Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze mchango wangu kwa kuzungumzia mateso wanayoyapata Askari wa Kituo cha Mkokotoni Kaskazini A Unguja. Kituo cha Polisi cha Mkokotoni kiliteketea kwa moto usiku wa tarehe 27 Desemba, 2017 saa 7.30. Ujenzi wa kituo ulianza mara moja kwa lengo jema kujenga kitu bora daraja (A) na kuwaondolea usumbufu askari wetu katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu kituo kiungue huu ni karibu mwaka wa tisa (9) ujenzi haujakamilika. Mazingira wanayofanyia kazi ni magumu sana kiasi cha kuhatarisha afya zao. Mfano mdogo mapokezi (reception) ni banda la mabati juu, chini, pembeni yaani limeezekwa kwa mabati, kuta zake mabati. Wakati wa joto kali askari wanapata shida kwa joto kali kiasi cha kusababisha uharibifu wa ngozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka tisa ni kipindi kirefu kufanya kazi katika mazingira magumu na hatarishi kwa afya za askari. Wabunge tumekuwa tukiuliza sana kuhusu kituo hiki lakini majibu ni yale yale, mwaka wa fedha 2016/2017 ukimalizika unaambiwa 2017/2018 lakini hakuna linalofanyika. Naomba sana na kwa heshima kubwa tuone huruma askari ni binadamu wanahitaji kupewa moyo. Nataka kujua ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa kituo hiki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi niliuliza kuhusu deni la mkandarasi wa ujenzi wa Kituo cha Mkokotoni, Naibu Waziri akajibu bado hajalipwa. Inawezekana kutolipwa kwa mkandarasi huyu ni sababu ya kutokamilika kwa jengo hili. Hata hivyo, huyu ni mfanyabiashara, kumcheleweshea kumlipa ni kumuua kibiashara. Mkandarasi huyu anaumwa, afya yake si nzuri, anataka matibabu hali yake ngumu, je, ni lini Serikali itamlipa deni lake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 25 Septemba, 2017, Mzee Ali Juma Suleiman alivamiwa nyumbani kwake Mtoni Kidatu Unguja saa 5.30 usiku na kundi kubwa la watu ambao wengine wana mapanga, marungu na silaha za moto. Kama kawaida ya mtu yeyote mwenye kuvamiwa aliomba msaada kwa kupiga kelele nyingi pamoja na watoto wake. Ili kuzuia jamii isisogee kutoa msaada zilipigwa risasi za juu, wakamchukua na kwenda kumtesa, akaokotwa kupelekwa Mnazi Mmoja siku ya tatu alifariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kushangaza Zanzibar kisheria umiliki wa silaha za moto ni vyombo vya usalama pekee. Inapotokea tukio kama hili risasi kama tatu mpaka nne zinapigwa halafu vyombo vyote vya ulinzi vinakaa kimya bila wasiwasi wowote, hili linatia wasiwasi mkubwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mzee Ali Juma Suleman alihojiwa akiwa hospitali na vyombo vya habari alisema na kutilia wasiwasi Jeshi la Polisi kuhusika kwao katika uvamizi uliomkuta. Jambo la kusikitisha na kwa mshangao mkubwa mpaka muda huu Jeshi la Polisi halijakamata mtu yeyote kuhusiana na tukio hili. Serikali inatuambia nini kuhusu dhuluma hii mbaya kabisa?