Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kwanza nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kufanya kazi kubwa na kuleta mabadiliko makubwa katika sekta hii ya madini. Pia kwa kuona Wizara hii inastahili kuwa peke yake na Wizara ya Nishati kuwa peke yake ambapo kwa Wizara zote mbili tutapata manufaa makubwa na ufanisi mkubwa wa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru Waziri, Naibu Mawaziri wote wawili pamoja na timu yao nzima kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya kuhakikisha kwamba sekta hii sasa inasimama vizuri na nchi yetu iweze kunufaika na rasilimali hii ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia. Naweza kusema kwamba kila aina ya madini yaliyopo duniani na Tanzania yapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la kwanza na siku zote huwa nasema hapa, kwenye bajeti hii nimeona pale mmeandika kwamba Oktoba mtaanza mafunzo katika Kituo cha TGC pale Arusha, kituo ambacho kitakuwa kinafundisha Watanzania jinsi ya kuchonga vito lakini pia na kupata mafunzo mbalimbali ya madini yaani vito pamoja na usonara lakini vifaa vinavyotakiwa pale bado havijatosheleza. Badala ya mashine 45 ambazo wanazo mngeongeza mashine zifike 100 na gharama yake siyo kubwa sana. Hii programu ya Diploma ni ya miaka mitatu (3) lakini bado mnaweza kuwa na certificate ambapo inafanyika International College Gemstones - Marekani, Bangkok na maeneo mengine ni miezi sita. Mtanzania ambaye hajui kusoma na kuandika kwa sababu kuchonga vito ni art yaani ile ni sanaa, kwa hiyo, mngeweze kufundisha watu 100 kwa kila miezi sita kwa muda wa miaka miwili (2) mtakuwa na watu 400 na hata mkipata asilimia 20 tu ambao watakuwa wazuri pale tayari madini mengi ya Tanzania tutaweza kusanifu hapa nchini na tutaweza kuongeza thamani na pia ajira itaongezeka kwa wingi sana. Kwa sababu tuna madini kwenye vito aina ya precious na semi-precious, zote hizo zitapata thamani na biashara hiyo itakuwa nzuri. Kwa hiyo, tunaomba kwenye bajeti hii mhakikishe kwamba mmeweka fedha ya kutosha ya kuwezesha kituo hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, siku za nyuma tulishafanya mabadiliko kwenye hizi leseni kubwa za Prospecting License (PL) ilikuwa unaruhusiwa kuwa na leseni nyingine za madini ya ujenzi lakini imefika mahali ukienda unanyimwa kuchukua leseni hizo za madini, kwa mfano, ya mawe kwa ajili ya moram au kwa ajili ya mchanga. Mtu akishachukua square kilometer 100, 200, 300 huko ndani nyie wengine wote sasa mnafanya kazi kienyeji, hamruhusiwi kupata hizo leseni. Nina uhakika kwamba hapa Bungeni tulipitisha sheria, tunashindwa kuamini kwa nini hiyo sheria haitekelezwi na huko chini kwa mfano kwenye Ofisi za Kanda wanashindwa kutupa leseni hizo za madini ya ujenzi ili watu katika Halmashauri zetu na maeneo mbalimbali waweze kuwa na fursa na haki ya kutumia hayo madini bila kubughudhiwa na huyo mwenye leseni kubwa ya utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kama alivyozungumza mwenzangu ni vizuri pia tukayaangalia haya madini aina ya chumvi, kwa sababu huyu mwenye leseni ya madini ya chumvi anatozwa sawa kabisa na yule wa dhahabu au wa madini mengine ambayo yana thamani kubwa. Kilo ya chumvi na kilo ya dhahabu ni vitu viwili tofauti, sasa kwa nini leseni zao zifanane? Kwa hiyo, mngeangalia hii leseni ya chumvi mngewaondolea kabisa au mngeweka ada ndogo tu ili chumvi yetu ambayo tunazalisha Tanzania iweze kuzalishwa kwa wingi na tushindane kwenye soko la Afrika Mashariki na Kati. Kwa hiyo, hilo naamini kabisa Wizara mtalichukulia maanani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, naomba Wizara pamoja na Wizara ya Fedha zifanye kazi kama Serikali kwa kusaidiana . Leo hii Arusha au Tanzania tungekuwa center of gemstones kwa Afrika. Jambo hili limeshindikana kwa sababu ya mifumo yetu ya kikodi kwa sababu mtu akitoka na madini katika nchi hizi ambazo zinatuzunguka kuja kuuza Tanzania anabanwa sana mipakani au kwenye viwanja vya ndege na anashindwa kuingiza mzigo wake. Vilevile kama akiingiza na hajaweza kuuza siku akitaka kuondoka na mzigo bado inakuwa ni kero na tatizo pale mipakani kutokana na mifumo yetu ya kikodi. Sasa ni vizuri tungeangalia mfumo huo ili watu wote wawe na urahisi wa kuingiza madini yao na wakitaka kuondoka na madini ambayo hawajauza waweze kuondoka nayo