Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze mchango wangu kwa kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote na Makatibu wa Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri inayofanywa na Wizara hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuchangia sasa Ofisi ya Rais, TAMISMI kama ifuatavyo:

Nianze na sekta ya elimu; sekta hii kwa ujumla wake ina changamoto nyingi sana, elimu yetu haijawahi kuandaa wahitimu kuweza kujitegemea hata wale wa elimu ya juu. Changamoto kubwa ni mabadiliko ya mitaala ya mara kwa mara ambako hakuendani na mafunzo kwa Walimu juu ya hiyo mitaala mipya na hata vitabu wakiandaa havitoshi hasa kwa shule za msingi. Vilevile hata miongozo inayotolewa kila kukicha kunachangia kuwavuruga Walimu mashuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya uhaba wa Walimu ni kubwa sana nchini, mfano, katika Halmashauri ya Liwale kuna shule nyingi zina Walimu chini ya watano. Shule ya Ndapata, Mtungunyu, Nambinda shule hizi zina Walimu watatu tu kila moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu la kujenga miundombinu ya shule limeachwa kwenye Halmashauri jambo hili limefanya shule nyingi kuwa na miundombinu mibovu sana kwani Halmashauri nyingi zinashindwa kumudu jukumu hili hasa baada ya vyanzo vingi vya mapato vya Halmashauri kuchukuliwa na Serikali Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya; changamoto zilizopo kwenye sekta ya afya zinafanana kwa kiasi kikubwa na zile za elimu. Uhaba wa watumishi na miundombinu mibovu ya zahanati, vituo vya afya na hospitali za Wilaya hali ni mbaya sana hasa kwenye zahanati na hospitali za Wilaya. Mfano, Halmashauri ya Liwale yenye Kata 20, Vijiji 27 kuna Zahanati 34 tu ambazo zote zinahudumiwa na Manesi Wasaidizi, hazina matabibu wala Madaktari Bingwa wala mmoja na mpiga picha wa x-ray.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, shida ya gari la wagonjwa kwenye hospitali ya Liwale ni kubwa sana. Mapato ya Halmashauri kununua gari ni jambo lisilowezekana kwenye Halmashauri ambayo hata zahanati zilizopo ni chache na miundombinu yake ni duni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri licha ya kupokwa vyanzo vya mapato, lakini Serikali imekuwa bado ikiwapa mzigo mkubwa wa kuhudumia jamii Wakurugenzi wa Halmashauri hizo. Serikali imekuwa haitoi fedha za maendeleo kwa kisingizio cha Halmashauri kutumia mapato ya ndani wakati ikijua kwamba kwenyewe haipeleki fedha za matumizi ya kawaida yaani OC. Jambo hili linafanya halmashauri kushindwa kupanga mapato yake ya ndani kwa miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali imekuwa haipeleki fedha za miradi ya maendeleo hadi mradi huo uanze kutekelezwa kwa ngazi ya Halmashauri. Jambo hili limekuwa likiongeza umaskini kwenye Halmashauri nyingi hasa zile zisizokuwa na mapato ya kutosha kugharamia miradi hiyo, hivyo Halmashauri kuendelea kubaki nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimamo huu wa Serikali hauwezi kuleta mgawanyo ulio sawa kwa nchi nzima. Kuna Halmashauri itakayopata fedha nyingi na zingine zikawa hazipati fedha kabisa. Mfano, Halmashauri ya Wilaya ya Liwale haina jengo la hospitali ya Wilaya, jengo la Polisi Wilaya. Miradi hii yote ni miradi ya fedha nyingi na ni miradi muhimu. Kama Halmashauri tukishindwa kuanzisha miradi hii maana yake Serikali haiko tayari kugharamia miradi hii. jambo hili ni vyema Serikali mkaliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo; pamoja na kuwa zaidi ya asilimia 70 ya watu wetu ni wakulima, lakini sekta hii haijapata msukumo wa kweli. Wakulima wetu bado wanaishi maisha duni sana licha ya kutumia zana duni kwenye kilimo bado hata hayo mazao wanayopata hawana uhakika wa masoko.

