Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uamuzi wake wa Kuendeleza Mji wa Dodoma na Kuupa Hadhi ya Jiji

MHE. ZUBEIR M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja hii iliyoko mbele yetu. Awali ya yote niseme kwamba siungi mkono hoja hii kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sijaelewa kipi kitatangulia? Hivi ni vigezo vinatangulia kuwa Jiji au Jiji ndiyo linatangulia halafu vigezo vifuate? Kwa sababu ukiangalia azimio hili, aya ya pili ya Mheshimiwa mtoa hoja anasema, anaiomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya miundombinu ya kuboresha Dodoma. Sasa sijaelewa kwamba ina maana yeye anakubali kwamba bado hatujafikia vigezo vya Dodoma kuwa Jiji. Kwa hiyo, anaiomba Serikali sasa itenge fedha ili Dodoma iwe Jiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeunga mkono hili azimio kama Mheshimiwa Rais angetamka kwamba nataka kufikia mwaka 2020 – 2025 Dodoma iwe Jiji. Ndiyo maana nasema sasa Serikali ijipange kwamba Dodoma iwe Jiji. Kwa nini nasema hivyo? Kwa sababu ninavyofahamu, Dodoma kuwa Jiji tayari ni mradi. Tayari inatakiwa bajeti itengwe kwa ajili ya Dodoma kuwa jiji. Hii ndiyo sababu leo hii hata kuhamia Dodoma. Tulihamia hivi hivi, kuhamia Dodoma ni mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako lilitenga bajeti ya kuhamia Dodoma? Leo hii Bunge limetenga bajeti kwa ajili ya Dodoma kuwa Jiji? Sasa mambo yote haya, hakuna mtu anayepinga Dodoma kuwa Jiji, lakini Mheshimiwa Rais angetamka kwamba nataka kufikia mwaka 2020 au 2022 nataka Dodoma iwe Jiji halafu miundombinu ifuate, kama ambavyo mtangulizi wangu alivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Dodoma hatuna stand, leo hii uwanja wa ndege uko mjini pale, wala haufai. Tunahamishia wapi? Tunahamishia Msalato; stand ya bodaboda na kadhalika tunahamishia Nanenane. Maana yake ni kwamba tunataka tutengeneze miundombinu ili Dodoma iwe Jiji...

T A A R I F A . . .

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na taarifa yake siipokei. Nilichokiongea ni kwamba vigezo vitangulie kabla ya kutangazwa kuwa Jiji. Dar es Salaam anayoisema ni kwamba ilitangulia vigezo vya kuwa Jiji. Ile inayoendelea sasa hivi pale ni nyongeza tu. Hatuna maana kwamba Dodoma itakapojengwa kuwa Jiji, hiyo miundombinu ikikamilika haitaendelea tena kujengwa. Maana yake ni kwamba miundombinu itakuwa inaboreshwa kila wakati. Ninachokisema na ndiyo maana CDA ilivunjwa, kwa sababu haikutimiza malengo yaliyokuwa yamekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Kwanza tangu mwaka 1973 alitangaza kwamba Makao Makuu ya nchi hii iwe Dodoma, lakini akaunda na mamlaka ile ya CDA. Kwa sababu CDA hawakufikia vigezo na ndiyo maana Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano akaja akaivunja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda niseme kwamba Bunge lako tukufu ili liweze kuunga mkono hoja hii, basi kauli hiyo ibadilishwe kwamba Mheshimiwa Rais ametamka kwamba kufikia mwaka fulani, Dodoma inatakiwa iwe Jiji. Leo hii Dodoma bado haijakidhi vigezo kuitwa jiji. Kama tukiamua kuweka jiji kisiasa, twende tuliweke jiji kisiasa, lakini vigezo bado havijakamilika.