Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana kwa ajili maisha na uhai wa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, nianze na eneo la uhifadhi wa mazingira na utunzaji wa vyanzo vya maji. Yapo mambo ambayo tunaweza kusema yanahitaji fedha nyingi lakini yako mambo ambayo pengine hayahitaji fedha kiasi hicho ni suala tu la umakini na utekelezaji wa sera na taratibu ambazo tumejiwekea.

Mheshimiwa Spika, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa alifanya ziara ya kikazi katika Bonde la Eyasi mwishoni mwa mwaka 2016. Wananchi walieleza kero zao nyingi ikiwemo uharibifu wa chanzo cha maji cha Mto Qangded. Baada ya Waziri Mkuu kuwasikiliza wananchi hao na kuona ukubwa wa jambo hilo alitoa maagizo mawili yafutayo; jambo la kwanza; eneo la chanzo cha Mto Qangded lihifadhiwe kwa mita zisizopungua 500 kila upande. Jambo la pili, mashine zote za ku-pump maji zilizoko kwenye
mto na kwenye chanzo ziondolewe jioni ya siku hiyo na zisirudi kwenye chanzo hicho. Jambo la kushangaza hadi leo mwaka na nusu maagizo ya Waziri Mkuu bado hayajatekelezwa. Naomba Mheshimiwa Waziri wa Maji unisikilize kwa sababu naongea na wewe, naona unaongea pembeni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni jambo kidogo la kusikitisha kama Kiongozi Mkuu wa Pili wa nchi anatoa maagizo na maelekezo halafu mwaka na nusu unapita hakuna jambo ambalo limefanyika. Mbaya zaidi hawa watu wenye kiburi, wenye jeuri wanaoharibu vyanzo hivyo sasa wamevuta na umeme wa gridi kuupeleka kwenye vyanzo vya maji ili wa-pump vizuri maji hayo na wale walioko chini hawapati maji, tunakwenda wapi? Ni jambo ambalo haliingii kwenye akili ya kawaida huku tunasema hatuna fedha za kufanya miradi lakini hata hili la kusimamia sheria tumeshindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri juzi uliulizwa maswali mawili ya nyongeza hapa na Mheshimiwa Paresso na dada yangu Mheshimiwa Catherine kuhusu chanzo hiki hiki na ukasimama, ukalidanganya Bunge kwamba chanzo kile kimepimwa. Mimi naomba nikuhakikishie chanzo kile bado hakijapimwa. Wataalam wako wa Bonde la Kati walikwenda Bonde la Eyasi, wamekaa kwa siku moja lakini wakakwamishwa na viongozi walioko chini yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni suala la athari za mafuriko. Ukiongelea chanzo cha Qangded, Bonde la Eyasi unaongea juu ya uhai wa wananchi wasiopungua 70,000. Chanzo kile kikipotea wanachi hao maisha yao yako hatarini. Juzi wananchi wa Mang’ola baada ya chanzo kile kuharibika wamejichangisha zaidi ya shilingi milioni 21 na Halmashauri ya Karatu ikaweka shilingi milioni 35 ili kunusuru chanzo hicho. Nikuombe sasa na wewe uweke mkono kwa sababu wewe uko kwenye chungu kikubwa ili kuhakikisha chanzo hicho kinaendelea kutoa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri ulipokuwa Mang’ola kabla kidogo ya ziara ya Waziri Mkuu ulitoa ahadi ya kuboresha miundombinu katika eneo hilo. Nikukumbushe tu kwamba bado wananchi wanakumbushia utekeleze ahadi yako ya kuboresha baadhi ya miundombinu ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, nimesoma katika kitabu cha Waziri, mwaka 1962, kiwango cha maji kwa mtu katika nchi hii ilikuwa ni mita za ujazo 7,862 lakini mwaka huu ni mita 1,800 za ujazo kwa mtu kwa mwaka. Tunakwenda chini kwa kasi kubwa sana. Nadhani kama nchi tuna kila sababu ya kuchukua hatua. Kama miaka 50 kumekuwa na tofauti kubwa kiasi hicho, miaka 50 inayokuja nadhani tutakwenda chini ya mita 100 za ujazo. Kwa hiyo, mimi nishauri hebu Serikali fanyeni jitihada za makusudi za kuhakikisha vyanzo vya maji nchi hii vinalindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2015/2016 asilimia 28 ya fedha ambazo tulipitisha ndiyo zimekuja, mwaka uliofuata asilimia 25, mwaka huu ambao tunamalizia asilimia 22. Mheshimiwa Waziri una jeuri gani kuja mbele yetu leo na mabilioni ya hela wakati siku zilizopita umekuwa unapata hizo asilimia chache? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia mimi simuoni Waziri kama anasikitika, simuoni Waziri kama analia, Waziri unataka tukusaidiaje? Hebu lia tusikie halafu na sisi tukusaidie. Mimi naona wewe unaridhika tu na hicho unachopewa. Pambana kama wenzio upate hela za kutosha, maana yake hapa tutakurushia madongo na mawe ya kila aina lakini mwisho wa siku kama ulikuwa unashuka na ukafika 22, bajeti hii hata 20 haitafika. Kwa hiyo, mimi nadhani ndugu zangu suala la maji halina mbadala, mtu aitaka maji unampa maji. Kwa hiyo, mimi niombe hebu tuweke jitihada za makusudi nchi hii tuhakikishe eneo hili linapewa fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante.