Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais, kipekee kabisa kwa kuona umuhimu wa Wizara hii ya Madini, ndiyo maana akaanzisha Wizara kamili inayohusika na suala la madini. Kwa kweli nizidi kumtia moyo tu kwamba aendelee kuchapa kazi kwa sababu Watanzania tuko nyuma yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri, pamoja na Naibu Mawaziri wake kwa kazi kubwa wanayoifanya kwenye Wizara hii. Ni Wizara mpya lakini kazi wanazozifanya kwa kweli zinatutia moyo wananchi ambao tulikuwa na changamoto nyingi hapo siku za nyuma. Sasa hivi changamoto zinapungua siku hadi siku, hongera sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Mawaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri baada tu ya kuteuliwa aliweza kufunga safari akafika mpaka Geita, akaangalia changamoto za wachimbaji wa madini, wakubwa, wa kati na wadogo. Kwa kweli nampongeza sana Waziri na Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, ahsanteni sana kwa kusikiliza kero, wananchi wana imani na nanyi kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Mheshimiwa Nyongo, Naibu Waziri alikuja Nyarugusu akasilikiza kero tukiwa pamoja na watu wakauliza maswali mbalimbali. Nina hakika wanaendelea kuangalia hizi changamoto ili kuzifanyia kazi, nasema ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishukuru Wizara ya Madini, kwa jinsi ambavyo wametupa heshima kwenye Kijiji cha Rwamgasa kwa kutengeneza kituo cha mfano kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Busanda na Geita kwa ujumla tunashukuru kwa ajili ya kituo cha mfano cha Rwamgasa. Kwenye bajeti hii wamesema kwamba kimefikia asilimia 70 ya utekelezaji, naomba mwaka huu kiweze kukamilika ili wananchi waweze kunufaika na kujifunza mambo mazuri hasa wale wachimbaji wadogo ambao wamekuwa na changamoto kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kwamba nchi hii ya Tanzania inao wachimbaji wadogo wengi sana. Katika takwimu baada ya utafiti wa UNEP mwaka 2012 ni kwamba wachimbaji wadogo 500,000 mpaka 1,500,000 wameweza kuwa na ajira kupitia shughuli za uchimbaji. Kwa sasa hivi hali halisi inaonesha kama watu 2,000,000 ni wachimbaji wadogo ambao wanajishughulisha na shughuli za uchimbaji madini. Niombe Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara waangalie namna ya kuwasaidia hawa wachimbaji wadogo. Ni kweli wana mchango mkubwa sana kwenye Taifa hili, wakiwezeshwa kwa kupewa mitaji, pengine hata kwa kukopeshwa kwa riba nafuu, wataweza kufanya kazi zao kwa umakini na mwisho wa siku watakuwa na uwezo wa kuchangia kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, japokuwa kwenye bajeti sikuweza kuona mahali ambapo mmezungumzia habari ya kuwawezesha kwa kuwapa mitaji, naomba Wizara iangalie uwezekano wa kufanikisha suala hili. Siku za nyuma kulikuwa na programu hiyo ya kuwapa ruzuku wachimbaji wadogo, hebu basi tuangalie namna ya kuwawezesha kwa ruzuku au kwa mikopo yenye riba nafuu ili waweze kujiinua kiuchumi kupitia shughuli hizi za uchimbaji. Uchimbaji ni shughuli ambazo zinahitaji mtaji wa kutosha ili kuweza kuzifanya kwa umahiri. Kwa hiyo, niombe Wizara iangalie namna ya kuwasaidia wachimbaji wadogo kwa sababu wanahitaji kusaidiwa ili waweze kuchangia katika pato la Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna ule Mgodi wa Buckreef ambao uliingia ubia kati ya TANZAM pamoja na STAMICO. Ni miaka mingi sasa tangu mwaka 2011 lakini hatuoni kitu chochote kinachoendelea kwa ajili ya mchango wa wananchi. Wachimbaji wadogo waliondolewa akapewa TANZAM kwa ubia na STAMICO lakini hatuajaona faida ya mgodi huu. Nimefurahi kuona kwamba kwenye bajeti wamesema kwamba Serikali inaianyia utafiti kuona kama TANZAM na STAMICO waendelee au vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe suala hili lifanyiwe kazi kwa haraka zaidi kwa sababu tangu walivyoanza mwaka 2011 kuna baadhi ya wananchi walifanyiwa tathmini, wanatakiwa