Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na nashukuru. Kwanza naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo, lakini pia niendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie katika Wizara hii, Ofisi ya Rais, (Utumishi) lakini pia Ofisi ya Rais, (TAMISEMI). Kwanza nawapongeza Mheshimiwa Jafo na Mheshimiwa Mkuchika kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na wasaidizi wao, Mheshimiwa Kandege na Mheshimiwa Kakunda, lakini pia Katibu Mkuu Ndugu Iyombe, Mzee Ndumbaro pamoja na watumishi wote kwa kazi nzuri na ngumu ambayo wanaifanya, lakini kwa kuhakikisha kwamba huduma hii ambayo Watanzania wengi wanahitaji na ambapo ndiyo engine nzima ya Serikali, wanafanya vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza niishukuru TAMISEMI kwa niaba ya wananchi wote wa Halmashauri ya Babati kwa fedha tulizopewa kwa ajili ya Kituo cha Afya Ngaiti. Tunashukuru sana, ni kituo ambacho kiko pembezoni na huduma ile itawasaidia watu wengi sana. Tumepata shilingi milioni 400 na kituo kinakaribia kukamilika, pamoja na ahadi ya shilingi milioni 200 kwa ajili ya vifaa, lakini pia fedha za P4R pamoja na ambulance kwa ajili ya Kituo cha Afya Magogo. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Jafo pamoja na timu yako nzima.

Pia tulikuwa na ombi kwamba Kituo cha Afya Magugu pale kinahudumia siyo tu Kata ya Magugu ya watu 30,000, lakini pia Tarafa nzima pamoja na baadhi ya nje ya Tarafa na pale ni highway, ikiwa ni pamoja na baadhi ya watu wa Babati Mjini. Tunaomba iongezewe bajeti kwani kile siyo Kituo cha Afya, kile kimekaribia kufanana na hospitali na idadi ya watu wanaotibiwa pale bajeti ikiongezwa itaweza kutoa huduma bora zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninaiombea Hospitali ya Mrara pale Babati Mji kwa sababu na yenyewe pia inaendelea kuhudumia watu wengi wa Babati Vijijini, lakini pia sasa hivi Mji wa Babati unakua kwa kasi sana na ni highway baada ya kufungua hii barabara kutoka Dodoma kwenda Babati na ile ya Singida. Sasa hivi magari mengi yanapita pale na pindi ajali inapotokea, hospitali ile huwa inazidiwa.

Pia nilikuwa naomba wakati tunapopanga bajeti na baadhi ya miradi, pawe na uwiano kutokana na idadi ya kata na vijiji, kwa sababu kama tunagawa sawa kwa Wilaya zote, unakuta Wilaya kama yangu, Halmashauri yangu ina kata 25, vijiji 102 lakini kilometa za barabara kule ni zaidi ya 1,000 zinazohudumiwa na TARURA lakini mgao wa fedha tunaopata unakuta ni sawa na yule ambaye ana robo ya watu wetu, halafu robo ya kata na vijiji. Kwa hiyo, huo uwiano ninaamini kabisa mkijipanga, mtaenda vizuri. Pia nilikuwa naomba kwamba fedha zile za CDG tulizoahidiwa za maendeleo kwa mwaka 2017/2018 zije mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilikuwa naomba kwenye suala la TARURA naipongeza Serikali kwa kuanzisha chombo hiki baada ya Wabunge wengi kukisemea, lakini kama wenzangu wote walivyounga mkono kwamba tunaomba fedha zile asilimia za mfuko wa barabara badala ya kwenda asilimia 30 kwa 70 kama ilivyo sasa, basi iwe 50 kwa 50 ili TARURA iweze kufanya kazi yake vizuri. Pamoja na hiyo, tuendelee kuipatia TARURA rasilimali watu pamoja na nyenzo nyingine ili kazi yao iende vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye suala la maji, nilikuwa naomba kwamba Wakala wa Maji Vijijini uanzishwe mapema. Mmeahidi kwamba mpaka mwezi wa Saba itakuwa tayari lakini bado naendelea kusisitiza kwamba ile shilingi 50 tuliyoomba kwa kila lita ya mafuta iendelee kuongezewa ili mfuko ule utune ili suala la maji liende vizuri. Vile vile pamoja na hayo yote, Serikali iendelee kufikiria kwamba bado kwenye suala la maji kuna vifaa kwa mfano vya kuchimba visima vya maji. Ile mitambo inapokuja inakuwa na kodi kubwa. Serikali ingeangalia namna ya kufuta kodi kwenye mitambo wakati inaingia, lakini wakati inapofanya kazi iendelee kutozwa kodi ili mitambo iwe mingi na watu wengi, huduma zisogee katika Wilaya zote na Mikoa yote ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye suala la maji, nilikuwa naomba Serikali iendelee kuangalia suala la e-water, mita za maji ambayo inatumia mfumo huu wa kielektroniki.

