Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nina shukrani kubwa mbele za Mungu hasa kujibu hoja leo hii mbele ya Mwalimu wangu aliyenifundisha Kiswahili, baada ya kufika darasa la kwanza nikiwa sijui Kiswahili na leo atashuhudia kwamba mwanafunzi wake alifaulu. Maana yake siku ya kwanza niliporipoti niliambiwa tupa takataka, nikatupa madaftari; tupa madaftari, nikatupa vyote kwenye maua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, mafanikio makubwa ya Mwalimu huyu, baada ya kujua Kiswahili, niliweza kupata mke mrembo Kilimanjaro na nikaoa. Imagine, nisingejua Kiswahili ningempata vipi binti huyu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye kujibu hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Katika mazingira ya kawaida, itakuwa vigumu sana kujibu hoja moja moja, lakini vile vile huenda nisiweze kuwataja Wabunge wote kwa majina kufuatana na wingi wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja hii imechangiwa na Wabunge zaidi ya 92. Kwa ujumla wenu Waheshimiwa Wabunge, tunashukuru sana kwa maoni yenu. Nami niseme, tutawajibu kwa maandishi, tunatambua umuhimu wa hoja zenu, lakini pia siyo tu kuishia kwenye majibu, niwaahidi tu baada ya Bunge nitapita eneo kwa eneo kufuatilia ufumbuzi wa hoja hizi mlizozitoa. Nitafika mpaka Mafia kwa Mheshimiwa Dau, ameongelea suala la wavuvi wake na hili tutalifanyia kazi na hatua hizo tutazichukua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo limeongelewa kwa kiwango kikubwa, linahusu pembejeo na hili limeongelewa na Wabunge wengi. Mambo mengine yanayohusiana na hili limehusishwa upande wa fedha. Niseme tu, tatizo kwenye Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, hasa katika mambo haya ambayo yamekuwa yakilalamikiwa na Watanzania, siyo fedha peke yake, kuna matatizo ya kiusimamizi, kimfumo na yale yanayohusisha mambo ya fedha. Sisi kama Wizara tumeamua tuhakikishe kwanza tunashughulikia yale ambayo yanahusiana na mfumo, muundo na utaratibu ambao umekuwa ukitumika katika upatikanaji huo wa pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mifumo yote ambayo imekuwa ikutumiwa na Serikali, hakuna ambao haujapata upungufu na mara zote nia ya Serikali imekuwa kuhakikisha kwamba kama inatenga fedha, fedha zile ziwafikie walengwa ili kuweza kutimiza jukumu hilo. Kwa hiyo, sisi kama Wizara, tunavyoliangalia jambo hili tumekuwa tukiangalia utaratibu ambao pembejeo hizo zitaweza kupata mchango ule ambao ni wa ruzuku zinapoingia ili zinapokuwa zimeshaingia ziweze kusambaa zikiwa tayari zina ruzuku na kila mtu aweze kuzipokea.
Kwa hiyo, jambo hili linahusisha Wizara zaidi ya moja, nasi tuna- coordinate na wenzetu ili tuweze kuona namna ambavyo formula hii itaweza kukubalika ya kuweza kuweka ruzuku kwenye source wakati bidhaa hiyo inaingia na punde inapokuwa imeshaingia iweze kuwafikia wakulima wote.