kiurahisi ili center ile ya Afrika ambapo ilikuwa ni Arusha wanafanya show kila mwaka iweze kukua na Tanzania iwe kama Bangkok na Brussels ili nasi kwa Afrika ndiyo tuwe kituo kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuangalie kwenye mfumo wa kodi. Leo hii tunalalamika kwa nini tanzanite au madini yetu ni mengi lakini yanauzwa kwa bei nafuu nje ya nchi. Leo hii ukitaka kuuza tanzanite nje ya nchi, uki-export officially, kihalali kabisa unalipa asilimia 5 tu ya royalty. Ukipeleka tu Kenya hapo asilimia 5 halafu ukitaka kuuza hiyo tanzanite iliyochongwa hapa nchini unatozwa asilimia 18 ya VAT, ina maana tanzanite itakuwa rahisi Kenya badala ya hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo kwenye dhahabu, bei ya dhahabu sisi hatupangi inapangwa kwenye World Market Stock Exchange, metals zote. Unakuta dhahabu yetu ukitaka kuuza hapa ni plus 18 percent locally, 18 percent kwenye VAT una-calculate pamoja na faida na gharama zote, ukipiga hesabu ni zaidi ya asilimia 25 mpaka 30. Sasa unakuta bei ya dhahabu hapa nchini locally itakuwa bei ya soko la dunia plus 25 percent. Ukienda Dubai ni asilimia 5 tu juu ya ile bei ya soko la dunia, ina maana watu wengi kwa sababu dhahabu hainunuliwi na watu wa kawaida, ni middle na upper class. Kwa hiyo, mtu anayenunua vitu vya Sh.10,000,000 ukiongeza asilimia 25 ni Sh.12,500,000, hiyo
Sh.2,500,000 inatosha kununua tiketi ya ndege kwenda Dubai, kulala five star, kufanya shopping na kurudi na unakuwa hujaingia gharama, ndiyo maana hapa biashara hiyo haikui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya dhahabu Tanzania inayochimbwa na wachimbaji wadogo ni kubwa kuliko ile ya migodi mikubwa. Sasa mgeweka tu royalty kama Dubai ilivyoweka asilimia 5, siyo lazima iwe asilimia 5, mnaweza kuweka asilimia 7/8 ili biashara ifanane. Ungekuta biashara halali ingefanyika hapa nchini na watu wengi sana wangekuwa wananunua na Serikali ingepata mapato ya kutosha na huu usonara na nini ungeweza kukua kwa sehemu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi pia tumebadilisha ile sheria kwamba haturuhusiwi kuuza madini ambayo hayajawa processed. Naomba Wizara itoe definition ya uhakika kabisa ya maana ya raw mineral kwa sababu raw mineral haijulikani, ina maana itafika mahali tutashindwa kutuma nje ya nchi madini ya aina yoyote au metal yoyote ambayo haijawa processed. Sasa ile definition mngeiweka vizuri kwa sababu hata kwenye dhahabu ya kawaida kama ni carat 24 ni ngumu, unakuta inakuwa na madini mengine ambayo yapo kidogo humo ndani. Sasa utakuta hiyo ni raw tutaanza kuingia kwenye mgogoro mwingine. Ni vizuri definition zote zikakaa vizuri ili suala hili sasa liweze kusaidia nchi yetu. Muhimu ni kwamba Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Fedha na Wizara ya Madini zikae kwa pamoja waangalie Tanzania inawezaje kuwa center ya Afrika kwenye suala hili la vito na pia kwenye jewellery na madini yote tunayo hapa gold, silver pamoja na fedha yote yanapatikana hapa nchini ili Watanzania waweze kunufaika na nchi iweze kupata kodi na mapato mengine kutokana na madini hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa hawa wachimbaji na wafanyabiashara wadogo zile gharama za leseni na ada wanazotozwa mngeangalia iwe ni fixed rate ili hata kwa mfano sonara anapoambiwa kwamba biashara hiyo wakitaka kufanya ni lazima wakate leseni ya dola 2,000, lazima awe na gemstone dealers license au gold dealers license ndiyo maana watu wanaingia kufanya biashara ya magendo. Mngeweka vitu kwa bei nafuu na isiyo na urasimu kila mtu angekuwa anafanya biashara halali na Serikali ingekuwa inapata mapato kama nchi nyingine zinavyofanya. Nchi ambayo haina hata madini ya aina moja inanufaika kuliko Tanzania ambayo tuna madini ya kila aina lakini niwapongeze Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambapo watu wanaendelea kugundua tatizo kubwa ambalo lipo na wenzangu wamelisemea ni mfano wewe unamiliki eneo lako, kwa mfano, Halmashauri yetu tuna watu ambao wana primary license hatujawahi kuwaona, hatujui wanalipa nini na wanalipia wapi, sisi hatupati hayo mapato na siku wakitaka kuanza kufanya kazi tayari wanaingia mgogoro na wanakijiji. Kwa mfano, Halmashauri ya Babati tulipotaka crusher ya mawe tulinyimwa kutokana na sheria hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante.