Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye hotuba ya bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Mpango na Mheshimiwa Dkt. Kijaji kwa kazi nzuri wanayoifanya. Kwa hakika kwa Wizara hii kutupiwa lawama ni jambo la kawaida kwa sababu ni Wizara ngumu na hasa ukizingatia kwamba fedha tunazozipata hazitoshelezi kufanya kila jambo kwa wakati tunaohitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwenye suala la mapato. Naona bado kabisa tuna mianya ya ukusanyaji wa mapato. Nikianza na mfano mdogo tu, bahati nzuri niliwahi kuwa Dar es Salaam pale, suala la Property Tax, kiwango tunachokusanya hakifanani na hali halisi ambayo tungeweza kupata. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, akae vizuri na watu wa TRA ukusanyaji wa fedha hizi ni mdogo sana. Pia hata suala zima la kukadiria, suala la malipo ya hizi fedha za Property Tax haziko katika kiwango kinachostahili. Kwa hiyo, naomba sana kwamba suala la ukusanyaji mapato katika kila eneo ambalo linatakiwa zikusanye lifanywe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, sasa hivi ukienda katika petrol stations zetu nyingi, kila petrol station karibu wiki nzima hii nikipita wanasema zile mashine zimeharibika. Kwa hiyo, kuna kila dalili kwamba katika miezi hii tutakosa mapato mengi. Naomba tu nimshauri Mheshimiwa Waziri, hivi haiwezekani badala ya kufunga zile mashine wale wafanyabishara wakubwa wa mafuta wanaomiliki vile vituo wakatozwa kodi moja kwa moja kule wanakonunulia mafuta ya jumla badala ya kuweka hizi mashine ambazo kila wakati zitakuwa zinaonekana zimeharibika. Nadhani tuangalie mfumo bora utakaosaidia ili huyu mlipa kodi alipe vizuri na Serikali ipate kipato chake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka nichangie kuhusiana na mapato ni suala la kilimo. Tunakwenda kuua zao la korosho ambalo lilikuwa linaipatia Serikali fedha nyingi sana. Nina mashaka sana inawezekana walioko Hazina pale kuanzia Katibu Mkuu na wengine ambao wana mamlaka hawaijui korosho vizuri. Ndiyo maana zile fedha zikija wanaona hakuna sababu ya kurudisha kule. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, fedha hizi zirejeshwe kwa wahusika wakulima ili ziweze kuzalisha tena. Kwa sababu fedha hizi kama hazitoki kwa ajili ya pembejeo, unategemea msimu ujao wakulima wale watazalishaje zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kule suala la kuanzisha vitalu vile vya kupata mbegu mpya. Wale wote walioandaa zile mbegu bora za korosho ambazo zimesambazwa hawajalipwa hata senti tano na walitumia fedha zao na wengine walikopa benki. Mimi nakubali kwamba ni kweli kuna baadhi yao inawezekana hawakuwa wakweli katika jambo hili lakini huo uhakiki ukishamalizika, basi wale ambao wanatakiwa kulipwa waweze kulipwa fedha zao, sasa uhakiki unafanyika lakini fedha hazirejeshwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wamezungumza hapa kwamba zao hili linahitaji utafiti na zile fedha zilikuwa zinarudi kule zinakwenda kwenye utafiti. Kwa maana hiyo Chuo cha pale Naliendele kitakufa, hawawezi kufanya utafiti kwa sababu hawapati fedha ambazo walikuwa wanapata kutoka kwenye Bodi ya Korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana kabisa kwamba kuna baadhi ya fedha zilikuwa zikirudi kule hazitumiki vizuri. Nashauri uhakiki ufanyike ili zile fedha zirudishwe ili ziweze kuleta tija katika zao hili la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilitaka nizungumzie ni juu ya viwanda. Bahati nzuri na Waziri wa Viwanda yupo, suala la kubangua korosho na kuweka thamani ya korosho ni jambo muhimu sana. Hili jambo tumelizungumza sana sioni progress, sioni kama kuna jambo la msingi linafanyika, tunawanufaisha wenzetu wa nchi za India ambako tunapeleka korosho ghafi, sisi tunategemea kuuza korosho ghafi. Viwanda vipo na ilitakiwa kwanza wale ambao wamechukua wavirejeshe Serikalini ili tupate wawekezaji watakaobangua korosho, lakini hivi sasa hakuna suala lolote la msingi ambalo linafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kuzungumzia ni juu ya ugatuaji wa madaraka kurejesha kwenye Serikali za Mitaa. Tanzania ilikuwa ni miongoni mwa nchi ambazo zimefanya vizuri sana katika Afrika katika suala zima la kushusha madaraka kwenye Serikali za Mitaa. Hivi sasa naona kila Wizara inataka kuchukua mamlaka zote zilizoko kwenye Serikali za Mitaa zirudi Wizarani kwao. Kwa hali hii, Serikali za Mitaa zinakufa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, enzi ya Mwalimu waliwahi kuzivunja Serikali za Mitaa lakini baadaye umuhimu wa Serikali ya Mitaa ulionekana na zilirejeshwa. Tusifike huko kuziua tena Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nilikuwa nashauri kwamba kama tunawaondoa Maafisa Ugani wote kule na wanarudi katika Wizara zao, lazima tutengeneze muundo mpya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutengeneze muundo mpya ambao utafanya Mabaraza ya Madiwani yafanye kazi, lakini kwa sasa katika utaratibu huu Mabaraza yale hayatafanya kazi vizuri.