Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili nami nichangie. Kwanza, namshukuru Mungu kwa kunipa nafasi lakini pia nawashukuru wapiga kura wangu wa Wilaya ya Urambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwapongeza Mawaziri Mheshimiwa Jafo na Mheshimiwa Mkuchika na Naibu wao; Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Kandege na Makatibu Wakuu; Mhandisi Iyombe na Dkt. Ndumbaro na Naibu wao; Dkt. Chaula na Ndugu Nzunda pamoja na watendaji wote wa taasisi za TASAF, MKURABITA na Mfuko wa Rais, kwa kweli wanafanya kazi nzuri. Mungu awasaidie na naomba Serikali iwaongezee fedha waweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona ni muhimu kwangu kwa niaba ya wananchi wa Urambo kuishukuru Serikali kwa kutupa ambulance, ahsante sana itatusaidia kukimbiza wagonjwa pale inapobidi. Pia nashukuru kwa kupewa wafanyakazi kumi na nne na kutembelewa na Waheshimiwa Mawaziri, ahsanteni sana kwa kufika kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru Serikali kwa kupewa milioni 400 ambayo inasaidia kumalizia Kituo cha Afya cha Usoke ambacho kilikuwa ni kiporo cha mradi wa ADB. Wakati huo huo, niiombe Serikali yetu sikivu itusaidie kumalizia theatre ambayo pia ni kiporo cha mradi wa ADB, iliyoko katika Wilaya ya Urambo kwani itakuwa na manufaa sana kwa sababu bado tunasaidia wenzetu wa Kaliua na maeneo mengine kutoka Wilaya ya Uyui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani za kupewa milioni 400 ya kusaidia kituo cha afya bado tuna uhaba mkubwa sana wa vituo vya afya. Tunaiomba Serikali yetu itusaidie kupata Kituo kingine cha Afya cha Vumilia ambacho kipo katika barabara ya kwenda Sikonge ili ajali zinapotokea kisaidie. Pia kituo hiki kitasaidia ajali zinazotokea kati ya Kigoma na Urambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo kingine cha Afya cha Usoke nacho tunaomba kisaidiwe. Kwa hiyo, tunaomba msaada wa kupata vituo vya afya cha Vumilia na Kata ya Usoke kwa sababu mpaka sasa tuna kituo kimoja tu cha afya kati ya kata 18. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuiomba Serikali iangalie sana suala la wafanyakazi wa afya. Sisi Urambo peke yetu tuna uhaba wa wafanyakazi zaidi ya 300, lakini ili angalau kupooza makali tunaomba wafanyakazi 75. Tutashukuru sana tukipata haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali iajiri na hasa hasa Wakunga. Tunapozungumzia kupunguza vifo vya mama na mtoto tunaangalia sana uwepo wa Wakunga. Kwetu sisi kuna zahanati ambazo zina mfanyakazi mmoja tu, sasa anapougua au anapokwenda kwenye semina mama mjamzito anapokuja pale inakuwa ni vigumu sana kupata huduma. Tunaomba Serikali iajiri wafanyakazi na kwa kuanzia waanzie Wakunga ambao tunaamini kabisa watatusaidia kupunguza vifo vya akinamama na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna uhaba mkubwa sana pia kwa upande wa elimu. Orodha ya mahitaji yetu sisi kama Urambo tulishapeleka TAMISEMI. Kwa hiyo, tunaomba Walimu wa shule za sekondari na shule za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la kuunda TSC ilikuwa ni kuangalia jinsi gani tunaweza kuwapunguzia Walimu adha katika kupata haki zao. Ombi langu kwa Serikali ifanye tathmini, kweli TSC iliyopo inakidhi mahitaji iliyoundiwa? Kwa sababu mpaka sasa hivi matatizo bado ni mengi tu, Mwalimu anapodai haki zake au anapotaka kuhama na kadhalika. Tunaiomba Serikali ifanye tathmini, je, TSC kweli inafanya kazi zake ilizokusudiwa? Naamini Serikali inaweza kuchukua hatua za kurekebisha ili Walimu waweze kupata huduma kwa wakati hasa hasa mahitaji ya kupanda daraja na wakati huo huo kurekebishiwa mishahara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwa upande wa elimu lakini hasa kwa kugusa mtoto wa kike. Naomba niseme wazi kabisa mimi nimo katika Kamati ya Utawala na TAMISEMI na naiunga mkono kabisa taarifa ya Kamati yangu kwenye ukurasa wa 37 ambapo inasema, naomba kwa ruhusa yako nisome, kutokana na kushindwa kumudu gharama za taulo za kike, wanafunzi wa kike wamekuwa wakikumbwa na athari za kushindwa kuhudhuria masomo kwa siku kati ya tatu mpaka tano kwa mwezi na hivyo kuathiri mahudhurio yao na wakati mwingine kuacha shule kabisa hasa wanaotoka katika familia duni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili ni muhimu sana. Naiomba kwa heshima na taadhima Serikali kuliangalia suala hili kwa undani na kuona jinsi gani ambavyo itaweza kumsaidia mtoto wa kike. Suala hili kama nilivyosema tunaiomba Serikali iliangalie kwa makini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tuna tatizo moja sugu kwenye Kamati yetu tulilitilia sana mkazo na tulimwambia Mheshimiwa Waziri husika wa TAMISEMI kuangalia suala la vyoo. Suala la vyoo pia limekuwa likisababisha wakati mwingine watoto wa kike kushindwa kuvitumia kutokana na kukosa milango na vilevile na Walimu kuchangia vyoo na watoto yaani wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali kwa heshima kabisa kuangalia jinsi gani wanaweza kuweka mkakati ambao utaondoa kabisa tatizo la vyoo na wakati huo kuiomba Wizara ya Elimu kwa kupitia taarifa hii hii, shule zisisajiliwe kabla ya kujenga vyoo. Vyoo vianze halafu ndiyo majengo mengine yakaguliwe. Nadhani jambo hili linahitaji mkakati wa karibu kabisa ili iweze kusaidia kuondoa tatizo la vyoo visitajwe kabisa tena kwa sababu ni jambo la kusikitisha kwamba tunazungumzia choo katika karne ya 21 kwa sababu tunaamini kabisa mtu ni afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeweza nikaongea mengi zaidi ya hayo lakini hasa hasa ni kuomba kwa heshima kabisa vituo vya afya kama nilivyosema Vumilia na Usoke;
kuomba theatre yetu Urambo ambayo ni kiporo cha ADB imaliziwe, lakini wakati huo huo kuiomba kabisa Serikali yetu kwa heshima na taadhima kabisa kuangalia upatikanaji wa wafanyakazi wa Idara ya Afya na hususan Wakunga ambao watasaidia kuondoa vifo vya akinamama au kupunguza kwani hali ilivyo sio nzuri tunahitaji huduma haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, nikiamini Serikali yetu nzuri itasikia haya niliyoyasema. Ahsante.