Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuhitimisha hoja kwa kusemea hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge walizitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa niseme kwamba hatutaweza kuzijibu hoja zote kwa muda huu, lakini Waheshimiwa Wabunge kwa ujumla wao wametoa hoja nzuri, hoja nzito na sisi kama Wizara zile ambazo zimekaa kwa muundo wa ushauri tumezichukua tutazifanyia kazi na zile ambazo zipo kwa maandishi tutaweza kujibu kwa maandishi. Nia yetu sote ni ya kujenga na tunakubali sana hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na suala la hoja zilizotolewa kwenye upande wa Jeshi la Zimamoto, kimsingi zilikuwa linaongelea kuhusu vitendea kazi na umuhimu wa Jeshi letu hili la Zimamoto. Tumepokea jambo hili na bahati nzuri umelikazia sana jambo hili tungali kwenye Kamati na tumelipokea ndani ya Serikali na tunaendelea kufanya mawasiliano kuweza kuhakikisha kwamba tunakamilisha viporo vile ambavyo ni vya ununuzi wa magari lakini pamoja na maeneo mahsusi yakiwemo ya majengo na kama ambavyo umetoka kusema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yale yanayohusu sare za Askari wetu Waheshimiwa Wabunge wamesema kwa hisia tumepokea na tunaendelea kuyafanyia kazi na hatua za mwanzo zimeshaanza zinazohusisha sare ili Askari wetu waweze kupata sare na waweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yale yanayohusu kuweka miundombinu ya kisasa ili Jeshi la Zimamoto liweze kufanya kazi hizo na yenyewe tumeendelea kufanya mawasiliano ndani ya Serikali na kuwezesha mazingira yawe rafiki ili Jeshi la Zimamoto liweze kufanya kazi vizuri. Mambo haya yanahusiasha masuala ya ujenzi, masuala ya ujenzi wa miundombinu kama maji pamoja na vitendea kazi vingine ambavyo vinatumika katika masuala mazima ya kazi kuhusu Jeshi letu la Zimamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaendelea kutoa elimu na wananchi waweze kutambua kwamba pana mambo ambayo ni ya msingi ya kuzingatia kabla moto haujatokea ama kabla janga halijatokea ambayo yanafanya ufanisi uwe mkubwa punde janga linapotokea tofauti na ilivyo sasa ambapo mambo hayo yasipozingatiwa huwa yanakuja kuleta upungufu katika utekelezaji wake punde janga linapotokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili si tu la Wizara wala si tu Jeshi la Zimamoto na wala siyo tu la Wabunge ni jambo la nchi nzima, kuzingatia masuala ya tahadhari kwenye masuala ya moto kabla moto haujatokea ama kabla janga hilo halijatokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwa upande uhamiaji jambo hili limesemewa sana na Waheshimiwa Wabunge, tunawapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa kutambua kwamba kwanza kazi nzuri inayofanywa na Jeshi letu la Uhamiaji, lakini na kazi nzuri ambazo zinafanywa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata huduma na kila mmoja amekiri kwamba kazi hizo zinafanyika vizuri na niendelee kusisitiza hata Wabunge tusiondoke hapa Dodoma kabla hatujapata passport zetu za kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Waheshimiwa Wabunge ambao tayari wameshapata passport zao, zoezi hili ni jepesi tu ukichukua zile alama asubuhi baada ya nusu saa ama dakika 40 taarifa zote zinakuwa zimeshaingia kwenye mfumo na order ya ku-print inafanyika na kwa mazingira maalum tumeshaliongelea kwa wale ambao watahitaji mazingira maalumu tutayafanya kwa umaalum huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja ambalo niliona nilisisite sana na nilifafanue na nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge tuelewane vizuri kwa sababu sisi ndiyoi tunakaa na wananchi ni hili suala la uraia na watu kuhojiwa panapotokea masuala ya passport, licha ya kwamba wapo ambao walishapata passport zilizopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imepita katika hatua tofauti kuhusu utambuzi wa uraia, jambo hili la uraia ni jambo la kisheria siyo jambo la jiografia wala siyo jambo la hisia ni jambo la kisheria. Hata hivyo, kwa wananchi wetu wengi wengi bado tunaenda na jambo la historia pamoja na jambo la jiografia. Hata wengine wapo ambao nimeongea nao mimi mwenyewe wakisema wazazi wangu walizaliwa Tanzania ama wazazi wangu walikuja wakati wa uhuru na wengine wa rika letu wakisema mimi nimezaliwa Tanzania nitakuwaje siyo Mtanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili