Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kuunga mkono hoja ambayo iko mbele yetu. Pamoja na kuunga mkono hoja hii, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri, ndugu yangu Mheshimiwa Lameck Mwigulu, Doctor kwa kazi nzuri anayoifanya katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Doctor nakupongeza sana. Pia nampongeza sana Naibu Waziri Mheshimiwa Engineer Masauni.

Waheshimiwa Wabunge, mara nyingi jambo ama kiatu usichokivaa huwezi kujua maumivu yake. Nasema hivi kwa sababu gani? Kuongoza Wizara ya Mambo ya Ndani na kuhakikisha kwamba misingi ile ya usalama wa raia inasimamiwa mahali ambapo unawasimamia binadamu wenye hulka na tabia tofauti, kwa kweli ni kazi ngumu na ndiyo maana nasema ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu na Naibu wake wanapaswa kupongezwa kwa kazi hii wanayoifanya katika Taifa letu; na sio wao tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea, kwa dhati ya moyo wangu, nitumie nafasi hii pia kumpongeza sana Kamanda Sirro na timu yake ya Jeshi la Polisi katika nchi yetu ya Tanzania. Ninaposema hivyo, sitaki kumaanisha kwamba askari wetu wote labda ni wazuri, hapana. Ni lazima Waheshimiwa Wabunge tukubaliane, naomba niseme na wala ninaposema haya sitaki kumaanisha kwamba Serikali yetu eti inafurahia askari labda mmoja kwa kutokufuata utaratibu na sheria, akasababisha matatizo makubwa kwenye nchi yetu, hapana. Serikali haisemi hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachotaka wote tukubaliane, kazi nzuri inayofanywa na Jeshi la Polisi kwa namna yoyote ile ni lazima tuwapongeze, tuwaunge mkono na tuhakikishe kwamba tunawatia moyo katika kazi hii ngumu waliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa Kabudi amesema hapa, wameapa kuilinda nchi na wawe tayari hata kufa kwa ajili yetu. Jambo hili siyo dogo, ni jambo zito sana. Kwa hiyo, hata sisi kama Wawakilishi wa Wananchi, tuna kila namna na sababu ya kuwapongeza askari wetu kwa kazi nzuri ya ulinzi na usalama wa raia katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitasema maneno kidogo tu, labda huko mbele nitaomba mwongozo wako baadaye kidogo kwa sababu Mheshimiwa dada yangu Mheshimiwa Mary Muro wakati anachangia amesisitiza sana kwamba kila jambo baya linalotokea kwa Jeshi la Polisi, kila akifuatilia anaambiwa kwamba ni maagizo kutoka juu. Hatupendi kuwe na watu wanaharibu halafu wanasingizia ni maagizo kutoka juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani ili tuweze kushughulika na hao watu wanaoharibu taswira ya Taifa letu, tutaomba angalau tuambiwe tu mmoja ama wawili wanaosema hayo maagizo kutoka juu ili watupe tu ushahidi wa mtu mmoja au wawili kusudi tusichafue taswira ya Jeshi letu la Polisi katika nchi yetu ya Tanzania. Nadhani huko mbele kwa kweli tuondoe jambo hili. Tukiliondoa nadhani tutaweza kulifanya jeshi letu libaki katika misingi ya heshima yake. Hivyo, baadaye tutaomba tu mwongozo Mheshimiwa Dada Mary atusaidie tu ili tuweze kuwa kwenye nafasi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumza sana hapa masuala ya Vyama vya Siasa na nampongeza sana mdogo wangu Mheshimiwa Upendo Peneza, alizungumza Ibara ya tati (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na alitusomea kwamba Jamhuri ya Muungano ni nchi ya kidemokrasia na ya kijamaa isiyokuwa na dini yenye kufuata Mfumo wa Vyama Vingi vya Siasa. Ni kweli kabisa Ibara ya tatu (3) inasema hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukienda Ibara ya 3(2) inasema:-

