Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na mchango wangu katika Wizara hii kwa kuishauri Serikali kutekeleza miradi yake ya maendeleo kwa wakati hasa miradi ya nyumba za Askari Polisi na Magereza kwani askari wetu kuishi uraiani kunawaondolea weledi wao na pia kuhatarisha maisha yao, kufuatia mazingira ya kazi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na ujenzi wa nyumba za askari vilevile ingeanza ujenzi wa vituo vya polisi vya Wilaya mfano hadi leo Wilaya ya Liwale haina jengo la Kituo cha Polisi cha Wilaya. Jengo linalotumika ni jengo la mtu binafsi ambalo lilipangishwa kwa iliyokuwa Benki ya NBC, jengo hilo sasa ni chakavu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashamba yanayomilikiwa na Jeshi la Magereza hayana hati miliki ya ardhi, mahali pengine hata jengo la magereza halina hati miliki licha ya kuwa na majengo yaliyokamilika. Mfano, Gereza la Wilaya ya Liwale lililoanzishwa mwaka 1982 lakini hadi leo jengo wanalolitumia ni la tope lenye uzio wa miti. Hata hivyo, wenye mashamba yaliyotwaliwa kipindi hicho bado hadi leo hawajapewa fidia za mashamba yao. Gereza lina miaka 36 sasa lakini wenye mashamba hawajapata haki yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma magereza zetu zilikuwa zinajitegema kwa chakula. Je, ni kwa nini sasa magereza zimekuwa mzigo mkubwa kwa Serikali kulisha wafungwa wakati magereza nyingi nchini zina mashamba makubwa na viwanda vya uzalishaji wa bidhaa mbalimbali? Kuna umuhimu gani wa kuwaweka wafungwa magerezani kisha iingie gharama kubwa ya kuwatunza wafungwa hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na ucheleweshaji mkubwa wa upelelezi wa kesi mbalimbali nchini. Jambo hili limekuwa likichelewesha kesi nyingi kuamuliwa mahakamani. Ni kwa nini kesi hizo zisiwekewe muda maalum ili ikifikia muda huo, basi kesi hiyo iweze kufutwa kwani haina ushahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na kesi mahakamani kwa muda mrefu kwa kukosa upelelezi, jambo ambalo linaashiria rushwa na kuwanyima haki raia wema. Hata hivyo, wakati mwingine kuchelewa kwa kesi nyingi ni kutokana na matamko ya kisiasa, kwani wako viongozi wanaowaweka ndani bila maelezo ya kutosha na kuwaamuru askari kuwa hakuna kumwachia huru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutekwa na kupotea watu, kumekuwa na matukio mengi nchini ya kutekwa na kuuawa kwa watu wetu, lakini jeshi la polisi na watu wa usalama wako kimya sana na siyo jeshi la polisi tu, hata viongozi waandamizi ndani ya Wizara hii wamekuwa kimya sana katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matukio ya mauaji nchini sasa limekuwa ni jambo la kawaida. Cha kusikitisha zaidi ni pale Jeshi la Polisi linapohusishwa na mauaji hayo na huku wengine wakibambikiziwa kesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi hili pia linahusishwa na utekaji nyara wa raia wema kwa kisingizio cha taarifa za intelejensia. Jambo hili kama wasemaji wanakuwa kimya jamii huamini kinachoandikwa kwenye mitandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa ni mgumu sana na watu wengi bado hawaelewi kinachofanyika kwani ni zoezi linalochukua muda mrefu sana na wala hatujui zoezi hili litakwisha lini. Kila mwaka fedha nyingi zinatengwa kwenye mradi huu lakini utekelezaji wake ni mdogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendea kazi vya Jeshi la Polisi, kumekuwa na uhaba mkubwa wa vitendea kazi katika Jeshi letu la Polisi hasa upande wa magari, mfano Wilaya ya Liwale haina gari la polisi, Wilaya yenye kata 20, tuna gari moja tu. Ikumbukwe kuwa Wilaya ya Liwale ina kituo kimoja tu cha polisi, hivyo kulingana na Jiografia ya Liwale gari la polisi ni muhimu sana hasa kwa Tarafa za Kibutuka na Makata ambako hakuna vituo vya Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Polisi kuzuia mikutano, kumekuwa ni jambo la kawaida sasa Jeshi la Polisi kuzuia mikutano bila sababu japo Sheria haisemi hivyo. Kwani Sheria inawataka watoe ulinzi kwani hata hao wanaoomba kufanya mikutano wajibu wao ni kutoa taarifa polisi na si kuomba kibali cha polisi, hivyo polisi kuzuia mkutano husika ni kukiuka sheria na kuwanyima raia kupata taarifa mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, polisi kutumia nguvu kubwa, kumekuwa na matumizi makubwa sana katika kuwakamata washtakiwa au watuhumiwa japo bado hawajathibitika kufanya kosa analotuhumiwa nalo. Matumizi haya ya nguvu pasipohitajika yamekuwa yakiwaletea hasara kubwa raia kwa kupoteza mali zao na hata wengine viungo vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya nguvu hizi ni kuwafanya raia wachukie Serikali yao na Jeshi la Polisi kwa ujumla wake. Watuhumiwa wengi hufika vituoni wakiwa na majeraha makubwa na wengine kuibiwa mali zao.