Hiyo ndiyo ilikuwa dhana ya kusema pembejeo; zikiwemo mbolea, mbegu, madawa, yatawafikia wahitaji kama Coca-Cola inavyowafikia matajiri na maskini na kwa wakati, popote pale wanapohitaji kupata bidhaa hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa tunachokiangalia ni namna ya kuiweka ile formula kwenye bidhaa inapoingia. Mathalan mbolea inapoingia, iwe imeshakuwa na ruzuku na tunapiga hesabu ambayo itasaidia kwamba bei iwe ile ile ambayo inakuwa sawa na iliyokuwa inatumia vocha, lakini iwe wazi kwa tani zote ambazo zinapatikana. Tuhangaike na namna ya kulinda mbolea yetu isiende katika Mataifa mengine kwa sababu itakuwa ya bei nafuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanikisha hili, tunawaza, pamoja na fedha zinazotengwa kwa ajili ya ruzuku, tunawaza makato yaliyokuwa yanaenda kutumika kwenye shughuli nyingine iweze kuelekezwa kwenye Mifuko ya kuendeleza mazao husika ili wakulima waweze kunufaika na fedha wanazokatwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa bado kuna mjadala kuhusu makato yale yanayokatwa kwenye ngazi za Halmashauri kwamba ipunguzwe kutoka 5% kwenda 3% kama ambavyo sheria imekuwa ikisema. Tukasema kama haipunguzwi, basi tuikate asilimia nusu iende kwenye Halmashauri na nusu iende kwenye Mfuko wa Kuendeleza Mazao ili wakulima watakapokuwa wamekatwa, watambue kwamba watapata pembejeo katika bei nafuu ambazo zitakuwa zimeshapata fedha kutokana na fedha zile walizokatwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni sawasawa na ile ambayo Waheshimiwa Wabunge waliisemea; alisema Mheshimiwa Njalu na Mheshimiwa Doto, kwamba kulikuwepo na utaratibu wa zamani uliokuwa unaitwa pass kwa ajili ya pamba na wakulima walikuwa wananufaika kutokana na fedha walizochangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Ushirika, Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea sana. Kama nilivyosema na yenyewe hii tuko kwenye kuiunda upya. Baada ya kuwa tumepata Tume, sasa tunaangalia uwezekano wa kusuka upya kikosi kwenye Tume ya Ushirika na Muundo wake ambao utasaidia usimamizi uwe makini na uweze kusaidia hawa watu kutimiza majukumu yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wengine waliokuwa katika ngazi ya Halmashauri na Mikoa. Kimuundo, mapendekezo ya kutaka kuwapeleka katika Tume ya Ushirika; na tunasema kila mmoja ataonesha umuhimu wake wa kuwepo kwenye Tume hiyo kufuatana na majukumu anayoyatekeleza. Wengi wao ambao watakuwa walisahau majukumu yao, tunawapa fursa wahakikishe kwamba kila mmoja anafanya jukumu lake kuhakikisha kwamba anapata sifa ya kuwa katika Tume hiyo ya Ushirika. Hilo litatusaidia katika kuhakikisha Tume hii inatekeleza majukumu yake kama ilivyokuwa imekusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wameuliza pia, tunatumia utaratibu gani katika kuhakikisha kwamba tunaondokana na zana duni? Waheshimiwa Wabunge, niseme jambo hili linawezekana na kwa kuwa tayari Sekta Binafsi na Serikali imekuwa na miradi ya aina hii ya usambazaji wa matrekta, hata hivi sasa tayari tumeshapiga hatua, lakini tunapoendelea pia tunapanga kuhakikisha kwamba tunaondokana na kilimo cha jembe la mkono kwa sababu mageuzi ya kilimo yanahitaji utaratibu wa kutumia zana za kisasa katika kulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata vijana hawa niliokuwa nahimiza kwamba tunataka kuwapeleka vijana kwenda kulima, siyo kwamba watakwenda kulima kwa kutumia jembe la mkono. Hakuna kijana atatoka Chuo Kikuu halafu akahamasika kulima ekari tano, kumi kwa kutumia jembe la mkono. Tunapoongelea tunataka kuwapeleka vijana kwenye kilimo, tunasemea kwamba tunakwenda kubadilisha kilimo kiwe cha matrekta.
Waheshimiwa Wabunge, pana jambo moja ambalo kama Taifa bado tunakosea namna ya kuliingilia kwenye suala hili la matrekta. Kwa Watanzania wa kawaida, sio kila Mtanzania lazima awe na trekta lake. Mtu mwenye ekari tano, 10, 50 au 70; mtu mwenye ekari 50 siyo lazima awe na trekta lake. Sisi kama Serikali jambo ambalo tunataka tuhangaike nalo ni upatikanaji wa matrekta pale punde mkulima anapotaka kupata trekta aweze kulimia. Tunafanyaje?
Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ya wenzetu ambao wamehama kutoka jembe la mkono kwenda kwenye kilimo cha matrekta, wana centre ambapo matrekta yanapatikana kwa ajili ya kukodisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo ilivyo kwa sasa, siyo kila Mtanzania lazima awe na bodaboda yake kwa ajili ya kumwahisha anakotaka kwenda; siyo kila Mtanzania lazima awe na basi lake kwa ajili ya kumpeleka Mkoa hadi Mkoa. Isipokuwa kila wakati anapotaka kupanda basi, anakuta mabasi yapo; kila wakati anapotaka kupanda bodaboda, anakuta bodaboda ipo.
