Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia hoja ya hotuba ya Waziri wa Mambo ya Ndani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za askari na vituo vya polisi, Jimbo la Tunduru Kusini ina tarafa tatu katika tarafa hizo ni moja tu Tarafa ya Nalasi ina vituo vya polisi lakini Tarafa ya Lukumbule na Tarafa ya Namasakata haina kituo cha polisi hivyo wananchi wanalazimika kufuata huduma hiyo Tunduru Mjini, zaidi ya kilometa 60 mpaka 80. Tunaomba angalau kila Makao Makuu ya Tarafa kuwa na kituo cha polisi ukizingatia kuwa tarafa hizo zinapakana na Msumbiji hivyo kuna mwingiliano wa watu kutoka Msumbiji na Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vya uhamiaji; Jimbo la Tunduru Kusini limepakana na Mto Ruvuma kwa maana ya Msumbiji kuanzia mwanzo mpaka mwisho, lakini hamna kituo chochote cha uhamiaji jambo ambalo linaleta kero kwa wananchi wa Tunduru mara wanaposafiri kwenda Msumbiji kwa sababu tunaingilia sana kati ya Msumbiji na Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Msumbiji kuna askari wengi sana wa Uhamiaji na polisi wanawanyanyasa sana wananchi wanaovuka mpaka kwenda Msumbiji wakati wao wakija kwetu hamna mtu anayebugudhiwa. Hivyo naomba angalau Kituo cha Uhamiaji katika Kijiji cha Lukumbule ili kuhudumia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Boma la Polisi Lukumbule, wananchi pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ilianzisha ujenzi wa kituo cha polisi Lukumbule tangu 2011, mpaka leo kituo hicho hakijakwisha, limejengwa boma tu halijaezekwa mpaka leo. Hivyo tunaomba Serikali itusaidie kumalizia kituo hicho ili kiwasaidie wananchi wa Kata za Lukumbule na Mchasi ambao wapo zaidi ya umbali wa kilomita 60.

Mheshimiwa Mwenyekiti, makazi ya polisi Tunduru; katika Halmashauri ya Tunduru ilikuwa na makazi ya polisi lakini yaliungua na moto zaidi ya miaka mitano iliyopita lakini nyumba zile mpaka leo hazijajengwa tena na askari wale sasa wanakaa uraiani. Hivyo tunaomba askari wetu wapatiwe makazi ya kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa askari polisi pamoja na vifaa vya kufanyia kazi, Tunduru hatuna polisi wa kutosha kuhimili eneo kubwa la Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru. Hivyo, tunaomba tuongezewe askari ili waweze kuhudumia wananchi wetu pamoja na mali zao. Vilevile kuna tatizo kubwa sana la usafiri, pindi matukio ya uhalifu yanapotokea, askari hawafiki kwa wakati kutokana na tatizo la usafiri. Wakati mwingine hata mafuta ya kuweka kwenye gari wanakuwa hawana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la fedha za uendeshaji wa ofisi; polisi wamekuwa ombaomba wa mafuta kwa ajili ya magari yao kutokana na ukosefu wa fedha za kununulia mafuta ya magari. Hivyo, tunaomba Serikali ipeleke fedha za OC ili polisi wafanye kazi zao kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la rushwa, wananchi wengi sana wanalalamikia Jeshi la Polisi kutokana na rushwa inayoendelea, wananchi kwao limekuwa kawaida kuombwa rushwa mshtaki na mshtakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanasema kuingia polisi bure ila kutoka polisi lazima uwe na pesa. Jambo hili linalichafua jeshi la polisi. Vilevile bado kuna malalamiko ya rushwa kwenye Jeshi la Polisi la Usalama Barabarani kwani kuna askari wa usalama barabarani wamefanya kazi hiyo kama mradi wao wakujipatia kipato kisicho halali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linachafua sana Jeshi la Polisi la Usalama Barabarani; kwa mfano kila basi linalotokea Ubungo linatozwa zaidi ya Sh.20,000 la sivyo gari/ basi halitoki. Vilevile vituo vyote vya ukaguzi vya mabasi kila basi linatozwa Sh.5,000 mpaka Sh.10,000, la sivyo basi linacheleweshwa kwa visingizio mbalimbali. Tunaomba jambo hili likomeshwe. Vitendo hivyo vipo kwenye vituo vyote vya mabasi yanayosafiri kwenda sehemu mbalimbali ya Mikoani na Wilayani.