi kamipango ambako kamefichwa mahali na pengine hakana autonomize sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilikuwa naomba kwamba, ofisi ya Mipango na fungu lake likae sawasawa na kama tulivyopendekeza basi ibaki Ofisi ya Rais ili tuwe na mipango iliyo sawa sawa na kwamba baada ya kuwa na mipango sasa tunaweza kuwa na bajeti zinazotabirika na tunaweza kuwa na shughuli ambazo zinaeleweka. Lakini tukiweka nguvu tu kwenye matumizi au kukusanya kodi sasa pesa tukizipata tunazipeleka wapi? Maana hatuna mipango ambayo imewekwa sawa sawa.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la tatu la malipo kwa watoa huduma na wakandarasi. Wenzangu pia wamelizungumzia suala hili kwa kweli lina shida kidogo hasa kwenye malipo yake. Kuna ukawizaji mkubwa sana wa kulipa watoa huduma na wakandarasi hasa wa ndani na hii ina athari kubwa tu, hasa wa ndani. Ninaelewa umuhimu wa kuhakiki madeni hasa yanapofika kuwa ni madeni ya muda mrefu, ni muhimu sana kuyahakiki kama Wizara nawapongeza ni sawa myahakiki kwa sababu lazima ujiridhishe na kile unacholipa.

Mheshimiwa Spika, wazungu wanasema in God we trust, in money we audit. Kwa hiyo, lazima tuhakikishe malipo yanayolipwa yanaridhisha, yana thamani ya pesa tunazotaka kulipa. Kwa hiyo, juu ya suala la uhakiki mimi nawaunga mkono kabisa, lazima mhakiki kabla hamjalipa malipo. Lakini tuwalipe basi hao watu baada ya kuhakiki. Maana sasa huu uhakiki unapochukua baada ya mwaka mmoja, miaka miwili kwa kuwa unakuwa uhakiki ambao hauaminiki aminiki au na wahakiki hawa basi na wenyewe wapelekewe wahakiki wengine kwa sababu vinginevyo kwa kweli watu haturidhiki kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia namna tunavyolipa haya madeni ya wakandarasi na watoa huduma. Kwa nini tusilipe watoa huduma na wakandarasi wengi angalau, badala ya kumlipa mtu mmoja, mkandarasi mmoja mnalipa bilioni 200 na pengine huyo mkandarasi ana ushirika na mtu wa nje, sehemu kubwa pesa inatoroka kwenda nje haizunguki hapa ndani.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana naunga mkono hoja.