Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. GEOGRE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nikushukuru kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri wa Wizara hii ya Mipango na Fedha kwa kazi nzuri wanayofanya na sisi tunasema kama Wabunge wa chama kilichopewa dhamana na Watanzania kuongoza nchi hii, tuko nyuma yao na wasiwe na hofu yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yamezungumzwa mengi juu ya uchumi wa nchi yetu. Leo nianze kwa kumuunga mkono nakubaliana sana mawazo ya mchangiaji aliyepita rafiki yangu Bashe kwa maeneo aliyogusa amefanya kazi nzuri ya kibunge na ni mfano mzuri wa Wabunge wengi ambao tunachangia michango yetu hapa inayokwenda sawasawa kabisa na tunachotakiwa kuwafanyia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labla pengine nilikuwa nikisikiliza wenzangu wanavyochangia wakihoji uwezo wa kuweka mipango ya nchi yetu na kuendesha uchumi wa nchi na wengine wakijaribu kubeza yanayofanyika. Nataka niwahakikishie na hasa Wabunge wenzangu wa CCM. Tusivunjike moyo watanzania wanatuelewa wanaona barabara zinajengwa, wanaona zahanati zinajengwa, wanaona vituo vya afya vinajengwa wanaona watoto wao wanasoma bure, wako pamoja na sisi na wanatuelewa sana tuendelee. Usitegemee adui yako akakusifia na ukiona anakusifia basi jambo hilo uliache, ukiona anakupinga jambo hilo lifanye sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nitumie Bunge lako kukumbusha misingi ya uchumi wa nchi yetu unapangwaje. Maana hapa zimekuwa zikielezwa theories mbalimbali za uchumi na wengine hata siyo Wachumi na hata mimi na-declare kwamba siyo Mchumi, lakini nataka nijadili uchumi kwa legal perspective, kwa sababu mipango na uendeshaji wa uchumi haji nao tu Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa sababu ni Waziri, ipo kwenye sheria na katiba hakurupuki tu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango akaja tu na mambo hapa akasema imekuwa hivi imekuwa hivi, hapana.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka nisome katiba na naomba niisome kwa ukamilifu maeneo yanayo-guide mipango na uendeshaji wa uchumi wa nchi yetu; ili tukiwa tunazungumza tuwe tunaelewana, maana wako wengine wana nadharia za kibepari, wako wengine wana nadharia za kijamaa hatuwezi kuelewana sisi wana TANU na ASP tunajua tulikotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba ninukuu Ibara ya tisa (9) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inasema hivi:

“Lengo la katiba hii ni kuwezesha ujenzi wa Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar au wa chochote kati ya vyombo vyake na udugu na amani kutokana na kufuata siasa ya ujamaa na kujitegemea, ambayo inasisitiza utekelezaji wa misingi ya kijamaa kwa kuzingatia mazingira yaliyomo katika Jamhuri ya Muungano.

Mheshimiwa Spika, naendelea anasema katika Ibara hii ya 9: ...Hivyo Mamlaka ya Nchi na vyombo vyake vyote inawajibika kuelekeza sera na shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha...

Mheshimiwa Spika, naruka (a), naruka (b) kwa sababu ya muda naenda (c):

(c) kwamba shughuli za Serikali zinatekelezwa kwa njia ambazo zitahakikisha kwamba utajiri wa Taifa unaendelezwa, unahifadhiwa na unatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote kwa ujumla na pia kuzuia mtu kumnyonya mtu mwingine; (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niruke zote niende (i) inasema:

(i) kwamba matumizi ya utajiri wa Taifa yanatilia mkazo maendeleo ya wananchi na hasa zaidi yanaelekezwa kwenye jitihada za kuondosha umaskini, ujinga na maradhi;

(j) kwamba shughuli za uchumi haziendeshwi kwa njia zinazoweza kusababisha ulimbikizaji wa mali au njia kuu za uchumi katika mamlaka ya watu wachache binafsi.”

T A A R I F A . . .