Kwa hiyo, tunataka katika kupiga hesabu katika Mkoa, mathalan Rukwa, ukishajua ekari zinazopaswa kulima ni kiasi kadhaa, tunatakiwa tuwe na matrekta yanayotosha kulima ekari hizo; ikiwezekana kila ngazi ya Tarafa, ili mkulima anapotaka kupata trekta aweze kuyapata. Hiyo ndiyo dhana tunayosema ya kulipeleka jembe la mkono kwenye makumbusho na vijana wa leo, watoto wanaozaliwa hizi siku za karibuni waweze kuliona jembe la mkono makumbusho au wanapokwenda makaburini pindi panapokuwepo na haja ya kuchimba kaburi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo tunahangaika nalo ambalo lipo na kwenye bajeti, tunaangalia...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri, kabla hujaanza hili jambo lingine, naomba ukae kidogo.
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kunipa fursa ya kuendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo tunaendelea nalo kwa sasa ambalo tunategemea kulitekeleza ni jambo la maghala na kutakuwa na maghala nane katika Kanda za uzalishaji, lakini pia katika Kanda za Usambazaji ambako itatusaida kurahisisha upatikanaji wa mahindi ama nafaka hizo kufuatana na uhitaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, alitoa ushauri Mheshimiwa Serukamba kuhusu kuhusisha pia na Sekta Binafsi katika ununuzi huu wa mahindi. Sisi tunaona hilo ni jambo jema. Ikumbukwe kwamba kwa kutumia NFRA peke yake kununua mahindi, ni kweli NFRA malengo yake ni kuweka mahindi ya akiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyoongea, tumepata uhitaji wa mahindi kutoka nchi nyingize za jirani, mfano DRC walikuwa wanahitaji tani 60,000; South Africa walikuwa wanahitaji tani 30,000; Zambia walikuwa wanahitaji tani 10,000; Zimbabwe tani 10,000; Sudani ya Kusini walikuwa wanahitaji zaidi ya tani 30,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, kipindi walipokuja kutuomba ni kipindi ambacho na sisi tayari tulikuwa na mahitaji mengi ya mahindi katika mikoa tofauti tofauti ya njaa, hatukuweza kuwapatia. Kwa hiyo, uwepo wa Sekta Binafsi pamoja na Bodi yetu ya Mazao Mchanganyiko, tunataka ifanye kazi hiyo na tayari nilishaelekeza kwenye Bodi ya Mazao Mchanganyiko waangalie setup ambayo itatuwezesha kuwa na wazo la aina hiyo na Bodi ya Mazao Mchanganyiko waweze kuwa na nafasi yao kwa ajili ya mazao yale ambayo itakuwa kwa namna moja ni soko la wakulima wetu ili kuweza kupanua wigo wa ununuzi wa nafaka kutoka kwa wakulima wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwa upande wa wafugaji, Waheshimiwa Wabunge wameongelea sana kuhusu migogoro. Namshukuru Naibu Waziri wa Ardhi kwa niaba ya Wizara ya Ardhi wamelisemea. Sisi kama Wizara, mambo tunayowaza kuhusu wafugaji yako ya aina hii: jambo la kwanza, tunagawa makundi ya ufugaji katika ngazi mbili.
Ngazi ya kwanza tunasemea wale wafugaji ambao wapo kwenye vijiji, wana ng‟ombe wanaotumika kwa kufuga na kwa kulimia na kwa diet kwa ajili ya vyakula vya familia. Tunasema hawa tutashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Ardhi kwa ajili ya kuangalia mpangilio wa matumizi bora ya ardhi ambayo upangaji wake unahusisha Kamati za Ardhi zilizoko katika ngazi za vijiji. Kwa maana hiyo, hili katika kila Kijiji tumesema pawe na Kamati, wajiwekee utaratibu wao kwamba kutoka eneo fulani mpaka eneo fulani itakuwa ni kwa ajili ya mifugo, kutoka eneo fulani mpaka eneo fulani itakuwa ni kwa ajili ya ufugaji.
