Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kijiji cha Lumecha wanaleta tena changamoto ya ardhi yao ya shamba la Likenangena waliyoikabidhi kwa Kampuni ya Tumbaku waliyoiazima kwa ajili ya kuandaa mbegu za tumbaku. Baada ya kusitisha kuendelea na uzalishaji wa mbegu za tumbaku Kampuni hiyo ya TLTC ambayo kwa sasa wamehamia Morogoro hawajairudisha ardhi hiyo ya Likenangena kwa wenyewe, yaani Kijiji cha Lumecha, Kata ya Msindo, Wilaya ya Namtumbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hao hawana uwezo wa kuwafuatilia Kampuni ya TLTC huko Morogoro, wanamwomba Mheshimiwa Waziri awasaidie wananchi hao warudishiwe ardhi yao waweze kuitumia kwa kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, historia ya shamba hilo ni ndefu na Mheshimiwa Waziri anao uwezo wa kuipata kupitia watalaam wako wa ardhi wa kuanzia Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo, Mkoani Ruvuma hadi hapo Wizarani. Wananchi hao kila wakitoa changamoto yao kwa wataalam wako, wataalam hao wanasikiliza lakini hawafanyi chochote cha kuwasaidia wananchi hao wakidhi haja zao. Ardhi hiyo ilitolewa bila malipo yoyote na hivyo dhana ya kuwa ardhi hiyo ni mali ya TLTC haikubaliki na haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri William Vangimembe Lukuvi, Mbunge wa Isimani mwenye dhamana ya Ardhi, anisaidie wananchi wa Kijiji hicho cha Lumecha wapate haki yao, warudishiwe ardhi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninalo tatizo la pili, katika Jimbo langu ambalo ni Wilaya yote ya Namtumbo tatizo lenyewe limesababishwa na Wizara yako kutoa Hatimiliki kwa Chuo cha Wanyamapori cha Likuyu- Sekamaganga kwa eneo kubwa lililochukuliwa na eneo la Kijiji cha Likuyu-Sekamaganga linalotumiwa na wanakijiji hao kwa shughuli za kilimo cha mazao mchanganyiko bila ya kuwahusisha wanakijiji hao wenye ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipaka ya ardhi ya Chuo hicho ilipanuliwa na kuchukua ardhi ya kilimo cha wakazi wa Kijiji cha Likuyu-Sekamaganga bila ya ridhaa yao, matokeo yake baada ya hatimiliki kutolewa na Kamishna wa Ardhi, Uongozi wa Chuo hicho umekuwa ukiwatumia Askari Wanyamapori kuwanyanyasa wakulima wa Kijiji cha Likuyu-Sekamaganga huku wakiwafukuza katika ardhi yao na kupelekwa mahabusu kwa makosa ya kutungwa. Hatimiliki ya ardhi iliyotolewa katika ardhi yao wanakijiji kwa chuo ndiyo kinga ya kuwapiga na kuwanyanyasa wanakijiji hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninakuomba kero hii uichunguze kwa umakini na hatimaye utoe haki kwa kurekebisha mipaka ya eneo lililotolewa hatimiliki kwa chuo kwa kuondoa eneo ambalo siyo sehemu ya chuo bali ni eneo la kilimo kwa wakazi wa Kijiji cha Likuyu- Sekamaganga ndani ya mipaka ya kijiji hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasilisha ili alifanyie kazi Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mheshimiwa William Vangimembe Lukuvi, Mbunge wa Isimani mwenye dhamana ya ardhi nchi hii.