wala siyo la ugomvi na nitoe rai kwa Watanzania tuelewane kwamba, ni jambo la kisheria na panapotokea mambo yanayohusu sheria ni vema tukafanya marekebisho yake. Jambo hili liko namna hii, mwanzoni tulikuwa na sheria iliyokuwa inatambua mtu aliyezaliwa ndani ya Tanzania kuwa raia wa Tanzania na nadhani kuna nchi ambazo zina utaratibu huo kwamba raia yeyote aliyezaliwa ndani ya jiografia ya eneo husika la nchi hiyo anakuwa raia wa nchi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwenye nchi yetu tulienda hatua zaidi za kisheria ambazo zinamtambua raia wa Tanzania si tu kwa kuwa alizaliwa ndani ya eneo la Tanzania bali awe amezaliwa na mzazi mmoja aliye raia wa Tanzania. Yule aliyezaliwa na mzazi mmoja aliye raia wa Tanzania analazimika na yeye atapofika miaka 18 aweke wazi kama anataka kuwa raia wa Tanzania ama anafuata uraia mwingine ambao ni wa mzazi asiye Mtanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, tuna idadi ya Watanzania ambao katika kipindi fulani waliwahi kuwa na passport za Tanzania. Hata hivyo, sheria ilipokuja kutambua kwamba raia wa Tanzania lazima awe amezaliwa ama na mzazi mmoja wa Tanzania ama wazazi wote wote wa Tanzania wale ambao walishapata hata hizo passport wanalazimika kurekebisha uraia wao ili waweze kuendana na masharti ya kisheria. Ni masharti ya kisheria na sheria tumetunga wenyewe wala Idara ya Uhamiaji siyo iliyotunga na masharti ya sheria ambazo zimetungwa na Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa wale ambao ama wazazi wake walikuja Tanzania na yeye akazaliwa na wazazi wakiwa bado hawajawa Watanzania ana wajibu wa kurekebisha status yake ya uraia ili aweze kuwa raia wa Tanzania wa kisheria. Watu wa aina hii hawana masharti magumu kwa sababu tunatambua kwamba hawana nchi nyingine, nchi yao ni hii kwa maana ya kwamba wamezaliwa hapa hawana nchi nyingine. Tunachofanya ni kuweza kurebisha status zao za kisheri na hata gharama zao ni tofauti na wale watu wanaokuja kuomba uraia wa Tanzania kwa kutokea Mataifa mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nitoe rai watu wanapoona kwamba kuna jambo la kosoro kwa upande wa masharti haya ya kiuraia wasichukulie kama ni jambo la ugomvi, wachukulie ni jambo la kisheria na wanachotakiwa kufanya ni kupewa ushauri, kupewa mwongozo na wao wafuate mwongozo huo ili kuweza kurekebisha matatizo ya aina hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo liliongelewa amelisema sana Mheshimiwa Mwilima na ameliongea kwa hisia sana kuhusu masuala ya watu kuhojiwa masuala ya uraia na akasemea sana kuhusu watu wa mipakani. Serikali kwa sasa inafanya zoezi kubwa sana ambalo litaenda kumaliza matatizo hayo ambayo yamekuwa yakiwapata wananchi wa mipakani kwa kutokutambulika ama kwa kupata kashikashi za kutiliwa mashaka. Zoezi la vitambulisho vya Taifa linaloendelea litakapokuwa limemalizika na kila Watanzania wakatambulika tutakuwa tumeshapata jawabu la nani si Mtanzania na nani ni Mtanzania, kwa hiyo na hiyo itaenda kuondoa bughudha hizo ambazo zimekuwa zikijitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge ameileta hoja kwa uzito mkubwa na alishaileta hata Ofisi tumeipokea na tutayafanyia kazi na hasa haya ambayo aliyoyasemea ambayo yanahusu utendaji kazi hasa aliposemea kuwa kuna watu wanadaiwa fedha ili waweze kuandikishwa vitambulisho hivyo vya Taifa. Jambo hilo ambalo halijatolewa maelekezo kwamba wafanye hivyo tunachukulia kama masuala ya kimaadili na tutafuatia nimeshaelekeza timu ya Wataalam, nimeshaelekeza idara inayohusika waweze kufuatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili alilileta Mheshimiwa Mbogo pia kutoa Mkoa wa Katavi pamoja na Wabunge wengine ambao jambo hili lilijitokeza katika mazingira ya aina hii. Ikitokea mmoja mmoja akafanya hivyo siyo maelekezo ya Wizara na wala siyo mpango wa Wizara kufanya hivyo, atakuwa ametokea mtu mmoja akapotoka na sisi wakitokea watu wa aina hiyo tutachukua hatua zinazostahili. Kwa hiyo, tuendelee kuwasiliana, kupeana maendeleo ya jinsi zoezi hili linavyoendelea ili tuweze kulifanya zoezi la ufanisi mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine lililojitokeza linalohusiana na masuala ya uraia pamoja masuala ya vitambulisho vya Taifa alilisemea ndugu yangu Mattar Ali Salum, aliposemea kuhusu kitambulisho