Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Ardhi na nichukue fursa kumwomba Mwenyezi Mungu amweke Mbunge mwenzetu ambaye ameitwa mbele ya haki, mahali pema peponi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida yangu kubwa ni upande huu huu wa migogoro ya ardhi. Pamoja na kwamba Liwale ardhi tunayo kubwa sana, lakini kutokana na uroho wa baadhi ya taasisi wameamua kutuingiza kwenye migogoro mikubwa sana. Sisi Liwale tuna mgogoro mkubwa sana na Selous. Nilikwenda ofisini kwa Mheshimiwa Waziri, majibu aliyonipa aliniambia kwamba mgogoro huu upo ndani ya Mkoa au Kamishna wa Ardhi, atakaposhindwa ndio atampelekea. Naomba nimwambie kwamba hawezi kushindwa akamletea, akimletea maana yake ni kwamba ameshindwa kazi na akishindwa kazi maana yake hataki ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kinakachofanyika pale, ule mgogoro kwa sasa una miaka zaidi ya kumi, haujatatuliwa, sisi na Selous tunagombana. Mpaka sasa hivi watu wanne wamepoteza maisha, kwenye mgogoro ule kati ya Kijiji cha Kikuyungu pamoja na Selous.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu, vile vile tuna mgogoro wa ardhi sisi pamoja na Wilaya ya Kilwa, sehemu ya Nanjilinji. Huu mgogoro nao ni wa muda mrefu sana na mgogoro huu ndio ulionipeleka mimi kwa Mheshimiwa Waziri na akanipa hayo majibu kwamba Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa akishindwa ataniandikia. Mkuu wa Mkoa hawezi kushindwa akamwandikia, akishindwa maana yake ameshindwa kazi, lakini bado watu wanaendelea kuteseka. Naomba Mheshimiwa Waziri achukue initiative kwenda kutatua huu mgogoro kati yetu pamoja na Kilwa, pamoja na huu mgogoro wa Selous. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niongelee huyu Kamishna wa Ardhi wa Kanda ya Mtwara. Mimi kwa kweli kwenye Halmashauri yangu ya Wilaya ya Liwale, migogoro hii kama kweli huyu Kamishna wa Ardhi wa Kanda ya Mtwara, angekuwa anafanya kazi kwa weledi hii migogoro mingine isingekuwepo. Sio hivyo tu, vile vile hata upatikanaji wa hati pale Mtwara; sisi kwanza tuko mbali sana; kutoka Liwale mpaka Mtwara ni umbali mrefu sana, lakini hata ule ushirikiane wake nao ni mgumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano hawa vijana wa Selous Kijiji cha Kikulyungu, walikuja mpaka hapa Bungeni tukawapeleka mpaka kwa Mheshimiwa Waziri na akaturudisha kwa Kamishna. Kamishna mpaka leo anawazungusha hakuna chochote kinachoendelea na wala hawajui waelekee wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo Kamishna wa Ardhi wa Mtwara aliokasimiwa madaraka mimi naona kwamba yeye badala ya kutatua migogoro analimbikiza migogoro, pengine ni kwa sababu ya kuogopa ajira yake, kwamba akionekana ameshindwa basi ataonekana hajafanya kazi vizuri. Kwa hiyo namwomba kabisa Mheshimiwa Waziri kwa nia njema aje Liwale atutatulie hii migogoro ya ardhi kati ya sisi pamoja na Kilwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwa upande wa watumishi katika Halmashauri yetu. Halmashauri ya Wilaya ya Liwale kuna mtumishi mmoja tu wa ardhi mwenye sifa, waliobaki wengine si watumishi wenye sifa. Matokeo yake sasa kuna tatizo kubwa sana, unapoingia mahali ambako sasa tunataka tupime ardhi kwa matumizi bora ya ardhi tatizo hilo linakuwa kubwa sana kwa sababu uhaba mkubwa sana wa watumishi wa ardhi katika Halmashauri yetu ya Wilaya ya Liwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si watumishi peke yake na vifaa vile vile. Mara nyingi tunatumia vifaa kutoka Halmashauri ya Nachingwea, kwa maana ya kwamba hatuwezi kufanya kazi pale mpaka tutafute wataalam na vifaa kutoka Nachingwea, ndipo tuweze kufanya kazi pale kwenye Halmashauri yetu ya Liwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili limesababisha viwanja Wilaya ya Liwale viuzwe ghali sana kwa sababu mara nyingi tunatumia wataalam kutoka nje; badala ya sisi wenyewe kupewa vifaa vya upimaji tukaenda kupima ardhi ili watu wapate viwanja kwa bei nzuri. Kuna tatizo kubwa sana la vifaa vya upimaji wa ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuiangalia Halmashauri ya Wilaya ya Liwale hasa kwa upande wa watumishi wa ardhi pamoja na vifaa ili nasi tuweze kufanya matumizi bora ya ardhi. Kwa sababu sasa hivi tunashindwa kupata wawekezaji; mwaka jana tulipata mwekezaji lakini kijiji ambacho ilikuwa aende kikakutwa bado hakijafanyiwa matumizi bora ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na jambo hili sehemu nyingi tunakosa wawekezaji kwa sababu vijiji vyetu vingi havijaingia kwenye matumizi bora ya Ardhi. Hakuna mtu ama Kamishna ambaye anaweza akatoa hati kwa mwekezaji kwenye kijiji ambacho hakijapata matumizi bora ya Ardhi.