Ngazi ya pili tunayohangaika nayo, ni ile ya makundi makubwa, wale ambao wana ng‟ombe 1000, 2,000, 3,000 na kuna wengine wamebarikiwa wana hata zaidi ya ng‟ombe 6,000 na wengine 9,000. Kwenye makundi haya, tunasema tutawageuza wenye mifugo ya aina hii kuwa ndio wawekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaopongelea wawekezaji, wawekezaji wa kwanza ambao tutawalenga ni hawa hawa ambao tayari wana mifugo hiyo. Kwa maana hiyo, wale wote ambao walikuwa na ranch wamechukua maeneo, wamesema wanahangaika kutafuta mifugo, tunawaambia wala wasihangaike kutafuta mifugo kwa sababu sisi tayari tuna wafugaji wenye mifugo na wana hobby ya kufuga.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutakalofanya, timu tayari inafanyia tathmini ya maeneo ya aina hiyo yaliyokuwa yanakodishwa. Baada ya hapo, tutapiga hesabu ya mifugo iliyopo tena kwa uwiano wa kitaalam, wa kisasa kwamba mifugo mingapi inatakiwa ichunge eneo gani kwa ajili ya ufugaji endelevu (sustainability) ili tuweze kugawa mifugo ya aina hiyo katika maeneo hayo.
Baada ya kuwa tumeshatengeneza utaratibu wa aina hiyo, ndipo tutakapomshirikisha ndugu yangu, pacha wangu Mheshimiwa Mwijage ili kuweza kushawishi watu waweke viwanda kwa ajili ya ufugaji endelevu. Kwa mazingira yalivyo sasa, imekuwa vigumu sana kwa mtu yeyote kumshawishi aweke kiwanda cha maziwa, kwa sababu hajui wale wafugaji pale ndugu zangu na Mheshimiwa Naibu pale, haijulikani kama mpaka wiki ijayo watakuwa bado wako pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ukiweka kiwanda, kesho wakahama, maana yake ni kwamba kiwanda kile hakitaweza kufanya kazi. Hivyo hivyo na kwenye nyama na ngozi. Tukishamaliza kuwaweka kwenye utaratibu ule, maana yake haya mazao yanayotokana na mifugo yataweza kupata soko lake na yataweza kushawishi kuwepo kwa kiwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo na lile alilolisemea Mheshimiwa Serukamba, linalohusu machinjio, kwa sababu elimu ya kuhusu kupanda majani, kupunguza idadi wa mifugo ina uhusiano wa moja kwa moja na unapopunguza ile mifugo unaipeleka wapi? Kama pana soko, sasa hivi wafugaji wanaweka fedha kwa muundo wa mifugo, lakini pakiwa na soko maana yake kama kuna kiwanda, kama kuna machinjio wataweka mifugo in terms of fedha. Kwa hiyo, hilo ndilo ambao tunaliangalia kwa namna hiyo na baada ya Bunge la Bajeti tunategemea kuanza kuzunguka katika maeneo hayo kuhakikisha tunalifanya hilo jambo kwa namna hiyo.
Kwa hiyo Mheshimiwa Doto, Mheshimiwa Mukasa, Mheshimiwa Bashungwa, Bilakwate pamoja na Mheshimiwa Shangazi na wengine ambao mlilisemea Mbunge wa Arumeru Ole-Meiseyeki. Tunafanya kwa utaratibu huo na kabla hatuja maliza Bunge hili tutapata fursa ya kukaa na viongozi wa wafugaji watakuja kwa kanda na kwa Wilaya kwa ajili ya mapendekezo ya namna ambavyo tunafanya. Lakini kwa yale yanayohusisha Wizara zaidi ya moja tutapata fursa ya kukaa na Wizara nyingine, lakini kwa yale yanayohusu kilimo, ufugaji na uvuvi yale yapo ndani ya Wizara yetu na sisi tutafanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine linalohusiana na eneo hili kuna malalamiko mengi yanatolewa kuhusu makato mengi kwenye sekta ya maziwa, zamani hatua ziliwahi kuchukuliwa, sasa tutaongea na wenzetu wa fedha na tutawaandikia rasmi, waangalie uwezekano wa zero rating kwenye maziwa na bidhaa zake. Waangalie pia kuondoa kodi kwenye vifungashio vya maziwa kwa sababu hizi sekta bado chaga sana vinginevyo tutaendelea kuona wafugaji wakimwaga maziwa, halafu na tukitumia maziwa yanayotoka katika viwanda vya kutoka nchi jirani.