cha Mzanzibari vis- a-vis kitambulisho cha NIDA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba kitambulisho cha Mzanzibari kinatambulika ni kitambulisho halali kimetumia gharama za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuweza kutengenezwa. Wizara idara hizi ambazo ziko ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinafanya kazi kwa pamoja, lakini maelekezo tuliyoyatoa ilikuwa tu ni kwamba maadam kwa Zanzibar uandikishaji wa kitambulisho cha NIDA umeshafanyika kwa zaidi ya asilimia 90 na kwa kuwa taarifa hizo zinasoma upande NIDA pamoja na Idara yetu ya Uhamiaji tuliona tuwapunguzie Watanzania usumbufu wa kutoa taarifa kama tayari walishatoa taarifa, waweze kutumia taarifa hizo ambazo tayari zimeshapatikana ili kuweza kuwapunguzia mlolongo wa kuendelea kuulizwa taarifa zilezile ambazo wameshatoka kuzifanya huku database zetu zikiwa zinasomana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haikuwa nia mbaya ya kutaka kutokutambua kitambulisho cha mkazi ama kutokutambua juhudi ambazo zimefanywa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, lakini ilikuwa ni kuweza kutumia data ambazo zimeshafanyika. Kwa Zanzibar zoezi la utambuzi na uandikishaji wa vitambulisho vya Taifa limeshafanyika kwa kiwango kikubwa mno na ndiyo maana tuliona tuanze zoezi hilo la kuanza kuoanisha data ambazo tumeshazipata kwa ajili ya Watanzania wetu, kuliko kila wakati kuwa tunatumia utaratibu wa kuanza kumhoji Mtanzania upya ilihali akiwa ameshatoa taarifa hizo katika ofisi ya Serikali ile iliyo moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Magereza zilijitokeza hoja nyingi, moja zinazohusu mambo ya sare, tayari zabuni ya upatikanaji wa sare imeshafikia hatua za mwisho na inafanyika ndani ya nchi hapa kwenye viwanda vinavyotengeneza majora hapa na hatua zitakazofuata sasa itakuwa ni ushonaji, vijana wetu wataenda kupata sare na baada ya vijana wetu kupata sare tutazingatia pia na suala la wafungwa ambalo na lenyewe lilisemewa kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo niliona niliweke sawa, Mheshimiwa Mbunge nadhani Mheshimiwa Mary Deo Muro wakati anachangia alisemea masuala ya watoto. Ni kweli kuna watoto ambao wazazi wao wanatumikia vifungo mbalimbali, kwa sasa watoto ambao walishachukuliwa na ndugu zao kwa takwimu zilizopo sasa ni sita, watoto walioko magerezani ni kama 45 na wafungwa wajawazito ni 37.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja tu naomba Bunge lako Tukufu lipate kumbukumbu zilizo sawa, hakuna mimba zinazopatikana gerezani. Narejea tena hakuna mimba zinazopatikana magerezani, kuna akinamama wajawazito ambao wamepata ujauzito kabla hawajaanza
kutumikia vifungo, kwa maana hiyo zinafuata taratibu za kisheria, kwanza mtoto akiwa bado mdogo kwa umri ambao akina mama mnajua, analazimika kuwa na mama yake. Akiwa katika umri ambao unamruhusu mtoto kutenganishwa na mama inafuata tu utaratibu kama ndugu atawepo atakayejitokeza kumpokea mtoto yule wanampokea, lakini kama ni upande wa Ustawi wa Jamii na yenyewe anaenda kupokelewa kufuatana na makubaliano yanayokubalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo lilijitokeza, lilikuwa la masuala ya kulifanya Jeshi la Magereza kujitegemea. Jambo hili Wizara tumepokea ushauri huu na jambo hili tayari Mheshimiwa Waziri Mkuu alishalitolea maelekezo, tulishakaa tutaanza kwa mfano, kwa Magereza yaliyo na maeneo makubwa kuweza kufanya utaratibu wa kulima kwa kisasa na tayari Mheshimiwa Waziri Mkuu alishaelekeza utaratibu wa kuyaunganisha matreka utakapokamilika tutaanza na 50 kwa upande wa Jeshi la Magereza ili kuweza kuhakikisha kwamba tunalima kwa kisasa na tunalifanya Jeshi la Magereza liweze kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo haya Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyaelekeza kwa uzito mkubwa na mara kadhaa Mheshimiwa Rais ameelekeza kuhakikisha kwamba hatuchukui fedha ambazo zingetumika katika maeneo mengine kwenda kulisha wafungwa na badala yake Jeshi la Magereza lijitegemee na ikiwezekana hata likatoa huduma zinazotokana na uzalishaji wake katika maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Wizara tumezingatia na tumeshaanza miundombinu kama hii niliyoisemea, tukianza na tunalenga Gereza la Songwe, Kitengule, upande wa Ludewa, Isapilo pamoja na maeneo mengine