Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa fursa hii ili nitoe mchango wangu kidogo kwa bajeti Kuu ya Serikali. La kwanza nizungumzie mambo ya jumla, kwenye jimbo letu kuna mambo hayajanyooka. Kumekuwa na shida, uchaguzi kila siku napiga kelele uchaguzi wa kata zetu tatu haukufanyika na mpaka sasa Serikali haijatoa maelezo yoyote kwamba nini kitafanyika, lakini watu hawa wamemchagua Rais, wamemchagua Mbunge, lakini kama tuliwapa uraia hawa kwa masharti ni vizuri tukaondoa masharti. Nchi yetu kama ilitoa uraia kwa nia njema, lakini tunaanza kuwabagua na jambo hili sio zuri sana kwa mustakabali wa maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niseme Waheshimiwa Mawaziri waache kubagua, watembelee na majimbo mengine hata kama, niishie tu kusema hata kama. Mawaziri kuna maeneo wanapishana Mawaziri wanne wanakwenda sehemu moja, tunashuhudia lakini kuna maeneo kama Uliyankulu hawataki kabisa kuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, toka afike Waziri Mkuu na Waziri Mkuu alikuja kutusalimia kwa sababu alikuwa DC wetu, lakini wengine kila siku hapa tunapigizana kelele, lakini mtu akiuliza hapa, hii nazungumzia mimi Waziri atakwambia tu niko tayari kuambatana na wewe, lakini muda ukifika ziara inapeperuka. Wananchi wetu wanakata tamaa kwamba hili eneo lilitengwa toka miaka yote toka enzi za Mzee Maswanywa, Mzee Sitta, Mzee Kapuya watu hawaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Uliyankulu linataka dhamira ya dhati, kama hawatupendi sisi tutajua namna ya kupendwa. Nawasihi sana waje bwana, basi waje waangalie tu hata kaburi la Mirambo, hawataki na yenyewe, nadhani wamenisikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kumaliza habari ya wakimbizi na kambi za wakimbizi ni jambo muhimu likaisha kama kuna sheria tunaziona ngumu, kama tunaona uamuzi wetu wa kuwapa uraia ulikuwa na shida tutamke, watu hawa sasa hawawezi kujenga kwa sababu kambi haijafungwa lakini ndani ya kambi kuna watu hawataki uraia wa Tanzania na hawataki kurudi Burundi, tunafanya nini? Najua mdogo wangu Mheshimiwa Mwigulu ananisikia vizuri na anajua vizuri. Kama Serikali walimalize hili kwa hiyo, watu wamekaa pale stranded hawajui kama watahamishwa au kama wataendelea kukaa hapo, matokeo yake wanatufikiria tofauti hasa wakati wa uchaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema wakati mwingine wanasema nasema sana, nimechaguliwa asilimia 70 ya raia wake wamenichagua, sasa piga hesabu wakigeuka? Ndio hofu lazima tuambizane, wakigeuka ni matatizo. Haya mara waseme hifadhi, kwa hiyo sisi watu wa Ulyankulu tupo tu kwa sababu watapita watatoka Tabora, wataenda Kaliua, Urambo, wataenda Kigoma lakini Ulyankulu lazima aje Ulyankulu awe na dhamira kweli leo nakwenda kwa Mheshimiwa Kadutu, hivi hivi hatuwezi kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuliwahi kusema hapa suala la kugawa maeneo, lakini sasa hivi Serikali inasema wanabana matumizi hawataki kugawa maeneo. Jamani Tabora ilivyo, hiyo sehemu ya Sumbawanga ilikuwa Tabora, Katavi yote ni Tabora, mkoa bado ni mkubwa kuliko kawaida, wataugawa lini, mpaka watakapotaka kuwagawia wengine ndio na sisi watupitishie humo, hiyo sio haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua ipo siku hapa tutasimangana hapa, kuna eneo watatoa eneo jipya la utawala ndio watakumbuka sasa na Ulyankulu. Tunataka sisi Ulyankulu iwe Wilaya, iwe halmashauri na uwezo huo tunao own source ya Wilaya ya Kaliua ndio inayoongoza kwa Mkoa wa Tabora kuliko hao wengine, sisi tunaweza kuleta hapa own source Bahi, nani wote hawa tukawasaidia, lakini hawataki kutupa eneo, sijui mpaka lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema ahadi za Rais zitatekelezwa, sasa hii ni ahadi ya Rais wakati wa uchaguzi. Wakati wa uchaguzi kulikuwa na mambo mawili, kuna ahadi za Rais, lakini kuna Ilani ya Uchaguzi. Sasa hizi ni ahadi za Rais alituambia siku tatu akiingia ofisini tunapata Wilaya na tunapata halmashauri, lakini mpaka leo! Sasa wameleta habari kwamba gharama kubwa na nini, lakini yako maeneo madogo wamewapa mkoa, wengine wilaya, watukumbuke basi na sisi Mkoa wa Tabora. Upo mkoa tulishapendekeza Mkoa wa Nzega na Mkoa wa Urambo ambao JK aliacha amependekeza. Sasa yale yaliyotendwa na wazee wetu walioondoka tuyatekeleze basi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi zile zilizomo ndani ya ilani lazima tujipime, sasa tumebakiza labda mwaka mmoja tu na nusu, je, tumetekeleza kwa kiwango gani? Yako mambo mengi hivi hakuna hata uratibu wa kuyaondoa moja baada ya lingine, wametuahidi lami, wametuahidi hiki tena ndogo ndogo tu kilomita tatu, kilomita ngapi, hakuna hata dalili. Hata hivyo, tunakuwa tunaona yapo mambo ambayo hayamo kwenye ahadi, hayapo kwenye ilani yanatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatupendi kwa kweli kuyasema lakini wakati mwingine hivi watu wa Ulyankulu huko wamenituma, halafu nakaa napiga makofi tu hapa mimi siwezi bwana. Tusaidieni ili hata uchaguzi wa 2020 watu mpete, hata tukisimama pale tunapiga kampeni wakati huo mimi mstaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze sasa juu ya fedha za maendeleo, hapa juzi wenzangu wamezungumza wengi tu hapa juzi wakaitwa Wenyeviti na Wakurugenzi hapa, tumewaita wapangue mpango huu, tunataka miradi ya mkakati tutatoa huko miradi midogo midogo achaneni nayo, wakaja hapa wakamaliza wakarudi kwenye halmashauri wakaitisha Finance pamoja na Baraza, watu wakalamba posho. Leo hii ni tarehe 20 maana yake zimebaki siku 10 tu, watuambie Serikali wanao uwezo kweli wa kuleta pesa kule? Kwa maana hiyo, Mheshimiwa Waziri ni kwamba halmashauri zile ambazo hazina own source zitakufa kifo cha kimya kimya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri nimetoka huko kwenye halmashauri, nazijua vizuri kweli, lakini wakati mwingine tarehe 28 wataingiza pesa ambayo haitatumika mwisho wa mwaka na CAG atahoji kwamba hizi pesa vipi mbona hawakuzitumia tutaleta maswali mengine. Mheshimiwa Dkt. Mpango ajaribu katika hali ya kibinadamu sasa juu ya madeni ya mawakala wa pembejeo na wazabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi uhakiki wa mawakala ambao hawafiki 1,000 unaweza kufanana na wafanyakazi zaidi ya 800,000. Wafanyakazi mnahakiki na imejulikana huyu tupa kule huyu huku, tupa huku, kazi imekwisha. Hivi uhakiki wa madeni ya wazabuni pamoja na mawakala wa pembejeo hivi kweli hawaoni ni tatizo. Mawakala sasa hao kila Bunge wapo hapa na wakati mwingine wanaishiwa hata pesa ya kula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge tunahangaika kuwalisha, siku moja Mheshimiwa Jacqueline hapa mpaka analia, hivi kweli wanataka watu tuanze kulia wote huko haifai. Kazi leo Mheshimiwa Waziri waifanye tu kwa nia ya kibinadamu kwamba watu wamekopa maeneo, sasa hata mali zao watafilisiwa. Kama mtu alidanganya watoe basi orodha, hawa wafuatao ndio wako halali, hawa wengine utapeli jazz band. Watu watajua ili jambo hili lifike mwisho kwa sababu sasa kwa mfano sisi wengine vijijini huko na kilimo kwa mfano cha tumbaku, yaani bila mbolea huwezi kufanikiwa, bila mtu kukusaidia wakulima wetu wamezoea hiyo, hawana nguvu za kununua pembejeo wenyewe, tusaidieni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuje suala la kilimo; kwenye vitabu vya Mheshimiwa Waziri amesema kweli kwamba pato la Serikali asilimia 30 linatokana na kilimo, lakini hebu atafakari mwenyewe, kilimo wameipa asilimia ngapi basi ya pesa hizi?