Kwa hiyo, tutayaangalia hayo na kwa kadri ambavyo tumefuatilia tumeona hata kiwango ambacho kinatoka huko kwa sababu ya uchanga wa sekta wala hakijawa kikubwa kwa kiwango hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikirejea tena kwenye jambo moja ambalo liliongelewa na Waheshimiwa Wabunge wengi, nimpongeze Mheshimiwa Kangi Lugola aliliongelea, Mheshimiwa Aeshi, Mheshimiwa Nsanzugwanko ni suala la mbolea. Mbolea ya Minjingu ni kweli kuna kipindi ilikuwa inalalamikiwa, mimi nimepata fursa ya kuongea na wataalam wangu, lakini nikaambiwa kwanza wamebadilisha formula, waliyokuwa wanatumia mwanzoni mchanganuo wake waliokuwa wanatengeneza mwanzoni wameubadilisha, wame-develop kufuatana na uhitaji wa maeneo yetu, kwa sasa ukienda Kenya wanatumia mbolea nyingi zaidi ya Minjingu kuliko mbolea wanayotoa maeneo mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hapa kwa sababu ya kampeni hiyo na formula ile iliyokuwepo kumekuwepo na watu kuaminishwa kutokana na watu ambao wamesema bila kuamini kutokana na fomula lakini pia na matokeo yaliyotokea katika mashamba yenyewe. Kwa hiyo, kwa sasa hivi niliwaambia hata wao wataalam wahakikishe wanaelezea watu vitu vya kitafiti wananchi wanatakiwa wavijue. Kwa hiyo, naamini hilo watalifanya lakini pia niliwaambia na wenye kiwanda na wenyewe waelezee kwamba hivi NPK ya Minjingu inatofauti gani kwa formula na NPK ambayo siyo ya Minjingu. Kwa sababu Mwalimu Nyerere aliwahi kusema jambo la kipuuzi likisemwa Kiingereza linaonekana ni zuri, kwa hiyo kuna watu tu inawezekana wanaona Minjingu ni la Kiswahili, wanaona labda mbolea hii ni ya kiswahili-kiswahili.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tumesema wataalam wasemee zile fomula kwa muundo wa fomula NPK ya minjingu na NPK nyingine tunazozileta, urea ya Minjingu na urea kutoka sehemu nyingine kitaalam kwa zile content zenyewe tofauti zake ni nini ili tuweze kujua na watu wetu wayajue hayo, ili wanapotumia watumie wakiwa wanajua lakini wafuatilie na formula zake zilivyokuwa zinatakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo mengine ambayo tuliyasemea Wizara lilikuwa ni jambo la kuwapeleka vijana shambani, jambo hili tumeshaongea na Waziri wa Ardhi na baada ya Bajeti tutakaa pamoja katika kuweka mkakati. Lakini sisi Wizara tunaanzia na mashamba yale ambayo yamebaki kama mapori. Shida moja kijana anayoipata moja ukimwambia tu aende akalime anaweza akashiriki katika lile shamba tu la mzee akalima, akashiriki kama tulivyokuwa tunafanya, Kinyiramba tulikuwa tunaita Nsoza unalimalima pembeni lakini sehemu kubwa unalima ya mzee. Tukisema tunaenda kwenye kilimo cha kisasa kijana atapata shida ya shamba, shida ya mahitaji yale ya kilimo cha kisasa, atapata shida ya matrekta, atapata shida mambo ya umwagiliaji, tunategemea Wizara hizi tukae tuamua tuone namna ya kutatua moja baada ya lingine. Lakini Wizara tumesema tutaanza na mashamba yale yanayomilikiwa na Wizara ambayo yamekaa kama mapori kama ulivyosema lile la Bugagara ambalo lipo kule kwako.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutakachofanya kwa sababu mbegu zinahitajika tunatafuta vijana waliopo kule wakae kwenye kikundi wanaotaka kulima mbegu na soko lake la uhakika, mbegu zile zinahitajika. Sasa hivi tunaagiza mbegu kwa zaidi ya asilimia 60 kwa hiyo kwa kuwa zinahitajika tuna uhakika kwa kuuzia mbegu zile, shamba lipo limekuwa pori, sisi ambacho tutasaidia ni namna ya kulima, mbegu ya kulima na namna ya kumwagilia ili tuweze kuhakikisha kwamba vijana wale wanaweza kufanya shughuli hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata la ndugu yangu alilolisemea rafiki yangu Mollel, jambo lile pia linafanyiwa kazi, lile shamba hata hivi tunavyoongea Waziri yupo kule linafanyiwa kazi patakuwepo na sehemu ambayo vijana wako watapata ardhi ya kuendelea