ambayo ipo miundombinu ya asili ama miundombinu ya awali ambayo italiwezesha Jeshi la Magereza kuweza kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazingatia ushauri ambao umetolewa na Waheshimiwa Wabunge kwenye upande wa kuboresha masuala mazima yanayohusu magereza ili tuweze kuhakikisha kwamba tunavuka hatua hii tuliyonayo tuweze kwenda ngazi zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazingatia masuala ambayo yamesemewa ya kiutumishi ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema masuala yanayohusu masuala ya kiutumishi, masuala ya maslahi kwa vijana wetu, tunaendelea kuyafanyia kazi na hii kwa sababu tuna mambo tunaendelea kuyafanyia kazi yatakopokuwa yamekamilika, tutafanya utaratibu rasmi wa kuweza kuliarifu Bunge lako ama kupitia Kamati ili tuweze kuwa na uwelewa wa pamoja kwa jinsi ambavyo tutakuwa tumeshafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni jambo ambalo lina umuhimu mkubwa sana ukizingatia kazi wanazofanya vijana wetu na tunaheshimu kazi wanazofanya, tunaheshimu mchango wanaoufanya na tunaheshimu moyo wao wa kujitoa kwa uadilifu na kwa uaminifu mkubwa katika kulitumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala yaliyoongelewa yanahusu maslahi ya askari wetu haya ni mengi, tutakapokuwa tumeyashughulikia tutaendelea kupeana taarifa ili tuweze kuhakikisha kwamba Waheshimiwa Wabunge hoja zao wanaona kuwa tumezifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo lilijitokeza Mheshimiwa Maige alisemea kuhusu Muswada wa Ulinzi wa Sekta Binafsi. Jambo hili tumeshalipokea na Serikali imeshafanya nalo kazi kubwa, tayari Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kushirikiana na wadau ilishaandaa rasimu ya mapendekezo ya kutunga sheria na hatua kubwa zilishafanywa kuhusu utaratibu wa rasimu wa kutunga sheria, kwa Tanzania Bara tayari yalishakamilika na maoni ya kutoka Zanzibar yalishakusanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatarajia mpaka ifikapo mwisho wa mwaka huu tutakuwa tumeshafika hatua nyingine ambayo inaelekea kwenye utungwaji wa sheria hiyo ikiwepo kupitia Cabinets Secretariat pamoja na Baraza la Mawaziri ili jambo hili ambalo Mheshimiwa Mbunge amekuwa mdau mkubwa na amekuwa akitoa maoni mazuri liweze kutimia na hatimaye liweze kuchangia katika maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka michango mizuri iliyotolewa na Wabunge kuhusu masuala ya magereza Mheshimiwa Omari Kigua, Mheshimiwa Deogratius Ngalawa, Mheshimiwa Maige mwenyewe, Mheshimiwa Maryam Msabaha, Mheshimiwa Rhoda Kunchela, Mheshimiwa Shekilindi, Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko pamoja na wengine wote ambao wameongelea masuala haya yanayohusu masuala ya magereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, orodha ninayo ndefu sana ikiwemo Mheshimiwa Amina Makilagi, Mheshimiwa Magdalena Sakaya, Mheshimiwa Zacharia Issaay ndugu yangu wa kutoka Mbulu na Mheshimiwa Zuberi pamoja na wengine, tumepokea hoja zenu zote tutazifanyia kazi, tutachambua moja baada ya nyingine, yale ya kiushauri tutayafanyia kazi na yale ambayo ni maelekezo tutapokea tuweze kuyafanyia kazi kwa sababu ni maoni mazuri na tunaamini yatatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo Waheshimiwa Wabunge walilizungumzia sana ni hili la vijana wa bodaboda. Kwanza kuna mambo ambayo sote tunakubaliana. Moja ni kweli, matumizi haya ya bodaboda ama usafiri huu wa bodaboda umetengeneza ajira nyingi sana kwa vijana wetu, hakuna Jimbo hata moja ambalo hawana bodaboda. Katika kuzunguka kwangu kila eneo kuna bodaboda. Kwa maana hiyo ni kweli jambo hili limetengeneza ajira kwa vijana wetu wengi sana hili hatubishani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni kweli kwamba jambo hili la usafiri wa bodaboda linaajiri vijana wengi sana na wengine wanafanya shughuli hizi za bodaboda wakiwa wamepata uelewa mdogo sana kuhusu matumizi ya vyombo vya moto. Hili wala hatubishani nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara tumeelekeza maeneo yote, mikoa yote kuwapa elimu vijana hawa wanaofanya shughuli hizi za bodaboda, lakini changamoto tunayokutana nayo kwa sababu ni wengi na wanaoingia kwenye sekta hiyo wanaingia karibu kila siku, kwa hiyo hakuna mkoa ambao unaweza ukasema umefanya mafundisho hayo na kuyamaliza kwa sababu wanaingia kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wengine ambao wanaazimana pikipiki ndani ya muda mfupi Wizara tunaendelea kulikazia kwamba jambo hili ni la kijamii wala siyo jambo tu la Wizara na hata Waheshimiwa Wabunge ni vema tukawaambia wananchi wetu kwamba hili ni jambo la kijamii na tukaliongea kama mambo mengine ambayo huwa yana athari kubwa katika jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema yanaathari kubwa kwa sababu ukienda kwenye takwimu ni kweli kwamba vijana hawa wengi wanaumia, wengi wanapata ulemavu wa kudumu, wengi wanapoteza maisha, wengi wanapoteza maisha ya abiria waliokuwa wamewabeba kwa sababu ya haya niliyoyasema ya kujifunza muda mdogo, kutokuwa na uelewa wa matumizi ya vyombo vya moto, kutokuwa na matumizi ya barabara ambapo kuna vyombo vingine vya moto na mambo haya yanasababisha hasara kubwa kwa Taifa letu kwa sababu yanapunguza nguvu kazi za vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja ambalo nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge, kwa yale ambayo yanafanyika kwa utaratibu wa ukamataji ambao unasababisha ajali zingine au unaleta madhara hiyo tutaelekezana ndani ya Ofisi kuweza kuzingatia utaratibu bora wa ukamataji ili kuweza kuwalinda vijana wetu hawa wakati tukiendelea kuwafundisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitoa maelekezo hata nilipokuwa Tanga naendelea kusisitiza pia kwamba vijana hawa wengine wamepata mikopo, lakini pia wanatengeneza ajira. Tumesema kwa wale ambao tunafahamu walipo tusichukue njia ya kuona ni vema pikipiki hiyo ikaozea kituoni kwetu badala ya kuwapa na kuwataka walipe gharama zile ambazo wanatakiwa walipe. Huu ni utaratibu ambao unatumika hata katika nchi zilizoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zilizoendelea mtu akifanya kosa kama ana gari halazimiki ku-park gari ile mpaka alipe gharama ile anayodaiwa. Anapewa kwamba unatakiwa ulipe gharama hii na anapewa muda kwa hiyo hata upande wa bodaboda nimeelekeza wakishamtambua na kituo chake kinatambulika na kosa ameshaelezwa alilokosea apewe pikipiki yake, aendelee na kazi lakini aelekezwe kwamba unatakiwa ulipe, pia unatakiwa usifanye makosa ya aina hiyo ili kuepuka kugeuza ofisi zetu kuwa ni karakana ama kuona ni vema pikipiki yake ikaozea pale kwa sababu hajaleta Sh.60,000 pikipiki ambayo ilinunuliwa kwa zaidi ya milioni mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tunaendelea kuongea na wenzetu wa Wizara ya Fedha kutofautisha faini kwa pikipiki hizi ukilinganisha na magari, kwa sababu kwa kweli kuweka faini ile ile kwa Basi ama Coaster iliyobeba watu 20 ama 30 inavyopita kwenye kosa moja la barabarani utoze faini sawa sawa na pikipiki iliyobeba mtu mmoja ndiyo tunawafanya wale vijana wanashindwa kuzikomboa pikipiki zao na kuzifanya ziendelee kubaki katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja tu ambalo ni vema tu likawa wazi, kuna makosa ambayo pikipiki zile zimebaki kama ushahidi. Kwa mfano, kama pikipiki mtu alibeba watu wa madawa ya kulevya ama watu waliofanya uhalifu wa matumizi ya silaha, ama watu waliofanya ubakaji na makosa mengine makubwa makubwa, ambapo pikipiki hizo zinatakiwa ziende kama ushahidi kwenye taratibu zingine za kisheria, hayo yanatakiwa yaendelee kubaki hivyo hivyo ya ukubwa wa makosa na uhitaji wa pikipiki hizo katika kesi ambazo zinatakiwa zisonge mbele. Kwa yale ambayo tunaweza tukayamaliza kwa kuonyana na masuala ambayo hayakuwa na athari ndiyo hayo ninayosemea, akishajulikana na kituo chake kinajulikana waruhusiwe kuendelea na kazi huku wakiwa wamepewa lini wanatakiwa wamalize kufanya malipo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda upande wa Jeshi la Polisi. Moja ya mambo ambayo yamejitokeza kwa kiwango kikubwa, nikianza na suala la watu kupotea, suala la mauaji, Waheshimiwa Wabunge wameongea kwa hisia kubwa sana. Nikianza na matatizo haya yaliyojitokeza kwa siku za hivi karibuni, nianze kwa kumpa pole sana Mheshimiwa Heche kwa kuondokewa na Ndugu yake na kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wametolea mfano, hatua zimeshachukuliwa kwenye jambo hilo na taratibu za kisheria zitafuata mkondo wake. Nitoe pole pia kwa familia na jamaa wengine ambao wamepatwa ama wameguswa na matatizo ya aina hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilihakikishie tu Bunge lako Tukufu kwamba panapotokea matatizo ya kiutendaji ya aina hiyo, hayo siyo maagizo na wala siyo maadili ya Jeshi la Polisi, inakuwa imetokea mtu mmoja katika upungufu wake wa kibinadamu anafanya hivyo na akishafanya mmoja siyo maelekezo ya Wizara wala siyo maelekezo ya Jeshi la Polisi na kwa maana hiyo yanapofanyika hiyo ambayo yanakiuka maadili, mara zote sisi kama Wizara na kama Jeshi la Polisi tunachukua hatua kwa wale wanaofanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua za aina hiyo kwa watu wanaofanya makosa hilo ni kosa kubwa lililopitiliza, lakini yapo na mengine yanayofanyika ambayo yanatambulika kwamba yanakiuka maadili namiiko ya utendaji wa kazi kila wakati taratibu za kisheria na taratibu za kijeshi zimekuwa zikichukuliwa ili kuweza kauhakikisa kwamba wananchi wananufaika na uwepo wa Jeshi la Polisi na wanafurahia uwepo wa Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mambo mengine yaliyoongelewa, tulitaka kuingia kwenye mtego wa kuona kama vile tuna madaraja ya Watanzania. Ni vema sana Bunge lako Tukufu likaelewa vizuri sana kwamba hapa Tanzania wananchi wote walioko ndani ya mipaka ya Tanzania, kwanza ambalo ni kubwa kuliko yote, tulipozaliwa tulizaliwa wanadamu hilo ni la kwanza. La pili ikafuatia kwamba atakuwa amezaliwa mwanadamu amezaliwa Mtanzania baadae anatambulika anatokea eneo (a), baadae anatambulika anatokea imani (a), baadaye anatokea anatambulika imani ya Chama (a), lakini la kwanza ambalo ni kubwa kuliko yote tumezaliwa wanadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukishazaliwa mwanadamu, damu ya mwanadamu haiwezi ikalinganishwa na gharama ama na thamani ya Chama chochote cha Siasa, haiwezi ikalinganishwa na thamani ya imani yoyote wala haiwezi ikalinganishwa na thamani ya kabila lolote. Kwa maana hiyo, hii dhana ya kwamba labda kuna utaratibu wa watu kutokupewa uzito ulio sawa kutokana na ama vyama vya siasa, ama kabila, ama dini, hiyo dhana siyo njema ikawepo katika nchi yetu. Ni dhana potofu na Serikali tunalinda usalama wa raia wote wa nchi yetu na hivyo ndivyo ambavyo tumekuwa tukifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea haya masuala na huku tukiwa tunaongelea katika kipindi ambacho kuna watu wengine wameguswa na matatizo kama hili tulilosema, ni vema sana tukahifadhi utu ambao unawahusu watu ambao wamepatwa na matatizo ya aina hiyo. Tukijumuisha tu kwamba kuna watu wamepotea, wameuawa, moja siyo dhana sahihi nitawapa sababu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, katika kipindi hiki kuna mambo mengi ya kimaadili ambayo tumeyafanyia msako. Kuna watu wengine hawako kwenye familia zao kwa kukimbia misako ya ushiriki kwenye madawa ya kulevya, wapo ambao tunaendelea kuwatafuta mpaka sasa ambao wapo kwenye orodha ya watu wanaojihusisha na madawa ya kulevya na wengine tumeambiwa hata wameshavuka mipaka ya nchi yetu. Sasa mtu wa aina hiyo ambaye ameshiriki kwenye madawa ya kulevya, tunamtafuta, amekimbia familia yake, akitokea mtu akisema mtu huyu haonekani kwamba ameuawa na mtu huyu kwamba haonekani kwamba anatafutwa, ukituuliza yuko wapi nasi tunakuuliza yuko wapi tunamtafuta, kwa sababu tunaendelea kufanya msako wa watu wote wanaofanya vitu vya aina hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, tumefanya msako ya watu ambao wamefanya uhalifu kwa kutumia silaha maeneo tofauti tofauti, tumefanya mapambano hayo. Kuna wengine ambao tuliwakamata wanaendelea kuwataja wenzao waliokuwa wanafanyakazi hizo pamoja wakiwa wanatumia silaha, tumewasaka watu wa aina hiyo na watu wa aina hiyo wengine tunaambiwa wameshavuka hata mipaka ya nchi yetu, wapo watu wa aina hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama watu wanatumia silaha na wenzao tumeshawakamata na wamekimbia, wametorokea mipaka ya mbali ama wako nje ya mipaka ama popote pale walikojificha, kama tunaendelea kuwatafuta kwa uhalifu huo, ukituuliza kwamba kwenye familia hii huyu mtu yuko wapi nasi tutakuuliza yuko wapi tunamtafuta, kwa sababu wale wote wanaofanya uhalifu nasi tunaendelea kuwatafuta watu wa aina hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, ukijumuisha tu watu wote wambao hawako kwenye familia zao ukasema wamekufa that is totally wrong over generalization. Kwa sababu hata sasa hivi, Watanzania ambao wako wanashikiliwa nchi