Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kutoa maoni yangu katika mpango wa bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kuipongeza Wizara ya Fedha kwa namna ilivyotuletea mpango na kwa jinsi ilivyojikita zaidi kufuta tozo au kodi zilizokuwa kero kwa wananchi, naipongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kuanza mchango wangu, naipongeza Serikali kwa namna ilivyoanza kulifufua zao la pamba kiasi kwamba sasa kumeanza kuwepo matumaini kwa wakulima wa pamba katika Mkoa wa Simiyu na Kanda ya Ziwa kwa ujumla. Naipongeza Serikali kwa kufuta mchango uliokuwa ukitozwa, Sh.30 kwa kila kilo kwa ajili ya kuendeleza zao la pamba. Mchango huu haukuwa na tija kwa sababu Mfuko huu ambao unajulikana kama CDTF haukuwa na tija yoyote, haukuweza kumsaidia mkulima na badala yake uliendelea kuleta pembejeo hafifu na uzalishaji uliendelea kupungua. Kwa mfano, takwimu za msimu 2015/2016, zilikuwa tani 149,000 na kupungua zaidi katika msimu wa 2016/2017 ambapo zilivunwa tani 121,000. Kwa hiyo, hakukua na tija yoyote kuwepo kwa mfuko huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kazi zilizokuwa zinafanywa na Mfuko huu zitafanywa na Bodi ya Pamba kwa kushirikiana na Maafisa Kilimo walioko katika halmashauri zetu. Kwa sababu muda wote ule kulikuwa na mgongano wa maslahi, mkulima alikuwa anamfahamu tu Bodi ya Pamba pamoja na Mfuko ule kwa sababu ndo uliokuwa unapelekea pembejeo ya mbegu na dawa kiasi kwamba Afisa Kilimo hakupewa nguvu yoyote au hakuthaminika kwa mkulima kuweza kulisimamia zao hilo kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina shauri sasa Serikali kupitia halmashauri iwawezeshe Maafisa Kilimo kikamilifu kwa sababu kila Kata kuna Afisa Kilimo. Iwawezeshe usafiri na iwawezeshe kwa namna yoyote ili waweze kulisimamia lile zao badala ya Bodi ya Pamba ambayo ina mtu mmoja tu katika Wilaya ndiyo aliyekuwa anasimamia zao hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza Serikali kwa kufufua ushirika na kwa msimu huu imeanza kununua pamba kupitia vyama vya ushirika. Nafahamu mwanzo ni mgumu, sisi Wabunge tuko nyuma yenu, tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jitihada zote anazozifanya kulisimamia hili zao. Mheshimiwa Waziri Mkuu mimi niko nyuma yako nitaendelea kukupa ushirikiano ambao ninaweza kukupa ili kuweza kufikia malengo ambayo Serikali inatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini sasa zao hili linaenda kuwa mikononi mwa Serikali, Serikali itakuwa na uwezo wa kuweza kulitolea maamuzi yoyote tofauti na ilivyokuwa mwanzo. Naamini sasa vile vyama vinaibuka na kutoza hela kwenye ushuru huo sasa vinaenda kujifuta vyenyewe kupitia ushirika. Halmashauri za Wilaya zinaenda kupata takwimu sahihi kwa ajili ya kutoza ushuru wa pamba. Nachoshauri vile vitabu vinavyotumika Wakurugenzi waone kwamba ni nyaraka muhimu kwa sababu zinaenda kutumika kukokotoa kupata takwimu sahihi badala ya ule mgongano uliokuwepo baina ya Halmashauri na Bodi ya Pamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tatizo lililopo hatuna Maafisa Ushirika wa kutosha. Halmashauri zetu zina Afisa Ushirika mmoja mmoja wengine wanaenda kustaafu mwezi wa sita. Kwa kipindi hiki cha mpito Maafisa Ushirika ni wa umuhimu kwa ajili ya kufufua ushirika, kwa sababu mara tu baada ya msimu ukaguzi unatakiwa ufanyike mara moja ili vyama vya ushirika vijiendeshe kwa faida. Bila Maafisa Ushika tunaenda kurudi nyuma, mapato yanayotokana na ushirika kwa vyama vya ushirika hayatajulikana badala yake tutaendelea kutengeneza hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi hiki ni muhimu sasa kuwezesha kuwepo kwa COASCO kwa ajili ya ukaguzi ili baadaye tusirudi kule tulikotoka. Kwa mfano, Wilaya ya Meatu ina AMCOS 80, ina vituo vya kununulia pamba 200, lakini Afisa Ushirika aliyepo ni mmoja. Je, ni nani anaenda kukagua mapato na matumizi ya vyama vya ushirika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza Serikali kwa kufuta Kodi ya Ongezeko la Thamani katika taulo zinazotumiwa na akina mama na wasichana wakati wa hedhi,. Kufuta tozo hiyo inaenda kumpunguzia mwanamke mzigo kwa kiasi fulani. Naishauri Serikali bado ina nafasi kubwa ya kumsaidia mwanamke kupunguziwa bei ya taulo hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nikiangalia pedi nyingi zinatoka nje, sisi Tanzania tunatumika kama wasambazaji, pamba inayozalishwa asilimia 30 tu ndio inayotumika nchini asilimia 70 inaenda nje. Hii inamaanisha kwamba hatuna viwanda vya kutosha vinavyoweza pia kutengeneza pedi. Hata pedi tunazotengeneza nchini pamba inayotumika inaenda nje kwanza ndipo inarudi Tanzania kwa ajili ya kutengeneza. Kwa hiyo, Serikali inalo jukumu kubwa la kuhakikisha sasa tunakuwa na viwanda vya kutosha ili sasa asilimia kubwa ya pamba iweze kutumika nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali katika ukurasa wa 85 umesema kwamba unaongeza uzalishaji wa mbegu bora za pamba aina ya UKM09 tani 40,000. Pia, inaenda kutenga maeneo kwa ajili ya uzalishaji wa mbegu hiyo; kutoa elimu kwa ajili ya wakulima; na kutoa vitendea kazi na kuhamasisha wakulima. Ukiangalia mikoa iliyotajwa Simiyu haijatajwa kama inaenda kuwezeshwa na hapo hapo Serikali imepanga shilingi bilioni 6.1 kwa ajili ya kutekeleza zoezi hilo. Ukiangalia Mkoa wa Simiyu pia asilimia 60 ya pamba inayozalishwa nchini inatoka Mkoa wa Simiyu. Kwa hiyo, naiomba Serikali Mkoa wa Simiyu na wenyewe uwemo katika kuwezeshwa kwa namna Serikali ilivyojipanga kuwezesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Simiyu unacho kituo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.