Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Nianze tu na alipoishia Profesa, ndugu yangu kwamba mimi nashangaa na sielewi kama Taifa tunataka nini? Tunataka ujamaa au ubebepari? Tunataka umeme wa maji au wa makaa ya mawe? Yaani nashangaa!

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina taarifa hapa ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa ya tarehe 3 Juni, 2016 anasema kwamba Serikali inawekeza katika Mradi wa Mchuchuma na Liganga ambao utazalisha megawatt za umeme na kuingizwa kwenye Gridi ya Taifa. Mradi huu navyofahamu ulikuwepo miaka mingi sana lakini haujatekelezwa na ulikuwa ndiyo ukombozi wa nchi hii katika umeme na ndiyo tulivyokuwa tunaambiwa hapa. Sasa tunakwenda katika umeme wa maji ambao tuna Mabwawa ya Nyumba ya Mungu, Kihansi, Mtera, Hale na Pangani na yote haya yanazalisha chini ya kiwango chake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka nchi hii inapatwa na ukame, hatuna uhakika huo umeme wa maji tunaoenda kuzalisha kama utaweza kumudu tabianchi. Umeme wa makaa ya mawe na chuma cha Liganga una uhakikika kwamba hauwezi kuadhiriwa na tabianchi. Kuna umeme wa upepo wa Singida tumeshindwa kuuendeleza. Mradi wa Umeme wa Singida Benki ya EXIM ya China, Mheshimiwa Waziri anajua, ilishakubali kutoa mkopo kupitia NDC ili umeme ule uweze kuendelezwa, umeshindwa kuendelezwa. Sasa unashangaa kwa nini tunachukua vitu nusu nusu? Leo tunaanzisha hiki, hatufikishi mbali tunakiua; kesho tunaibuka na kitu kingine. Fedha za Watanzania zinazama kwenye miradi ambayo siyo endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi watu wamezungumza hapa juu ya Kiwanda cha Urafiki ambacho kilikuwa ni mali ya Watanzania kwa asilimia 100. Wamekichukua kiwanda, wakakiuza kwa mwekezaji, mwekezaji akawa hana mtaji, wakamkopesha fedha za Serikali, Serikali ya Tanzania ikamdhamini kwenye benki za nje, akaenda kukopa na fedha hakurudisha na hisa anazo yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati fulani aliyekuwa Rais wa Awamu ya Pili, Mzee Alhaj Ally Hassan Mwinyi aliwahi kuita timu yetu ya Taifa Kichwa cha Mwendawazimu kwamba kila mtu anajifundisha kunyoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli unashangaa kwamba jambo tunalianzisha, tumeanzisha umeme wa gesi, wamekuja hapa Maprofesa, Profesa Muhongo alitembea na agenda ya umeme wa gesi nchi nzima, ndiyo ilikuwa agenda. Leo tumeacha gesi, tunazungumza umeme wa maji. Umeme wa maji ulikuwepo wakati wa Mwalimu Nyerere yakajengwa hayo mabwawa makubwa, tukahama tukaenda kuanzisha umeme wa mashine za kukodi; Songas, APTL, Richmond, DOWANS, tumeona huko nako; yaani sijui tunaelekea wapi? Sijui Taifa hili wataalam wetu wanafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Mheshimiwa Dkt. Mpango, Waziri wa Fedha, kaka yangu namheshimu sana, nimemsoma akiwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, amefanya kazi nzuri, naomba asimame kama Waziri wa Fedha, amshauri Mheshimiwa Rais vizuri. Rais wetu siyo mchumi na hakuna binadamu yeyote aliyekamilika mahali popote pale. Waziri amshauri Rais, awe kama Mawaziri wa Fedha waliopita. Alikuwepo Mheshimiwa Mgimwa, alikuwa Waziri wa Fedha anayejiamini alikataa mpaka kulipa hela za Escrow, record zipo. Mheshimiwa Waziri Mpango amshauri Rais, hivi kweli mnachukua fedha shilingi bilioni 211 za korosho za wananchi wa Mtwara hamzirudishi, mnarudisha shilingi
bilioni 10, mnakuja na Muswada leo wa kuzuia hizo fedha zisirudi tena Mtwara. Jamani, huu ni wizi wa fedha za wananchi. Hii ni dhuluma! Hawa ni wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mama yangu Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti nilikuwa India wakati naumwa ni miongoni mwa watu wa kwanza waliokuja kuniangalia. Mama simamia hii kitu, itakuondoa Bungeni. Wananchi wa Mtwara hawatakuelewa. Hawakukuelewa kwenye gesi, hii ndiyo hawatakuelewa kabisa. Simama mama, fedha za wananchi hizi zinataka kuondoka, simama zitetee ili wananchi wa Mtwara, Kusini, Mafia na maeneo mengine wanaolima korosho wapate matunda ya zao lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri, unakuta kodi kwenye ndizi zinazotengenezea pombe, matunda, mimi nilitegemea tuletewe fedha za makinikia zile shilingi trilioni 409, tuzione humu ili wananchi wetu waachane na hizi kodi na TRA iache kukimbizana na Wamachinga Kariakoo. Shilingi trilioni 409 ni fedha nyingi kweli ambazo zinatosha kuendesha nchi hii kwa zaidi ya miaka 10. Sasa badala yake hizo fedha hazipo, wimbo wa makinikia hatuusikii tena, tuachane na hivi vitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu Nyerere aliwahi kusema hivi, ukikuta Serikali inakimbizana na Wamachinga mtaani, haikusanyi kodi kwa wafanyabiashara wakubwa, ujue kuna tatizo. Sisi kodi zetu zote ni kwa wafanyabiashara ndogo ndogo; wauza vitumbua, bodaboda, Machinga, tuachane na vitu hivi, tuleteeni kodi za migodi, ondoeni misamaha ya mafuta kwenye migodi, tuleteeni vitu vikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti nzima hii wanasema haitekelezeki, mimi sijui kama haitekelezeki, lakini Mheshimiwa Waziri anajua kwamba mapato yetu yanashuka mwezi hadi mwezi na kwenye mwezi Mei na Aprili mwaka huu, mapato yetu yalipungua na yalikuwepo mapendekezo ya kupunguza fedha za maendeleo katika baadhi ya maeneo. Ni lazima Serikali itafute mpango madhubuti wa kuendesha uchumi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkiwa mnakwenda kulia, mnajiita wajamaa wakati Serikali haimiliki hata benki moja kwa asilimia 100, inamiliki asilimia 30 au asilimia 31 kwenye NMB na NBC, halafu Serikali inajiita ya ujamaa. Mtu mmoja anasimama anajiita mjamaa lakini ukimwangalia kwa nyuma ana shamba heka 150 halafu anasema ni mjamaa. Sasa sijui ni mjamaa au Kijiji cha Ujamaa, mimi sielewi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili Taifa ni letu wote na likididimia, tunadidimia sote, hakuna atakayekuwa salama. Mheshimiwa Waziri analeta mapendekezo na amesema kwenye Muswada na analeta humu kwamba kutakuwa na akaunti moja ya kuhifadhi fedha. Mkipata Rais anayefanana na Sani Abacha tutakuja kulia huku. Ni lazima tuweke mipaka ya madaraka. Ninyi mlikuja na mapendekezo ya kupunguza madaraka ya Rais katika Katiba Mpya. Mapendekezo ya Katiba Pendekezwa ni kupunguza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kusema Mheshimiwa Waziri wa Fedha amshauri Rais vizuri.