Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. SUSAN A. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii japo fupi. Nitaanza moja kwa moja na TAMISEMI nami kama Mwalimu nitazungumza zaidi masuala ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ungeniuliza kipaumbele namba moja, mbili na namba tatu vyote ningesema elimu, lakini kwa masikitiko makubwa bado Serikali hii haijawekeza ipasavyo kwenye elimu. Ukiangalia takwimu sekta ya elimu mwaka jana bajeti inaisha kwa ujumla wake ilipata trilioni 4.7, lakini trilioni tatu zimeenda TAMISEMI kwenye sekta ya elimu, katika fedha hizo asilimia saba tu ndiyo inakwenda kwenye fedha za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba miundombinu ya elimu ambayo wote tunaipigania including nyumba za Walimu hazijengwi. Hii ndiyo sababu ukiangalia kwenye hii hotuba hawajaeleza upungufu wa nyumba za Walimu ni ngapi, wamesema tu nyumba za Walimu kwa mwaka huu zimejengwa 290.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti ya World Bank inaonesha kwamba tuna upungufu wa nyumba 186,000. Kama tuna upungufu wa nyumba 186,000 na kwa mwaka mmoja wameweza kutengeneza nyumba 290 maana yake tunahitaji miaka 500 kukamilisha kujenga nyumba za walimu hapa nchini. Hili ni jambo la aibu na halipendezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kwa mwaka huu ukiangalia, bajeti ya mwaka huu trilioni sita kwa Wizara hii, only one trillion ndiyo inaenda kwenye maendeleo, maana yake ni kwamba only 27% ndiyo inakwenda kwenye maendeleo, yet tunategemea shule, nyumba za Walimu na vyoo vijengwe na kadhalika. Hatuwezi kuwa na elimu bora kama fedha haziendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanazungumzia suala la eti kumekuwa na ufaulu zaidi, nataka Serikali ituambie huo ufaulu unapatikanaje wakati Walimu 70% hawako motivated, huo ufaulu unaongezekaje wakati hakuna chochote kilichorekebishwa katika elimu. Naomba Serikali iangalie ni jinsi gani fedha za maendeleo zitakuwa angalau zinalingana na fedha za maendeleo katika Wizara hii inayo- deal na elimu na afya ili watu wetu wasiendelee kufa kwenye vituo vya afya na ili wanafunzi wetu waweze kusoma in a comfortable way. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala zima la Meya. Tunajua kwamba Mameya wote wanatakiwa wachaguliwe na Madiwani ambao wamechaguliwa. Leo Meya wa Manispaa ya Dodoma ameteuliwa na Waziri lakini ndiyo Meya wa Dodoma. Hivi kama tunatunga Sheria yetu ya Serikali za Mitaa, Kifungu Namba 20 kinaelekeza wazi Meya anapatikanaje, lakini inashangaza kuona kwamba mtu anayeteuliwa ndiyo anakuwa Meya wa Manispaa ya Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua ni kwa nini na hapo Naibu Waziri wa Wizara ya Jenista ni Diwani pale, sasa tunashangaa kwa nini tuna sheria zetu lakini tunazipuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuzungumzia suala la Walimu wanaoondolewa kwenye shule za sekondari kwenda shule za msingi. Nakubaliana na wazo lakini ni kwa kiasi gani Walimu hawa watapewa mafunzo ili waendane na hali halisi ya kule wanakoenda kufundisha. Haiwezekani Mwalimu aliyekuwa anafundisha kidato cha tano au cha kidato cha nne anapelekwa kwenda kufundisha darasa la kwanza au darasa la pili, ni lazima wawe na mafunzo vilevile tunajua hawa wote hawajapewa fedha za kwenda kule wanakopelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimsikia Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Selemani Jafo akizungumza, naomba kujua hawa Walimu watawaondolea adha hii lini wapate fedha ili waweze kufanya kazi zao. Kwa taarifa nilizonazo Walimu karibu wote waliohamishiwa huko hawaendi na kama wanaenda basi wanaenda siku moja moja, kwa sababu maeneo waliyopo ni mbali na kule ambako wanatoka. Hivyo, naomba hilo pia lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie kidogo japo limeshazungumzwa, kuhusu suala la Tunduma. Naomba sana Mheshimiwa Waziri alichukue kama special case kwa sababu haiwezekani Baraza la Madiwani ambao ndiyo wanapanga maendeleo tangu mwezi wa Agosti mpaka leo hawajakaa, limezungumzwa lakini naomba kusema kwamba sauti ya wengi ni sauti ya Mungu na Mheshimiwa Jafo najua yeye ni msikivu, naomba jambo hili alifanyie kazi haraka iwezekanavyo ili Madiwani wetu waweze kufanya kazi za maendeleo kama ambavyo miongozo yao inavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni suala la elimu ya msingi. Ni kweli wamesema kwamba asilimia 99 ya shule zetu za Serikali zina elimu ya awali, pamoja na uwepo wa shule ya awali Mheshimiwa Jafo hebu atuambie hizi shule… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)