Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa, Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu katika hoja ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uzima na afya na kukutana siku hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee na mchango wangu kuhusu Chuo chetu Kikuu cha Dodoma kwa kuongeza udahili wa wanafunzi kujiunga katika Chuo cha Umma baada ya kuongeza ajira ya Wahadhiri na vifaa ili waweze kujaza chuo chetu na kufikia lengo la kuwa na wanafunzi 45,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kutoa ushauri wangu kwa Serikali kutoa kipaumbele cha kwanza katika udahili wa wanafunzi na kutoa mkopo kwa wanafunzi wa vyuo vyetu vya umma. Kwa sababu hivi vyuo vilijengwa kwa fedha za umma kupitia kodi na mikopo iliyochukuliwa italipwa na umma huu wa Tanzania na kwa maana hiyo ni vizuri kujaza vyuo hivi kwanza ukizingatia tulishafanya uwekezaji mkubwa katika vyuo hivi vya umma na tunafanya mrejesho na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka pia kutoa ushauri wangu katika usimamizi wa ubora wa elimu katika vyuo vikuu vyetu hasa ubora wa mitihani na ufundishaji kwa ujumla. Utakuta Mhadhiri anatakiwa kufundisha topic 12 kwa muda wa wiki14, lakini utakuta Mwalimu amefundisha topic mbili au tatu tu na kutoa mtihani katika topic hizo ili kuficha udhaifu wake wa kutokuwepo chuoni na kutofundisha kwa muda mrefu. Pia baadhi ya Wahadhiri hawahudhurii madarasani kwa muda mrefu na kuja ama mwisho wa muda wa muhula au mwanzo wa muhula na kufundisha vipindi na mada zilizotakiwa kufundishwa kwa wiki 14, badala yake anafundisha kwa wiki moja au mbili topic zote kwa muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tajwa hapo juu zinaathiri kwa kiasi kikubwa ubora wa elimu yetu kwa ngazi ya vyuo vikuu kwa sababu wanafunzi na Wahadhiri wanajali zaidi kupata cheti chenye alama za juu ili kupata ajira kwa urahisi sababu katika soko la ajira mahitaji ya soko yanaelekezwa katika wahitimu waliopata alama za juu badala ya dhamira, uelewa, utaalam, ufahamu na mahitaji. Ili kukabiliana na tatizo la kushuka kwa ubora wa elimu katika vyuo vyetu nina ushauri ufuatao:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuandaa chombo cha udhibiti ubora wa elimu katika ngazi ya Vyuo Vikuu ili kukagua ubora wa elimu katika upande wa Walimu, ufundishaji, mitaala na ubora wa mitihani inayotungwa kama ina tija inakidhi mahitaji katika soko la ajira nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kuja na mpango mkakati wa kubadilisha mitaala ya elimu ya juu na chini ili ilingane na mahitaji ya sasa katika soko la ajira hasa kuwaandaa wahitimu kujiajiri wenyewe hasa mkazo kuwekwa katika elimu ya ufundi, ufundi stadi, kilimo, sayansi na elimu ya kiteknolojia na computer.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kuunda Tume ya Raisi ya Elimu kama ile ya Makwetta ili kufanya tathmini ya elimu yetu hasa katika ubora wake kuanzia ngazi ya elimu ya awali mpaka Chuo Kikuu ili kubaini upungufu,,fursa na mahitaji na kuja na mapendekezo ya kuboresha ubora wa elimu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho na sio kama kwa umuhimu nirudi tena kusema changamoto zinazowakabili wananchi wenzangu wa Morogoro Kusini Mashariki ninaowawakilisha hapa Bungeni na kuiomba Serikali kuyapatia ufumbuzi wake. Naomba Serikali kutupatia magari mawili ya wagonjwa kupitia Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais katika Kituo cha Afya Mkuyuni kinachofanyiwa ukarabati na Kituo cha Afya Kinole chenye idadi kubwa ya watu. Kwa kutoa huduma kwenye kata tatu za Kinole, Tegetelo na Ludewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, magari hayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais ya mwaka 2010 kwa gari la Mkuyuni na mwaka 2014 kwa gari la Kinole na mbele ya aliyekuwa Waziri wa Ujenzi na wakati huo ambaye kwa sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dokta John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali kutupatia magari haya ili kuokoa vifo vya wagonjwa na hasa watoto na kwa mama. Pia naomba Serikali kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini ili kufungua mawasiliano ya barabara zifuatazo:-

 Mkuyuni – Ludewa – Mgozo;

 Mkuyuni – Kibuko – Tununguo

 Mkuyuni – Luholole – Kibuko;

 Mwalazi – Kibuko – Luholole;

 Seregefe B - Kuaba;

 Seregefe A – Lubumi – Mafulu;

 Mkulazi – Mvuha;

 Mbarangwe - Kisanga Standi;

 Kwoka – Mfumbwe - Kibwaya;

 Kizinga - Kimbwala – Kwika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.