zingine kwa kushiriki kwa madawa ya kulevya wako kwenye magereza ni zaidi ya 1,000. Hivi sasa watu wa aina hiyo, familia za aina hiyo, hao watu wao hawapo, wewe ukisema tu kwamba watu wa aina hiyo wameuawa, that is wrong kwa sababu kuna watu wako na makosa mbalimbali, lakini hata ondoka zao wanaondoka kwa njia ambazo ziko tofauti tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, kuna kijana mmoja siku moja nilitembelea gerezani nikaenda kuongea naye akakiri kufanya matukio ya uhalifu, alitaja zaidi ya matukio matano ya uhalifu. Walipochukua silaha Bukombe akasema na mimi nilikuwepo, walipoua Askari pale Sitakishari akasema na mimi nilikuwepo, waliposhiriki matukio ya Mbagala pale akasema na mimi nilikuwepo, akasema lakini naomba kama utanihakikishia niendelee kukwambia, nikamwambia nimekuhakikishia sema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, akasema Mheshimiwa mimi nimeshiriki sana haya matukio hata kwenye utekaji wa basi kutoka Itigi kuelekea Makongorosi hadi Mbeya mimi nilikuwepo. Akasema tuliteka Sekenke nilikuwepo lakini akasema Mheshimiwa Waziri jambo moja tu, katika hizi kazi tulizofanya, ilikuwa kila tukifanya shughuli hizo, katika mapambano wengine wanauawa. Akasema mimi mnihakikishie kwamba mtanisamehe, nimeshaacha kufanya hivyo, yuko gerezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama watu wengine ambao wako gerezani wanasema mwingine huyu tumefanya naye tukio hapa akauawa, mkija mkauliza tu kwamba kuna watu hawa hawapo, mmeshachukua takwimu za wahalifu? Mmeshachukua takwimu za madawa ya kulevya? Mmeshachukua takwimu za wale ambao tunawatafuta mpaka sasa ambao wameshiriki kwenye uhalifu wa silaha? Mmeshachukua takwimu za wale wengine ambao wamekimbia tu wako kwenye mafunzo ya mambo ya uhalifu katika maeneo mengine? Waheshimiwa Wabunge, ni vema sana jambo ambalo linahusu masuala ya usalama tukayabeba kwa umakini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, IGP, kama tunasema kuna watu tunawatafuta, tunasema kuna watu wamekimbia na tunasema kuna watu wameshiriki kwenye uhalifu na tunasema hakuna mtu ambaye ameuawa, kama kuna mtu anayesema kuna mtu ameuawa ni vema sana akajitokeza akaenda akasaidia jambo hilo kwa sababu mambo ambayo yanatokea ya kiuhalifu tunahitaji kuyashughulikia, kwa sababu kuua mtu asiye na hatia ni uhalifu na kama kuna mtu amefanya hivyo ili tuweze kufanyia kazi mambo ambayo yanahusu uhalifu wa aina hiyo, kuliko kuwa watu wana majonzi halafu sisi tunafanya ni jambo ambalo tunaweza tukajibizana. Hii haiwezi ikajenga jamii yetu, inaweza ikatengeneza uhasama ambao hautalifaa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wengine tukiongelea hawa watu ambao wamekuwa wakitupwa na hawa watu wanaosafirisha watu kwa njia haramu, kuna wengine wana- challenge. Ndugu zangu mnapo-challenge basi muwe na takwimu rasmi. Tumekamata kule watu wakiwa wamebebwa pamoja na mkaa, wame-faint, wakapoteza maisha kule Lituhi na Kitahi, tumekamata watu huku Handeni wakiwa wamechanganywa na cement wame-faint wakapoteza maisha. Tumekamata watu 80 wakiwa wametupwa, actually tumewaokota wakiwa wametupwa kwenye hifadhi kule mpakani mwa Tanga na Bagamoyo. Polisi na Magereza wamelazimika kuwatengenezea uji mwepesi ili wapate fahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu kwa sababu wakichoka wengine wanawatupa ili safari iendelee. Kama wanaweza kutupa watu 80, hivi mpaka watu 80 wa-faint kwa nini huwezi ku-suspect kwamba inawezekana walishatupa wengine ambao walipoteza maisha? Kwa nini sisi tunafurahia sana kujengea taswira nchi yetu kwamba kuna mambo mabaya yanafanyika kuliko kuona na tunabisha ambayo yanaonekana, interest yetu ni ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani haya yote yanayotokea Waheshimiwa Wabunge hatuoni kwamba inaweza ikawa moja ya jambo na tuhamasishe ama tuhimize jambo hili udhibiti ufanyike kwa kiwango kikubwa zaidi kwa sababu unachafua taswira ya nchi yetu, sisi tunatamani yale ambayo yana taswira kwamba yanaweza yakawa yana reason kwamba siyo hayo, tunatamani yale yanayochafua nchi yetu, tunanufaika na nini ikiwa hivyo? Hivi nani ananufaika ama nani anafurahia ikionekana kuna Watanzania wanauawa, Watanzania wauawe ili tunufaike na nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, Waheshimiwa Wabunge ni vema sana na ni