kutumia na patakuwepo na sehemu ambayo ushirika utakuwa na sehemu yao katika program yao. Serikali marazote ina nia njema ya kuhakikisha kwamba ina-balance mambo haya ya uchumi ili shughuli za uzalishaji ziweze kuendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwa ndugu yangu Mheshimiwa Joseph Kakunda alisemea fedha zile ambazo zilishakusanywa, nimepokea hoja yako nitakaa na wataalam wangu ili tuweze kulimaliza jambo hilo vizuri na liweze kufanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwaka pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine walioongelea mazao ya kwetu kutumika, Mheshimiwa Ngonyani alisema kuhusu benki, kupelekwa sehemu kubwa ya uzalishaji ambayo ipo Ruvuma pamoja na wengine walioongelea Benki ya Kilimo. Tumepokea hoja zenu tunazipa uzito na tutahakikisha kwamba tunalifanyia kazi jambo hilo na liweze kuwafikia watu hawa waliopo maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ndassa ameongelea suala la mbegu za pamba, tumekaa juzi juzi nilienda Mwanza nilikaa na watu wetu wa Ukiriguru. Niliongelea suala la pamba kwamba wakati tuna watafiti wachache enzi zile pamba ilikuwa inafanya vizuri na mbegu zilikuwa zinaota, lakini sasa tuna watafiti wengi, tuna watalaam wengi, tunao wasomi wengi, tumesambaza Maafisa Ugani ndicho kipindi ambacho mbegu hazioti, Nikawaambia lazima tuangalie ni wapi ambapo tumefanya makosa, kwa hiyo sasa hivi baada ya bajeti nitakutana na timu ile niliyoiunda ya wataalam kutoka Ukiriguru pamoja na watu wanaofanya kazi hiyo waje watuambie bila kuwa na mtazamo wa kimaslahi binafsi ili tuweze kupata jawabu la kudumu na watu wetu wa Kanda ya Ziwa ambao nembo yao mara nyingi ilikuwa pamba iweze kurejea katika hali yao, hivyo tutafanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata taasisi za utafiti tutaongea ngazi ya Wizara tuone kama na wenyewe wanaweza wakawa na shamba darasa la mbegu ili kuweza kuonyesha tofauti ya wao na wale wengine wanaozalisha kwa maslahi binafsi ambao katika maeneo mengine kwa wale wasio waaminifu mbegu zinazotolewa zinakuwa zilishaathiriwa na maslahi binafsi ikiwemo kuweka mawe ama kuziwekea maji kwa ajili ya kutafuta namna ya kujipatia kipato zaidi.
Mheshimiwa Almas Maige, Mama Sitta pamoja na Wabunge wa Mkoa wa Tabora nimesikia hoja yenu na mimi sina namna tukishamaliza shughuli hizi za Wizara nitakuja Tabora siyo mbali. Nitaunganisha na Wabunge wa Singida ambao wameongelea kuhusu alizeti na mimi ni mdau mkubwa wa alizeti na huko tutatafuta muda tutakuwa tunakimbia kuweza kuona namna ambavyo tunahamasisha shughuli hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni sambamba na yale ambayo yaliongelewa na Mheshimiwa Juma Nkamia ambapo ameongelea kuhusu eneo lake la Jimbo lake pamoja na majimbo jirani ikiwemo kwa mtani wangu Naibu Waziri wa Fedha. Nitakuja huko lakini niwaombe tu msinilazimishe kuwaletea nyama ya punda kwa sababu tulikuwa tunataniwa zamani tu, siku hizi huwa hatuli tunajua punda ni kwa ajili ya kubebea mizigo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo lilijitokeza kwa kiwango kikubwa ni majosho pamoja na mabwawa. Mheshimiwa Bobali alisema tunakusudia kutumia Jeshi kwenye uvuvi, ulinukuu vibaya. Tulisema tunapanga kuongea na wenzetu wa Wizara ya Ulinzi kutumia vifaa vya Jeshi kuchimba mabwawa. Kwenye uvuvi hatujaongelea kuhusu kutumia Jeshi, tunachosema ni kwamba, kama tumetenga fedha kidogo ambazo zinaweza kutumika kujaza mafuta, kila Wilaya ina ma-engineer wanaoweza kusema bwawa linatakiwa liweje, kila Wilaya wakajua sehemu ambazo zinaweza zikawa na bwawa na wenzetu wa Jeshi wana vifaa na Wizara ya Maji pia kuna vifaa walivyochukua kutoka Wizara ya Mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini fedha zile tulizotenga zisitumiike tu kwa ajili ya kuweka mafuta, lakini vifaa kwa sababu vipo