Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ili kusudi na mimi niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii muhimu ya Maji na Umwagiliaji chini ya Mheshimiwa Waziri Kamwelwe.

Mheshimiwa Spika, maji ni uhai. Kwa hakika ndiyo maana Serikali yetu imekuja na mpango mzuri na miradi mingi mikubwa imeorodheshwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, Wilaya yetu ya Mbogwe ni miongoni mwa Wilaya ambazo tulifanikiwa kunufaika na miradi ya World Bank tukapata maji katika eneo la Nyerere, Mji wa Masumbwe, Shenda, Bulugala Kata ya Nyasato na Lulembela, Kata ya Lulembela. Miradi hii inafanya kazi vizuri, naipongeza Serikali. Pia tumeleta makadirio ya maombi ya fedha kwa ajili ufungaji wa umeme katika hivi vyanzo vya maji vya visima virefu katika hii miradi minne World Bank.

Mheshimiwa Spika, nataka niiambie tu Serikali kwamba Wilaya yetu ya Mbogwe ilikuwa ni sehemu ya Wilaya ya Kahama ambayo kimsingi ilionekana dhahiri kwenye Serikali kwamba tuna upungufu wa maji ardhini na kwa maana hiyo Serikali ikaamua kuleta maji kutoka Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, nimpongeza Mheshimiwa Waziri Kamwelwe aliwahi kufika Mbogwe. Nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu ombi letu ulilikubali na ukafika na uliojionea hali halisi. Wilaya yetu ya Mbogwe tuna Makao Makuu yetu ambayo yako katika Mji wa Kasosobe na wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri ulifika na ukajionea hali halisi kwamba pale kumefanyika jitihada za kuchimba maji lakini kutokana na upungufu wa maji ardhini visima hivi vimekuwa vikitoa maji machache ambayo yanastahili kwa ajili ya kuweka pump za maji peke yake. Kwa hiyo, niiombe tu Serikali ifikirie uwezekano wa kutupatia maji kutoka Ziwa Victoria kwa sababu Wilaya ya Kahama ipo jirani na kwetu pale, ikiwezekana basi pesa zipatikane za kuweza kutuletea maji hayo ili hatimaye tuwe na uhakika wa maji muda wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maji ni kitu muhimu sana kwa mambo yote, iwe uwekezaji wa viwanda ambao sasa tunafikiria kwamba Tanzania itakwenda kuwa ni Tanzania ya viwanda, viwanda bila maji haiwezekani. Maji yanahitajika pia kwa mifugo na shughuli za kilimo cha umwagiliaji. Kwa maana hiyo, niiombe Serikali iendelee kuweka pesa katika Wizara hii na zitolewe kwa wakati. Pale tunapopitisha bajeti ni vizuri sasa Wizara ya Fedha ikazitoa pesa hizo kwa wakati na miradi ile ambayo imependekezwa itekelezwe kwa mujibu wa bajeti ya mwaka husika.

Mheshimiwa Spika, tunayo pia miradi ambayo imetengewa pesa kwa ajili ya kuchimba visima katika Kata ya Ng’homolwa, Kijiji cha Chakabanga, pia katika Kijiji cha Lugunga Luhala. Vijiji hivi vimefanikiwa kupata maji wamechimba wakapata maji na kwa maana hiyo certificates zimepelekwa kwa Waziri ili kusudi tupatiwe pesa na utandazaji wa mabomba uweze kufanyika. Kwa maana hiyo, naomba Serikali utupatie hizo pesa kwa ajili ya uendelezaji wa visima hivi kwa maeneo ambayo tumefanikiwa kupata lita za ujazo ambazo zinaweza zikafaa kwa ajili ya uanzishaji wa visima vikubwa au visima virefu ili wananchi wetu waweze kupata hii huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, maeneo mengi ya vyanzo vya maji pia yanatakiwa yapewe utaratibu mzuri wa hifadhi ya mazingira. Kwa sababu bila kuwa na mazingira yaliyo safi hakika tunaweza kujikuta tunapata shida zaidi. Ni dhahiri kwamba vyanzo hivi vya maji tunavyokuwa tunavianza na kuvisambaza kwa wananchi, vilevile tutarajie kwamba kutakuwa na maji machafu. Kwa maana hiyo, niombe tu kwamba wakati Serikali inakuja na mipango hii ya maji safi na salama basi tuwe na mipango mahsusi kwa ajili ya treatment ya maji machafu ambayo yanazalishwa kutokana na matumizi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua wazi kwamba maji ndiyo chanzo kikubwa cha maradhi. Kwa maana hiyo, tukiwa na maji ambayo ni salama nina uhakika magonjwa mbalimbali ya kuambukiza ikiwemo kipindupindu na magonjwa mengine ya matumbo yanaweza yakadhibitiwa tukajikuta kwamba hata ile huduma ya dawa hospitalini bajeti yake inaweza ikapungua endapo watu hawaugui magonjwa maambukizi ya kuwadhuru wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, niombe tu Serikali iendelee pia na utaratibu huu wa kuhakikisha kwamba tunapanda miti kwenye vyanzo vya maji. Vyanzo vya maji vikiwa vimepandwa miti naamini kwamba kwa namna ya moja au nyingine tutakuwa tumesaidia kuhakikisha kwamba ukame unadhibitiwa na tutakuwa na uhakika wa kupata mvua za kuaminika. Wakati wote tutajikuta kwamba tumeondokana na ukame ambao unasababisha upungufu wa maji.

Mheshimiwa Spika, kutokana na taarifa ambazo tayari tumeshapeleka Wizarani, ninayo imani kwamba miradi yetu ambayo tumeiomba kwa Serikali itafanyiwa kazi. Kwa maana hiyo, niseme tu kwamba Wanambogwe tunaiunga mkono Serikali na niseme kwamba naunga mkono hoja, ahsante sana.