afya sana kwa Taifa letu tunapoongelea mambo haya makubwa tuwe na vivid evidence na kama tuna vivid evidence tu-report kwenye chombo kilicho rasmi ili taratibu ziweze kufanyika. Sasa mtu akikataa akasema wale waliookotwa walikuwa ndugu wa hawa watu, tunawaambia basi kama kuna ndugu wanahisi wale walikuwa ndugu zao kila mwili uliookotwa tunachukua DNA ili kama kuna mtu atajitokeza afananishwe na yule mtu aende kwenye DNA ili afananishwe hivyo ndivyo tunavyofanya. Sasa wewe kama watu wanaelekea kuharibika unataka tufanyeje? Tuwahifadhi Ofisini? Tunachukua DNA halafu ndiyo tunawazika hivyo ndivyo duniani kote wanavyofanya ili ikitokea mtu akafanya claim iweze kufananishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, niwaambie tu jambo moja, siyo jambo zuri sana kujadiliana ama kutolea mfano watu ambao wako kwenye majonzi lakini ilishatokea mifano ya watu ambao wametaka kufananisha DNA na jambo hilo likafanyika na vipimo vikaonesha, sasa kwa nini tunang’anga’na tu kutaka kulazimisha yale ambayo kuna Mataifa wangetamani anyway iwe hivyo nasi tunatamani yawe yale, tuna interest gani kwenye hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge kwanza tunapojadili jambo la aina hii twende kwa tahadhari lakini kama tuna mtu ambaye ana taarifa za mambo haya specific issues tusaidiane ili tuweze kuisaidia jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kwa sababu kengele ilishagongwa, lilijitokeza suala la maagizo. Kama kuna mtu ana maelekezo yaliyo tofauti atayafikisha kama Waziri wa Nchi alivyosema, lakini mambo yanayohusu Wizara ya Mambo ya Ndani kama kuna Mbunge hajapata kibali, alitoa taarifa ya kufanya jambo lake hakupata kibali, taratibu zinasema ana-appeal kwa Waziri. Kama kuna jambo linahusu uraia wa mtu yeyote ama jambo lolote linalohusiana na uraia anayetoa uraia ni Waziri. Kama kuna jambo la mtu kuondoshwa nchini anayeondosha watu hao ni Waziri, sasa mnatafuta juu ipi? Juu yenyewe ndiyo hii!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama kuna jambo unakutana nalo ukiona OCD akasema limetoka juu na yuko Wizara ya Mambo ya Ndani, RPC akasema limetoka juu na yuko Wizara ya Mambo ya Ndani wewe tuko wote hapa mara zote, Mbunge mwenzangu na mimi ndiyo niko juu sasa si useme kuna jambo liko hapa. Nimeshafanya mambo ya aina hiyo ambayo yalijitokeza katika maeneo husika nimeshafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja nitoe mfano tu, kuna siku moja Mbunge wa Viti Maalum, Njombe, Diwani wake alikuwa na mkutano pale yeye wakamwambia hatakiwi kuhutubia, Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge anayetambua juu akaniambia Mheshimiwa Waziri, mimi ni Diwani katika Manispaa hii kuna mkutano wa Diwani mwenzangu hapa na niko Mkutanoni nimezuiwa kuongea. Nikawaambia mkutano ule ni wa nani? wa Diwani wa CHADEMA na yule Mbunge ni wa Chama gani? Ni Mbunge wa CHADEMA, kuna jambo lolote la kiusalama hakuna! Nikawaambia basi mwacheni aongee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine lilitokea la misinterpretation mkoa mmoja, Maaskofu waliandaa kongamano lao, wanafanya kongamano lao wameshaweka vyombo pale wameshaweka maturubai, wameshaita wahubiri wao kikatoka kibali wasifanye mikutano, nauliza kwa nini, yule mmojawao pale akaja juu kwangu, nilivyouliza kwa nini mmewazuia, wakasema unajua Mheshimiwa Rais amezuia mikutano, nikawauliza amezuia lini? Kwa hiyo nikawaambia waruhusuni waendelee na mikutano yao. Sasa wewe ukishapata jambo hilo ukatulia tu na huku tuko wote siku zote hapa, unatafuta kutengeneza taswira ya juu yako unayoielewa, huo siyo utaratibu wa Kiserikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twendeni kama tuna hoja tusaidiane, wala msitafute juu wala msitafute taswira, hapa tuliko hapa juu zote ziko hapa, mbona mambo mengine mkiyapata hapa mkitoka kwa Waziri mnaenda juu nyingine iko hapa hapa? Kwa nini tunataka kutengeneza na yenyewe iwe story. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge hoja nyingine mlizosema za ufanyaji wa kazi za Kibunge Wabunge wote ni daraja moja, kazi za kibunge Wabunge mnatakiwa kufanya kazi za Kibunge, tusichanganye taratibu, tufanye kazi za Kibunge kwa taratibu na wala tusitengeneze ajenda ambazo zinatugawanya badala ya kutuunganisha kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii naomba sasa kutoa hoja.