“Mambo yote yanayohusu uandikishaji na uendeshaji wa Vyama vya Siasa nchini yatasimamiwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na sheria iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo sheria iliyotungwa na Bunge Cap 258 ambayo ndiYo inasimamia uhuru huo wa Vyama vya Siasa vyote vilivyosajiliwa katika nchi yetu ya Tanzania. Ukienda kwenye kifungu cha 11 cha hiyo Sheria ya Vyama vya Siasa kwenye suala la mikutano ya hadhara, limetolewa maelezo mazuri sana tu. Maelezo haya kama vyama vyote vya siasa vingekuwa vinayafuata, tusingefika katika hii migogoro na kuwasababishia Polisi kama ndio vyanzo vya kuharibu amani katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakubaliana na ushauri wako uliousema asubuhi, Waheshimiwa Wabunge tukiweza kuisoma katiba kwa ujumla wake, lakini tukaweza kusoma na sheria zilizotungwa kwa mujibu wa Katiba, ninaamini kabisa hakuna mtu ambaye ataingia kwenye mgogoro na Jeshi la Polisi kwenye nchi yetu ya Tanzania. Kwa mfano, kifungu cha (5) cha Katiba, kinaeleza kabisa haki ya kupiga kura na uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa utaratibu wa kisheria wa uchaguzi uliowekwa, baada ya uchaguzi Jenista anakuwa amechaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho na mwingine, kila mtu anakuwa tayari ni mwakilishi kwenye Jimbo lake husika. Inapendeza; na kwa mujibu wa taratibu tulizojiwekea na hasa kwenye sheria hii, nimesema kifungu cha 11 ukikisoma, kila Mbunge awajibike kwenye Jimbo lake kwa wananchi waliomchagua. Ukishachaguliwa kwenye Jimbo husika, yapo mambo mengi ambayo wananchi wako wanatarajia utawawakilisha inavyopasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukisoma kifungu hicho cha 11 nenda kwenye kifungu kidogo cha (2) utapata maelekezo kabisa hapa, wajibu wa Polisi kutumia sheria walizonazo katika kusimamia masuala yote ya mikutano ya hadhara; iko wazi kabisa na wala haihitaji ugomvi wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwetu sisi Wanasiasa wote kutambua haki za Kikatiba lakini kwenda kwenye wajibu wa Kikatiba kama Ibara ya 25 ya Katiba inavyosema, kila mtu ana haki lakini ana wajibu katika nchi yetu kuhakikisha anazingatia sheria za nchi zilizowekwa kwa misingi ya Katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, naomba sana Vyama vya Siasa vifanye yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, vijielimishe zaidi kuhusu katiba tuliyonayo katika nchi yetu ya Tanzania; pili, vijielimishe kuhusu maana na muktadha wa sheria ambazo zimetungwa kwa kuzingatia Katiba tuliyonayo; na tatu, Vyama vya Siasa vijifunze utii wa sheria bila kushurutishwa. Tukifanya hivi nadhani tutaweza kuwa tunaenda vizuri na hatutakuwa na migongano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vyama vya Siasa vikubali kuwa sheria kwa kweli ni msumeno na itakata kila chama; iwe ni Chama cha Mapinduzi, CHADEMA, CUF, ni kila mahali. Ni lazima tunapofika kwenye suala la kuheshimu sheria, kila kiongozi na kila chama kijue kwamba kina wajibu wa kuheshimu sheria kwa mujibu wa Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tujitafakari sisi kama viongozi, tumepewa dhamana, tuna kila namna ya kuheshimu dhamana tulizopewa na wananchi katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeaminiwa, lakini tunategemewa na Watanzania. Tunapokiuka miiko ya kisheria na dhamana tulizopewa, hatutendei haki dhamana tulizopewa wala hatutendei haki Katiba wala sheria ambazo tumezitunga wenyewe Wabunge ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, navipongeza vyama vile ambavyo kwa kweli vimeonyesha ukomavu wa kisiasa. Ukiangalia kama kaka yangu Mheshimiwa Mbatia na chama chake huwezi kukuta kwamba kimekuwa na migogoro; na vyama vingine vingi. Kwa hiyo, unaona kabisa kwamba viko vyama unavipima tu na unaona kwamba vimetambua hii mipaka ya demokrasia ilivyo, sheria tulizonazo na Katiba ya nchi yetu ya Tanzania. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuvihimiza vyama kwa mujibu wa sheria tulizonazo na kwa mujibu wa Katiba, hakika tunapaswa kuheshimu sheria, tunapaswa kuheshimu Katiba tuliyonayo. Tukifanya hivyo, tutawawakilisha wananchi wetu vizuri sana na hakutakuwa na haja ya kugongana na vyombo vyovyote vinavyosimamia usalama wa raia katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, IGP na timu nzima ambayo inasimamia usalama katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.