Maana kilimo hatukizingatii. Mwaka jana hapa zao letu la tumbaku maana yake sisi ukizungumza siasa lazima uzungumzie tumbaku hata kama huipendi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Serikali ika-delay kutoa uamuzi, niseme tu natoka kwenye eneo linalolimwa tumbaku nyingi Tanzania, kwa hiyo, najua vizuri. Matokeo yake hapa tukajichanganya Serikali imechelewa kutoa maamuzi wakulima wetu wamekwenda kuuza tumbaku kwa bei ya chini zero point. Wamepata hasara, mtu alikuwa ame-plan kupata milioni ishirini, anaishia milioni mbili laki tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali lazima iangalie, hili zao tunasema asilimia thelathini ya pesa inakwenda Serikalini inazalisha mazao ya kilimo, lakini sisi hatutaki kuhudumia kilimo. Unasikia korosho wanalalamika, kahawa wanalalamika, ndugu zangu kule Kanda ya Ziwa pamba wanalalamika, kilimo kipi sasa ambacho tumefanikiwa matikiti? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda matikiti yamekuwa mengi, mtu anaweza akasimama hapa akasema tumefanikiwa, lakini kila eneo la kilimo, kelele hata kwa ndugu zangu kule Wanging’ombe maua sijui nini, wote kule ni malalamiko. Hakuna yaani sijui lumbesa sasa haitajwi yaani shida tupu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri, wajaribu kukaa, kweli wote humu hatuwezi kuwa wachumi, lakini tuna macho na akili. Tunaona, mambo haya wayarekebishe twende mbele, tumebakiza mwaka mmoja tu, yaani bajeti yenye kuweza kujadili kwa utulivu imebaki moja, ile nyingine watu wote humu watakuwa akili kwenye uchaguzi. Hakuna tena majimboni, watu wanatafakari nani ananifuatafuata huku, hakutakuwa na mjadala mzuri, umebaki mmoja, hebu wajaribu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa lingine tumeshafanya Serikali imefanya mambo hayo makubwa ya ununuzi wa ndege, sijui ujenzi wa reli, hebu sasa twende kwa wananchi wa kawaida, yale mapato ya pesa, watu wapate wananchi wa kawaida wazione. Unajua ukimweleza mwingine, kwa mfano, kule Ulyankulu ukimweleza habari ya bombadier mimi nasema ukweli tu, wakinichukia na wanichukie, bombadier mfano Ulyankulu wao wanaamini hizi hela za Serikali zinatokana na tumbaku. Sasa ukiwaeleza habari za bombardier, barabara mbovu, hospitali mbovu hawaelewi wapeleke sasa huduma hizi ziende kwa wananchi, barabara kule vijijini ziboreshwe, hao TARURA wapewe pesa, tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishie hapa..
Ahsante sana.