Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE.DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Nianze kwa kuunga mkono hoja. Pili napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wa Wizara hii ya Fedha kwa bajeti nzuri yenye mwelekeo wa kuipeleka nchi yetu Tanzania katika hadhi ya uchumi wa kati mwaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa mkakati wa ujenzi wa viwanda ili nchi yetu iweze kujikomboa kutoka kuwa nchi tegemezi kwa karibu kila kitu na kuelekea katika hadhi ya uchumi wa kati nchi yenye uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza mpango wa kutenga maeneo maalum ya uwekezaji EPZ na SEZ. Uwekezaji katika maeneo haya utachochea sana maendeleo ya viwanda katika nchi yetu hususani maendeleo ya viwanda ambayo yana mpangilio mzuri na yanawezesha kulinda mazingira na kusaidia ukuaji wa miji yetu katika hali nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Bagamoyo Serikali imetenga hekta jumla ya 9,080 kwa ajili ya viwanda, eneo maalum la EPZ katika jimbo la Bagamoyo. Awamu mbili zilifanya hivyo, awamu ya kwanza jumla ya hekta 5742 na EPZ awamu ya pili jumla ya hekta 3388. Katika EPZ awamu ya kwanza ilitathiminiwa mwaka 2008, wafidiwa 2,180 kwa thamani ya shilingi bilioni 60, lakini mpaka hii leo mwaka 2018 kwa maana baada ya miaka 10 baadaye, wafidiwa 1,025 bado hawajalipwa fidia yao, jumla ya shilingi bilioni hamsini na moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumwambia Mheshimiwa Waziri kwamba, fidia ni mazingira wezeshi ya viwanda, kwa maana unapolipa fidia ardhi ile sasa inakuwa huru ili mwekezaji aweze kuwekeza viwanda. Kabla hujafanya hivyo maana yake mazingira yale si wezeshi tena. Pia inamuwezesha mwananchi wa kawaida kuweza kujenga upya maisha yake, kumudu kukimu familia na kuweza kuhakikisha kwamba anafaidika na eneo lile ambalo ameliacha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu Tukufu iwalipe fidia wananchi hawa ili ardhi ile iwe huru, pia wananchi waweze sasa kuendeleza maisha yao vizuri na wawekezaji waweze kuwekeza viwanda. Muda si rafiki, miaka imepita mingi na wananchi wa Tanzania wanakiu ya maendeleo wamechoka na umaskini, sasa tufanye kazi tu kama ambavyo Mheshimiwa Rais anasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya EPZ Bagamoyo ilihusisha maeneo ya makazi ya watu wengi, naiomba Serikali kwamba iondoshe maeneo ya makazi ya watu wengi katika mpango wa EPZ, wananchi hawalikubali hili, hawana mahali pengine pa kwenda. Tuache katika hiyo awamu ya kwanza ya hekta 5,742 iwe sehemu ya EPZ kwa ajili ya Bagamoyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa hatua ya kijasiri ya ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge, hili ni jambo kubwa sana. Reli ni kichocheo cha maendeleo ya viwanda na kichocheo cha maendeleo ya uchumi katika nchi yetu. Ila reli hii ya kisasa yenye uwezo mkubwa italipwa na sehena za mizigo kutoka nchi yetu na nchi jirani ambazo zinatuzunguka kama Rwanda, Burundi, DRC-Mashariki, Zambia na Malawi, ni shehena hizi za mizigo ambazo zitalipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma ya abiria ni nyongeza tu na ni faida ambayo itawezesha watani wangu Tabora na Mwanza kuweza kusafiri lakini siyo nauli za abiria hazitoweza kulipa. Kwa maana kwamba bila shenena ya mizigo itakuwa vigumu sana reli hii kubwa kuleta manufaa katika nchi yetu, haitoweza kujilipa. Sasa mwenzie reli yenye uwezo kama huu ni nini? Mwenzie