MHE. GEOGRE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Spika, nia yake ilikuwa ni kuona kwenye TV umeonekana. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nimenukuu eneo hili theories tunazozitoa nyingi hapa kila mtu anatoa theory yake na anachukua mfano best practice ya nchi anayoiona yeye. Wakati asili ya uchumi wa Taifa lolote, asili ya mipango ya uchumi wa Taifa, mipango ya maendeleo ya Taifa lolote inatokana na historia yake. Sisi Watanzania kwa asili ni wajamaa na fikra zetu sisi ni za kiumoja umoja na ujamaa jamaa, huwezi kuwabadilisha Watanzania hapo.

Mheshimiwa Spika, leo hii mtu akija na mawazo ya purely ubepari, basi hatokani na misingi ya Kitanzania, ingawa katika Ibara hii ya tisa (9) inasema tutafuata siasa ya ujamaa na kujitegemea kwa kuzingatia mazingira na mabadiliko ya wakati. Ndiyo maana katika sheria zetu tumetambua baadhi ya misingi ya kibepari, tukatunga sheria ya PPP kwamba wakati mwingine Serikali itapaswa kufanya biashara na sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, tukapima tukaweka sheria ya ubinafsishaji kwamba tukaribishe sekta binafsi iingie kufanya kazi na Serikali. Ndiyo maana tuna viwanda na ndiyo maana shughuli mbalimbali zinazofanywa na sekta binafsi, lakini katika katiba hii inatukataza kupeleka njia kuu za uchumi mikononi mwa watu wachache maana huo ni unyonyaji. Ndiyo maana tunapokuwa tunazungumza mambo haya ni lazima twende kwa kiasi maana nchi yetu kwa asili na hata fikra za watu, utamaduni wa watu wanafikiria… (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. GEOGRE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Spika, nikubaliane kwamba wakati mwingine mtu unapochangia ukakatizwa katizwa inaondoa ladha nzima, lakini nime-cite hapa Katiba yetu na naomba nirudie maana sasa sina namna na kwa hiyo hata hotuba yangu haitakwisha.

Mheshimiwa Spika, eneo la katiba hili linazingatia kwamba ambavyo inasisitiza utekelezaji wa misingi ya kijamaa, kwa kuzingatia mazingira yalimo katika Jamhuri ya Muungano. Mazingira yatakavyojitokeza tutabadilika kulingana na ndiyo maana sisi hatuwezi kusema ni wajamaa per se au mabebari per se. Ukitaka kutengeneza misingi ya uchumi wa Tanzania haiwezekani ikafafana na nchi nyingine that’s what I want to say! Ni lazima itokane na asili ya watu wale ndiyo maana kwenye miaka ya 90 mpaka 2000 tulipoingia kwenye sera ya ubinafsishaji, tulipobinafsisisha wengine walipotaka kutuondoa madarakani wakasema hawa wameuza viwanda, wakati wao wenyewe wanasema tukumbatie sekta binafsi, wakasema tumeuza viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tulikuwa tuna Shirika la Ndege ambalo tumejaribu kucheza na sekta binafsi tukaingiza South Africa wakachukua baadhi ya hisa na nini likashindwa kwenda. Tumeamua Serikali ya Awamu ya Tano kununua ndege zetu imekuwa nongwa. Leo hii tunayo reli ambayo tumeamua kuijenga sisi wenyewe kama nchi na kwa kuanza na fedha zetu wanasema kwa nini tusiwape sekta binafsi waweze kufanya mambo yenye gharama kubwa. Huku wakiona kabisa kwamba yako baadhi ya mabehewa ya watu binafsi yanayotembea kwenye reli…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia ni lazima Watanzania tuunge mkono tijihada hizi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano maana mengi haya yanayofanywa leo yalikwishashindikana kwa formula hizo wanazozisema. Ndiyo maana tunasema tuungane mkono kwa sababu hakuna kanuni moja ya uendeshaji wa uchumi na uchumi unatokana na historia ya watu wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja.