Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. ABADALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu, muumba wa mbingu na nchi na muweza wa mambo yote. Aidha, nakupongeza wewe binafsi kwa kuliongoza Bunge vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi ni chombo muhimu sana katika kila nchi duniani kote. Ni chombo cha ustawi wa jamii kinachostawisha amani na usalama, kwa mujibu wa sheria za nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa polisi ni chombo kinachotegemewa katika hali zote, ni matumaini ya wananchi wote kupata huduma na utumishi uliotukuka wa Jeshi la Polisi na Vitengo vyake vyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna malalamiko mengi ya Jeshi la Polisi kutumika vibaya au kisiasa zaidi. Naishauri Serikali chombo hiki kitumike vizuri kwa mujibu wa Katiba na Sheria za Nchi. Ikiwa Polisi watafanya kazi zao kwa weledi na kutumia taaluma zao, jambo hili likifanyika vyema amani na utulivu wetu wa nchi utatengamaa. Waepukane na dhana ya kuwa Polisi wanaweka taaluma zao nyuma na kufanya kazi zao kwa kufuata maagizo kutoka upande mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira za polisi, kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu kuhusu nafasi za kuajiriwa vijana katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani hususan Zanzibar yaani Unguja na Pemba. Sote tunafahamu sana kwamba kuna kasma maalum ya nafasi za ajira za Polisi na Jeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila Mkoa kuna idadi yake maalum inayotengewa lakini kuna malalamiko kwamba inapofika wakati wa mahojiano ili kupata nafasi hizo kuna mambo mengi yanayofanyika ambayo sio mazuri ili kuziparanganya nafasi hizo na kukoseshwa nafasi hizo wale wanaostahiki. Yasemekana kwamba watoto wa wakubwa ndio huchukua nafasi nyingi hata kama si wakazi wa mikoa husika. Mambo haya hasa huwa yanatokea Mikoa ya Zanzibar yaani Unguja na Pemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haya yanatendeka naiomba Serikali na Wizara husika kulishughulikia jambo hili ili kuzifanya nafasi hizi ziende kwa walengwa na kuondoa malalamiko ya siku nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matukio ya kihalifu na utekwaji wa raia. Jambo hili ni tatizo kubwa na sasa limekuwa likilalamikiwa sana na raia. Ni ukweli usiopingika jambo hili linaleta usumbufu kwani tuhuma zinakwenda kwa askari wetu na Serikali inalijua lakini jawabu la Serikali ni kwamba matendo hayo huwa yanafanyika au yanafanywa na watu wasiojulikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kwa kutumia weledi wa askari wetu kuwabaini watu hawa wanaofanya matendo haya ya uharamia na kuwabaini watu wasiojulikana na kujua ni akina nani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili la matendo maovu yanayotendwa na watu wasiojulikana tunaiomba Serikali ije na majawabu maridhawa na watu wasiojulikana iwe sasa ni watu wanaojulikana ili ufundi na weledi wa polisi wetu uwe wa manufaa zaidi.