Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nishiriki katika mjadala wa hotuba hizi za Mawaziri wawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza sana kwanza kumpongeza Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Selemani Jafo na Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Kakunda na Kandege kwa kazi kubwa sana wanayoifanya. Sifa kubwa waliyonayo Mheshimiwa Selemani Jafo na Mzee George Mkuchika, ni kwamba ninyi ni wasikivu sana kwa Waheshimiwa Wabunge. Wanawasikiliza lakini pia ni wafuatiliaji wazuri katika shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza pia Watendaji wanaofanya nao kazi Mhandisi Iyombe, Naibu Makatibu Wakuu wanawasaidia, lakini pia na Ndugu Seif ambaye ndiye mteule katika kusimamia TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa ku-declare interest kwamba nimekuwa sasa Mwakilishi wa wananchi kwa miaka 22. Katika miaka 22 hii nimekuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa kwa miaka mitano, nimekuwa Diwani kwa miaka kumi, Nimekuwa Meya kwa miaka mitano na sasa ni Mbunge kwa miaka saba. Kwa hiyo nimekuwa TAMISEMI kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwenye kada ya Wenyekiti wa Serikali za Mitaa na Vijiji na Madiwani. Naishauri Wizara kwamba msingi wa Serikali ni kuanzia kwenye ngazi za vijiji na mitaa, lakini uboreshaji wa maeneo haya umekuwa siyo kwa kasi kubwa. Nashauri kwamba posho za Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa ni muhimu sana, kwa sababu viongozi hawa wamekuwa wakifanya kazi kwa masaa 24 na ndiyo viongozi wanaokaa na jamii. Maeneo mengine ambako Maafisa Watendaji wa Vijiji ama Mitaa hawapo wao ndio walinzi wa amani, kwahiyo ni muhimu sana tukazingatia kuhakikisha na maeneo ya hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye maeneo ya Madiwani. Waheshimiwa Madiwani ndiyo wasimamizi wa mabilioni ya fedha tunayoyapeleka kwenye Halmashauri zetu,
lakini posho wanazozipata zinafanya wakati mwingine Waheshimiwa Madiwani sasa wawe ombaomba hata kwa Watendaji. Kwa hiyo, inakuwa ngumu sana kusimamia kikamilifu katika maeneo hayo, nashauri kwamba ni vizuri sana tukaangalia. Pia suala zima la mafunzo ya viongozi hawa wakichaguliwa wanakaa miaka miwili au mitatu hawajapata semina yoyote. Ni vizuri sana viongozi hawa wakapata semina ili kuhakikisha watende kazi yao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la pili napenda kuchangia ni sekta ya afya. Waziri Mheshimiwa Jafo na Watendaji wake na Wasaidizi wako nadhani wameandika na wanaendelea kuandika historia ya kwamba ni Viongozi waliosimamia kikamilifu katika suala zima la kuhakikisha ujenzi wa vituo vya afya, lakini pia ujenzi wa hospitali 67 za Wilaya, lakini pia upatikanaji wa dawa katika mahospitali yetu na zahanati zetu. Haya ni mambo ambayo wote tunayaona na tumpongeze Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimkushukuru sana Mheshimiwa Jafo na Serikali kwa kuwakumbuka wananchi wa Wilaya ya Masasi hususani Jimbo la Lulindi kwa kupata hospitali ya Wilaya, tunawashukuru sana. Katika hilo nina ombi kwa Mheshimiwa Jafo na Serikali kwamba katika kituo cha afya cha Nagaga ambacho nilikielezea kwamba kilipata tatizo la gari lake la wagonjwa kuungua moto miaka saba iliyopita, hakijapata gari tena, hivyo kupelekea tatizo kubwa sana katika maeneo hayo hasa wagonjwa kuwapeleka mbali katika hospitali ya Wilaya. Naomba sana katika mgao ujao wa magari, hebu tufikirie kupeleka gari katika kituo hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye TARURA. nampongeza Mkurugenzi ama Mtendaji Mkuu wa TARURA Ndugu Seif kwa maandalizi ambayo yanaendelea kwenye TARURA. Hata hivyo, nitoe angalizo tu kwamba kama hawatapata fedha za kutosha itakuwa ni wakala pekee hapa nchini tuliouanzisha ambao hautaleta tija. Tumeshuhudia wakala zote REA, TANROAD zinafanya vizuri, lakini hapa tunahitaji papatikane fedha za kutosha ili waweze kukidhi haja na matarajio ya Watanzania kuhusu eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la watumishi mpaka sasa wameazimwa tu kutoka kwenye Halmashauri wawe pia na watumishi wao ambao wataweza kukidhi kusimamia suala hili. Vile vile kama TARURA hatukuwapa fedha za matengenezo ya kawaida za barabara kwa sababu barabara hizi ambazo TARURA wanakwenda kuzifanyia kazi ni barabara ambazo nyingi ni za changarawe na mvua ikinyesha huwa barabara hizi nyingi hazipitiki. Kwa hiyo kama hawatapata fedha za maintenance maana yake barabara nyingi hapa nchini hazitaweza kupitika hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nilizungumzie ni eneo la migogoro na kero mbalimbali za wananchi kwenye maeneo yetu. Uzoefu wangu mdogo ndani ya TAMISEMI unaonesha kwamba baadhi ya Halmashauri zetu Watendaji hawafuatilii kero za wananchi na matokeo yake sasa hivi Waheshimiwa Mawaziri wakienda kutembelea, Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Makamu wa Rais ni mabango chungu mzima yanayoonesha matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeomba sana Mheshimiwa Jafo aimarishe kitengo cha ufuatiliaji wa kero za wananchi ili zipungue hata yeye anapokwenda kule asianze kukumbana na mabango kwa sababu huo ni upungufu unaoonesha kwamba watu hawajawajibika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ambalo nataka kuchangia ni juu ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Uzoefu unaonesha kwamba liko tatizo kweli la kucheleweshwa fedha na Serikali imejitahidi kwamba wamefikisha asilimia hizo 49,asilimia 50, lakini tukumbuke tu kwamba bado mwaka wa fedha haujausha bado tuna miezi mitatu, tuiombe Wizara ya Fedha ikamilishe ule upungufu wa fedha ambazo zilikuwa hazijaenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuchelewa pia kwa miradi kunatokana na baadhi ya Watendaji kutoharakisha michakato ya kupelekea uanzishaji wa miradi. Kwa mfano, suala zima la kutangaza tender, kuhakikisha kwamba Mzabuni anakuwa awarded inachukua muda mrefu sana.