ni bandari, bandari kubwa, yenye uwezo mkubwa wa kuweza kuleta shenena ya mzigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2008 Mamlaka ya Bandari iliweza kufanya study na ika-establish kwamba itahitaji kujenga bandari Bagamoyo, bandari kubwa ya kisasa, miundombinu mipya ambayo inaendana na Tanzania ya kesho. Sasa Mheshimiwa Waziri ili reli hii iwe na tija maana yake ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo ni bora uanze mapema na uanze kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina wasiwasi na mkakati wa ujenzi wa Bandari Bagamoyo, kwa sababu Rais wa China na Rais Mstaafu Jakaya Kikwete tarehe 24 Machi, 2013 walishuhudia utiaji saini wa implementation agreement kuhusu ujenzi wa Bandari Bagamoyo, leo ni miaka mitano baadaye bado tunazungumza. Katika kipindi hiki cha miaka mitano wabia wetu wa China Merchant wamekamilisha mazungumzo na wamejenga bandari katika maeneo yafuatayo; Djibouti, Abuja, Ivory Coast, Colombo-Sirlanka, wamejenga pia Tin-Can City Nigeria na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hawa wenzetu hawa wanawezaje kukamilisha maongezi na kuanza kujenga ndani ya miaka mitano hii wakati sisi tunaongea. Wao wana nini na sisi tuna nini? Tuna watalaam wa kutosha wa kuweza kukamilisha maongezi na kuweza kuhakikisha kwamba ujenzi unaanza mapema iwezekanavyo. Wananchi wa Tanzania wana kiu ya maendeleo na ni muhimu tuhakikishie kwamba
tunaondoa umaskini wa wananchi hawa mapema iwezekanavyo. Hatuwezi kuendelea kusubiri kila siku wakati, wakati tuna watu ambao wanaweza kufanya kazi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapohitimisha atuambie ni lini tunaanza ujenzi wa Bandari Bagamoyo ili bandari hii iweze sasa kuungana na reli mpya ya SGR na barabara zetu kuu za usafirishaji ili kuweza kuchochea maendeleo ya uchumi katika nchi yetu, tunahitaji tuondokane na umaskini. Mwaka 2025 Tanzania kuwa na uchumi wa kati ni miaka sita tu usoni yaani muda hatuna. Muda umekwisha ama sivyo tutafika mwaka 2025 tunajitathmini ni kwamba hakuna ambacho tumeweza kukifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali kubwa kabisa namba moja kwa maendeleo ya nchi yetu ni watu wetu, wakiwemo vijana wetu wa kike na vijana wa kiume. Kuna mahitaji makubwa sana ya mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana wetu wanaomaliza darasa la saba na kidato cha nne ambao wanakosa nafasi ya kuendelea katika elimu ijayo. Jambo ambalo linanisikitisha ni kwamba, Serikali imekuwa na mtindo wa kutokupeleka VETA fedha za SDL na hili ni jambo la kisheria. Kwa taarifa nilizonazo takribani shilingi bilioni 65 hadi mwezi Aprili mwaka huu zilikuwa hazijapelekwa katika Wizara ya Elimu kama fedha za SDL kwa ajili ya VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni fedha za malimbikizo karibu miaka mitatu, sasa VETA wanahitaji hizi hela za SDL ili waweze kupanua nafasi za mafunzo kwa ajili ya vijana wetu. Kupanua nafasi za mafunzo kwa kutujengea VETA katika Wilaya zetu, kununua vifaa vya mafunzo na kununua vifaa vingine ambavyo vinawezesha mafunzo mazuri kwa ajili ya watoto wa kitanzania yaweze kutekelezwa. Vijana hawa wawe na skills mikono mwao, waweze kuingia katika soko la ajira wakiwa na skills katika mikono yao, wawe watu ambao wataisaidia nchi hii kufika katika uchumi wa kati mwaka 2025. Naiomba Wizara ya Fedha wahakikishe kwamba hizi pesa zinapelekwa….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.