Matamko mengi ya Serikali juu ya kilimo yanachangia kwa kiasi kikubwa kudumza kilimo. Mfano kuzuia watu kusafirisha mazao kufuata soko ni unyanyasaji mkubwa. Ni nani mwenye jukumu la kutunza chakula cha akiba kwa nchi, ni mkulima au Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ucheleweshaji wa pembejeo za kilimo ni kikwazo kingine cha kumkwamua mkulima. Mfano, hadi leo pembejeo za korosho hazijulikani zitaingia lini nchini wakati mwezi Mei ndiyo mwezi wa kuanza kuweka dawa kwenye mikorosho na hata bei za pembejeo hizo hadi leo hazijulikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa Maafisa Ugani pamoja na vyombo vya usafiri kwa hawa wachache waliopo kunachangia kwa kiasi kikubwa watu wetu kulima bila kuzingatia kilimo cha kisasa kwani wananchi wengi hawafikiwi na watalaam hao. Hivyo, ni vyema Serikali ikahakikisha inakuwa na Maafisa ugani wa kutosha na wawe na vitendea kazi. Vilevile sekta ya kilimo cha umwagiliaji ndiyo kimetupwa kabisa. Miradi mingi ya umwagiliaji nchi nzima imekuwa haikamiliki na fedha zake kuliwa kama hazina mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuhudumu kwenye Wizara hii, Mungu ampe umri mrefu ili aweze kuendelea na jukumu hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utumishi na watumishi hapa nchini ni hali mbaya sana. Hali ya watumishi nchini kwenye kada mbalimbali ni mbaya. Kilio cha uhaba wa watumishi nchini ni kikubwa sana na hata hao wachache tulionao hali na mazingira yao ya kazi ni mbaya sana kwani walio wengi malipo yao hayalingani na kazi zao. Walio wengi wanafanya kazi kwa sababu tu hawana namna ya kuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linapunguza ufanisi na ari ya kazi. Ikumbukwe kwamba baada ya punguzo kubwa la wafanyakazi hapajatokea mkakati maalum wa kuziba pengo hilo. Mishahara ya watumishi wengi, hasa wa kada za chini bado ni midogo sana na ni miaka miwili kama si mitatu haijafanyiwa mapitio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi wengi hasa wa sekta ya elimu na afya wanafanya kazi chini ya kiwango kwa kuwa kazi zao hazithaminiwi, hivyo walio wengi hufanya migomo baridi, jambo ambalo halina tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile mipaka ya kazi sasa haiko wazi kwa wakuu wengi wa mahali pa kazi, wanafanya kazi kwa matamko zaidi kuliko weledi wa kazi. Jambo hili linachagizwa zaidi na kutokuwapa mafunzo au semina kwa watumishi wengi wa umma. Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri walio wengi hawajui mipaka ya kazi zao ndiyo maana kuna migongano mingi kazini. Ubabe ni mwingi kuliko weledi, watumishi wanajazwa hofu badala ya kutiwa moyo na ari ya kazi, kazi za kitaaluma zinafanywa kwa matamko badala ya kitaaluma, hivyo kuondoa ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko kwenye sekta binafsi ndiko kumeoza kabisa. Wafanyakazi huko hawana taasisi yoyote inayowasimamia, tumeacha watu wa chini wapambane na matajiri wao. Katika mazingira haya ya uhaba wa ajira tunatarajia nini kitatokea kama si watu wetu kunyanyasika na matajiri tunaowaita wawekezaji? Hali ya ajira kwenye sekta hii ni mbaya sana, hakuna anayesimamia mikataba ya ajira zao wala hali bora ya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utawala bora; dhana ya utawala bora ni pana sana na ili itekelezwe ipasavyo kuna haja watu waliopewa dhamana ya kusimamia dhana ya utawala bora waelewe maana ya utawala bora na utawala wa sheria kwani mahali ambapo sheria hazifuatwi hakuna utawala bora. Utawala wa sheria ni dhana nyingine inayowataka viongozi au watawala kufuata sheria kwa mujibu wa Katiba wakijua kuwa roho ya amani ni haki na haki ni kufuata sheria/Katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali ya sasa dhana ya utawala bora imeanza kutokomea kwani watoaji haki wameanza kukiuka dhana ya utawala bora. Sasa hivi tumeanza kujenga Taifa la watu waoga na si watii wa sheria kwani kuna tofauti kubwa kati ya kutii sheria na woga. Mtii wa sheria siku zote atabaki na utii wake, lakini mtu mwoga siku akibadilika akaacha woga basi hapo amani huwa mashakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, roho ya amani ni haki na wala haitakuwa woga, kulea watu waoga ni kulea bomu katika jamii. Ni vizuri Serikali ikaanza sasa kuwafanya watu watii sheria badala ya kuwajengea woga ambao ipo siku utakwisha. Vitendo vinavyoendelea nchini sasa havina mwelekeo mzuri, vitendo vya watu kutekwa, kupotea na hadi kuuawa ni hatari sana, hasa pale Serikali inapokaa kimya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matamko ya Viongozi. Uongozi wa Awamu ya Tano umekuja na namna mpya ya kuongoza. Kumekuwa na matamko mengi kutoka kwa viongozi na mara nyingi yamekuwa yakipingana kutoka ngazi moja hadi nyingine. Vile vile kuna viongozi ambao hawafanyi kazi wakisubiri maagizo kwani wakifanya bila maagizo wanaweza wakaondolewa kwenye nafasi zao hata pale anapofanya jambo lililo chini ya mamlaka yake. Watendaji wako ofisini wakisubiri maagizo tu. Uwajibikaji wa pamoja nao umeanza kutoweka, viongozi walio wengi wanaogopa dhana ya uwajibikaji wa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haki na amani; watu wa kwanza watakaowajibika kwa Mungu siku amani ya nchi yetu ikitoweka ni wale wanaosimamia utoaji haki ambao ni pamoja na polisi, mahakama, Msajili wa Vyama vya Siasa, Tume ya Uchaguzi na Usalama wa Taifa. Taasisi hizi ni muhimu sana wakatenda haki na jamii wakaona haki ikitendeka na haki hiyo lazima iende na wajibu. Hakuna amani bila haki na hakuna haki bila wajibu, naishauri Serikali kusimamia haki ili kulinda amani yetu.