tutumie vile vifaa vichimbe mabwawa. Babu zetu zamani walikuwa wanachimba mabwawa kwa mikono. Kwa hiyo tunaamini kwamba tunaweza tukaongea, tunaandaa utaratibu wa kuwasiliana Kiserikali lakini nimeshaongea na Mheshimiwa Waziri tuone namna ipi itakuwa rahisi kuliko utaratibu wa mabwawa ya zabuni ambayo yanachukua muda mrefu lakini pia yanatumia gharama kubwa na kuwafanya wafugaji wasiendelee kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niliyekulia jamii ya kifugaji ukiniambia bwawa mimi ninachojua ni kukinga maji yaliyokuwa yanapita yanazagaa, ukipeleka mitambo ile kama ya Kijeshi naamini itaweka mazuio na maji yatapatikana na wafugaji watapata mahali pa kunyweshea maji, hicho ndicho tulichokuwa tunasemea kuhusu matumizi ya Jeshi, tulikuwa tunaongelea vifaa vya Kijeshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upande wa korosho, Mheshimiwa Mama Ghasia, Mheshimiwa Mwambe pamoja na ndugu yangu Mpakate na wengine Kaunje, Mheshimiwa Chikota na wengine wote wa ukanda wa maeneo yapotoka mazao ya korosho, kwanza nitakuja mwenyewe.
Mliniambia hata matatizo ya bodi niwaambie tu, nitoe siri Waheshimiwa Wabunge kuna bodi nyingi sana kwenye upande wa mazao ya kilimo mpaka sasa nilikuwa bado sijapeleka mapandekezo ya majina, sababu kubwa ni moja tu na niseme na wenye bodi zile wajitambue, nilikuwanafanya tathmini ya justification ya uwepo wa bodi hizo, na kwenye vyama vya ushirika hivyo hivyo, kwenye APEX nilikuwa nafanya tathmini kwamba hivi kuna mazao hayana bodi, hatuna ulalamishi wowote wa kuhusu makato, hatuna ulalamishi kuhusu kuibiwa, watu hawa wanazalisha hakuna kesi ya wizi, hakuna kesi ya makato, hakuna kesi ya unyonyaji, hakuna kesi ya madeni ya mikopo kwa ajili ya kutumia hivi vitu na yanafanya kazi vizuri tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mpunga sasa hivi ni wa tatu kwa uzalishaji wa mpunga na hatuna bodi ya mpunga. Halafu maeneo ambapo tuna bodi ndipo wizi upo mkubwa, unyonyaji mkubwa, nitoe rai kwa maeneo haya niliyoyataja wajitathmini, wa-justify uwepo wao, kama hawatakuwepo tutatengeneza kuwa na bodi ya mchanganyiko halafu na bodi ya mazao ya biashara halafu tutatumia watendaji kusimamia mambo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni fursa yao ya mwisho, kwa sababu hatuwezi tukawa na taasisi ambazo zinatumika kama vichaka vya kuwanyonya wale ambao wanavuja jasho katika kazi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu makato hatuwezi tukawa na taasisi ambazo zinafanya kazi ya kuwa kichaka cha kuwanyonya wale wanaovuja jasho katika kuzalisha mazao hayo. Tunahitaji taasisi zozote zinazokuwepo zioneshe uhalali wao wa kuwepo katika shughuli hizo ambazo zinafanya zenyewe ziwepo. Hivyo hivyo hata kwa wataalam wetu.
Kwa hiyo, kwa upande wa makato tumebainisha maeneo yote. Mheshimiwa Kiswaga, Mheshimiwa Mabula pamoja na wengine wote wanaotoka ukanda wa uvuvi, tumeyapitia makato ya leseni yote tumeorodhesha, tumepitia makato yote kwenye mazao yote yaliyokuwa yanakatwa. Sasa hivi tunachofanya tumeshayafanyia uamuzi, kuhusu makato yale yanayokatwa, kama Wizara tunayofanya ni mawasiliano ya Kiserikali tunavyoelekea kwenye Muswada wa Fedha ambao utakuja mwishoni ili tuone yapi ambayo tutataja kwamba tumeshayafuta kwa sababu yanatakiwa yaingie kwenye kufutwa kule.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wavuvi kwa mfano wanapata leseni ya uvuvi, Leseni ya Vibarua, SUMATRA, BMU, Zimamoto, sasa zimamoto kule kwenye kuvua, maji yenyewe si ndiyo zimamoto, kwa sababu magari yenyewe hayaji na maji. Kwa hiyo, tunaangalia yale ambayo kwa kweli uwepo wake imetumika kama kichaka, tunaenda kuyafuta na tunahakikisha watu wetu wanapata tija. Nasikia mambo ya aina hii aliyasema pia Mheshimiwa Kemirembe, Mheshimiwa Kiteto pamoja na ndugu yangu wa Jimbo la Rorya Mheshimiwa Airo.
Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, hoja ni nyingi lakini kwenye makato niwahakikishie kwamba yote tulishaorodhesha na tunategemea tu-share na wenzetu tunapotengeneza sheria ile ili tuweze kurekebisha. Hiyo ndiyo ilikuwa dhana halisi ya kutengeneza chombo cha aina moja kinachokusanya ili kuweza kuondoa mlolongo. Hivyo hivyo na kwenye mageti, watu wengine walikuwa wanasema Halmashauri zitakosa mapato, Waheshimiwa Wabunge ninawaambia tu kwa nia njema, katika mazingira tuliyo nayo tunatoza ushuru mara mbili kwa zao moja ama bidhaa moja mara nyingi mno, watu wetu mpaka wanatushangaa! kwa hiyo lazima tutafute formula kitu ambacho kimeshatozwa, tena ni mara mia ikatozwa kwa kiwango kikubwa lakini mtu akajua sina usumbufu nikishalipa kitu cha aina hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, watu wetu wanasumbuliwa fedha nyingine zinapotea kwenye rushwa tu, watu wengine wanapata ajali ya kupita usiku wanakimbizana na wale walioweka mageti, ni lazima tukaweka utaratibu kama Halmashauri zetu ziseme kwenye mageti zilipata fedha kiasi gani halafu zipewe, fedha nyingi zinapotelea kwa wale wanaokaa kwenye mageti na kuwatoza rushwa wale watu. Tutengeneze utaratibu bidhaa ikishalipiwa kodi ikawa na risiti, ile risiti imtoshe mtu kutembea akiwa anajua kwamba nimeshalimaliza hili, sitabugudhiwa na mtu na nakwenda kufanya kitu chenye tija. Hiyo ndiyo dhana halisi ambayo tunaiangalia katika taswira hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua sokoni ndiko ushuru unapotolewa, ukishafika mtu akawa na leseni anajua ameshatoa na masoko haya tunajenga kila mahali watolee katika maeneo hayo. Hiyo ni sawa sawa na maeneo ya minada na kwenye minada hivyo hivyo, kama mtu atakuwa ameshatozwa leseni ama ameshatozwa ushuru basi ile risiti ambayo ametumia kutozwa iwe inatosha anapokuwa ameenda katika eneo lingine.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimepokea yale ya ndugu yangu Airo mnada ya Kirumi pale tumesema utaendelea hivyo hivyo, tulipokea pia mnada wa Magena kutoka kwa bibi yangu pembeni kule Tarime. Sisi kama Wizara tumesema wenzetu wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wamesema sababu zilizosababisha mwanzoni isiwe hatuoni ubaya kama kutakuwa na mnada ambao upo Kirumi siku yake na kukawa na mnada huko Magena siku yake na kuna mnada upo pale mpakani kidogo na Kenya na wenyewe upo siku yake. Kwa hiyo mambo ya aina hii tunayaangalia na tutaangalia financial implication zake, lakini siyo jambo la kufa na kupona tukigombana na watu wanaotaka wakusanye fedha na watupatie fedha kama Serikali.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mazingira ya kawaida mambo yale yanayohusisha Wizara yetu na Wizara nyingine Serikali ni moja, Mheshimiwa Mukasa waambie wananchi wako wala wasinoe mapanga, Serikali tutakaa tutaamua, tutatoa uongozi ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanafanya kazi katika mazingira yaliyo rafiki kwa wao kuweza kufanya kazi hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya niendelee kusema kwamba Waheshimiwa Wabunge michango yenu ni bora sana tumeshaipokea, siyo tu kwa ajili ya majibu tutaifanyia kazi na niendelee kusema kama mnataka mali mtazipata shambani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba sasa kutoa hoja!