Babati Vijijini ni eneo la mfano, tayari tuna vijiji vitatu ambapo inaenda vizuri sana na wananchi wote wamezoea kutumia njia hiyo. Tukifanya vizuri naamini kabisa tatizo na changamoto hii ya maji inaweza ikaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni muhimu sana, naomba kwa sababu Ofisi ya Rais ndiyo ina Wizara zote hizi mbili ya Utumishi pamoja na TAMISEMI, mwangalie suala la watendaji, yaani kada ya chini, ngazi ya kijiji na kata, watumishi wote wanaohitajika huko, mhakikishe mnatoa vibali vya kutosha ili watendaji kwa mfano wa vijiji, kada ya afya, wale wa sekta ya kilimo wale wote ambao wanatakiwa ngazi ya kata na vijiji wawe wametosheleza badala ya kujaza huku juu. Kwa sababu tukiwa na Watumishi huku juu, ngazi ya Wilaya na Mkoa na huku Taifa na huko chini hakuna na maendeleo yote yanaenda kufanyika kule, unakuta fedha nyingi tunapoteza kwa sababu OC zinatolewa za kutosha, lakini kule chini hakuna mtu wa ku- monitor.

Kwa hiyo, tungejaza huko chini ambapo huduma ndiyo inakotolewa na mishahara yao ni midogo. Mtu mmoja huku juu ukimwajiri, anaweza kuajiri watu wanne kule chini. Kwa hiyo, mwajiri huko chini wa kutosha halafu huku juu watu wafanye kazi kwa ufanisi zaidi. Lingine ambalo nilikuwa naomba ni suala la kukaimu. Suala hili tungejitahidi pawe na kiwango maalum, kama ni miezi mitatu, isizidi hapo. Baada ya hapo mtu awe amethibitishwa ili ajiamini afanye kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuangalia performance. Siku hizi suala la mtu anavyo-perform na utendaji wake, haiendani na shughuli ambazo tunazifanya. Kwa hiyo, naomba tuendelee kuangalia katika sekta nzima ya utumishi katika performance ya watumishi ili kutokana na hiyo basi, wawe wanapandishwa madaraja, lakini pia wawe wanalipwa kutokana na performance ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la posho za Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji na Mtaa. Najua Serikali haina uwezo wa kuwalipa, kwa nini tusiwe na mfumo
ambapo Madiwani wakikaa huko kwenye vijiji, wakifanya kazi nzuri wakaongeza mapato zaidi kutokana na mapato ya ndani, basi waweze kupatiwa posho zao, posho ziongezeke. Utaona mtu kwa sababu ya incentive atakuwa anafanya kazi kubwa zaidi na wataongeza mapato ya Halmashauri zetu. Kwa hiyo, nilikuwa naomba suala hilo pia tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ilikuwa ni suala la Sheria hii ya Manunuzi. Tumefanya vizuri sana, niwapongeze hasa TAMISEMI, mmesimamia vizuri suala la force account kwenye sekta ya afya na elimu, imeenda vizuri. Ninaomba hiyo pia mwendele kutumia kwenye maji na pia kwenye TARURA.