kulipwa fidia, mpaka leo hawajalipwa fidia yoyote na wanauliza ni lini sasa wataweza kulipwa fidia zao. Mashamba yao hawalimi, hawafanyi kitu chochote na hawayaendelezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huu ubia kati ya TANZAM na STAMICO kwa kweli ni kero kubwa sana katika maeneo yetu ya Rwamgasa na sehemu mbalimbali. Niombe Mheshimiwa Waziri mlifanyie kazi jambo hili ili hatimaye liweze kuleta tija. Kwa sababu lengo kubwa ya uwekezaji ni kuleta tija kwa wananchi wanaozunguka maeneo husika lakini pia kwa wananchi wetu kwa ujumla. Mpaka sasa hatuoni tija yoyote kupitia huyu mwekezaji TANZAM na STAMICO, ni ubia kwa asilimia 45 kwa 55 lakini hatuoni faida yoyote ya kuhusiana na uwekezaji huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto hiyo, tunaiomba Serikali sasa iangalie na kuchukua hatua mapema ili hatimaye wananchi waweze kunufaika na uwekezaji au madini yaliyopo katikati yetu. Tunamshukuru Mungu kwamba nchi ya Tanzania tunayo madini ya kutosha, tuna mambo mengi makubwa lakini sasa vitu vingi vimekuwa havitunufaishi vizuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa ajili ya kubadilisha hizi sheria, mwaka jana tumeweza kubadilisha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 tumepata sheria mpya ya mwaka 2017. Kwa hiyo, najua kabisa kwamba kupitia mabadiliko haya, ndiyo tunaona tija na mabadiliko mazuri ambayo ni kwa manufaa ya wananchi wetu na kwa ujumla kama Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazidi kuiomba Serikali iangalie katika migodi mbalimbali midogo na mikubwa, kwa mfano, katika Mkoa wetu wa Geita tuna rasilimali dhahabu lakini bado wananchi wa pale hatunufaiki ipasavyo. Kwa mfano, mitambo ya uchenjuaji wa dhahabu mingi iko Mwanza wananchi wa Geita hawanufaiki. Kwa hiyo, tunaomba Serikali itusaidie, hata hizi carbon zinazosafirishwa kila wakati kutoka Geita kwenda kuchenjuliwa Mwanza siyo mzuri, wananchi wa Geita wanakosa mapato ambapo pengine watoto wetu wangepata ajira pale kupitia uchenjuaji huu. Kwa hiyo, ikiwezekana tunaomba Serikali itusaidie wawekezaji wajenge mitambo yao ya uchenjuaji hapo hapo Geita ili hatimaye process zote za uchenjuaji wa dhahabu zifanyike Geita ili wananchi wa Geita waweze kunufaika na madini ambayo Mwenyezi Mungu amewapatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkitusaidia hilo hakika wananchi wa Geita hawatawasahau, watajua kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri amewasaidia na Mungu ataendelea kumuinua Waziri na kumbariki kwa sababu atakuwa amewasaidia sana. Kwa hiyo, niombe tu Serikali kupitia Wizara hebu wafanye utafiti kidogo juu ya jambo hili. Tunachotaka kupitia dhahabu wananchi wetu waweze kupata ajira. Tunajua kabisa Geita na maeneo mengi ambayo yanashughulika na kuchimba madini miji inakua kutokana na madini yaliyopo nasi tunahitaji kupitia dhahabu tuweze kunufaika zaidi. Kwa hiyo, uchenjuaji na viwanda vile vya kuongeza thamani ya madini, tunaomba pia vijengwe kwenye Mkoa wetu wa Geita ili wananchi waweze kunufaika zaidi. Ni kama korosho kule Mtwara, huwezi ukazungumzia korosho ukiwa Geita yaani kila kitu kinafanyika kule. Kwa hiyo, nasi tunaomba Geita sasa kila kitu kuhusiana na dhahabu kifanyike pale na kuwe na kituo kikubwa ili wananchi wetu pia waone umuhimu wa hiyo rasilimali ambayo Mungu ametupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naiomba Serikali iangalie wachimbaji wadogo kwa kuwawezesha mitaji ili tuweze kuona umuhimu wa kuweza kuchangia katika Pato la Taifa kupitia kuwawezesha wachimbaji hao. Kikubwa zaidi Wizara itusaidie kuendelea kuboresha zaidi sekta hii ya madini hasa katika suala zima la usafirishaji wa carbon na kuhakikisha kwamba tunajenga mitambo pale Mkoani Geita ili tuweze kunufaika zaidi vizazi vyetu pamoja na wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana, naunga mkono hoja kwa sababu mambo mengi yamekwisha kufanyika.