Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uhai ili kuendelea kuwatumikia wananchi wetu. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo ameendelea kuifanya kuhakikisha haya madini yanawanufaisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri. Hatua ambazo Mheshimiwa Rais anazichukua kwa huyu Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa uadilifu wenu tunaamini mtasimamia sekta hii muhimu ili iweze kuwanufaisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niongelee Wilaya yangu ya Kyerwa. Wilaya ya Kyerwa tuna madini ya tin, madini haya ni muhimu. Naamini Serikali ikiona na ikayasimamia yanaweza kuliingizia Taifa hili kipato kikubwa pia tunaweza tukatengeneza mabati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo napenda kulizungumzia mwaka 2016, Mheshimiwa Waziri Profesa Muhongo alifika pale na akajionea mazingira yalivyo. Maeneo yale bado utafiti haujafanyika kuweza kubainisha yale maeneo ambayo yana madini ya bati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine Wizara hii imechukua muda mrefu, tangu 2016 walikuja wataalam mara moja na hawajarudi tena. Nimwombe Mheshimiwa Waziri atueleze hatua hizi zitachukuliwa lini ili tuweze kujua ni kiasi gani cha madini tuliyonayo kwa sababu mpaka sasa hivi uchimbaji unaoendelea, wachimbaji wadogo wadogo wanachimba lakini sehemu kubwa ya madini yetu Mheshimiwa Waziri naamini anajua hatuyafaidi bali yanawafaidisha majirani zetu. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri pawepo na mkakati na hatua za haraka ili kuweza kunusuru haya madini ambayo ni ya muhimu yasiende kuwanufaisha majirani zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wachimbaji wadogo wadogo, naishukuru Serikali angalau imeweza kuwatengea maeneo lakini siyo wote, bado wanapata usumbufu sana wanapofanya utafiti wao wakapata sehemu ambayo ina madini wanakuja hawa watu ambao ni wakubwa wanasema haya maeneo ni yetu. Hivyo, wanataabika, bado hawajatengewa maeneo ambayo yataweza kuwasaidia. Niwaombe Serikali, Mheshimiwa Kairuki naamini wewe pamoja na wasaidizi wako ni wasikivu, mtakapokuja kupima yale maeneo ili kujua ambayo yana madini muweze kuwatengea wachimbaji wadogo wadogo ili wawe na uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuna wawekezaji ambao walifika pale wamekuja kujenga viwanda vya uchenjuaji. Kuna mmoja ambaye alikuwa hajafuata taratibu Serikali imemsimamisha ili aweze kufuata utaratibu. Niiombe Serikali huyu mwekezaji anapokuja na ninyi muweze kumsaidia haraka ili hawa wachimbaji wetu waweze kupata uhakika wa kuchenjua hayo madini wanayochimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wale wachimbaji wanapochimba hawana uhakika wa soko, wale ambao wana leseni ya maeneo yale ndiyo wanaochukua yale madini. Wanachukua kwa pesa ni ndogo kwa hiyo wachimbaji wadogo hawapati pesa ambayo inalingana na thamani ya yale madini. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri tuwe na uhakika wa soko na haya madini yatambuliwe. Majirani zetu ndiyo wanayatumia sana lakini sehemu kubwa inatoka kwetu. Tuweke mkakati ambao utaweza kuyatambua haya madini na ikiwezekana tuyatangaze. Bado tunaweza kufungua viwanda ambavyo vinaweza kukusanya madini haya na yakatunufaisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka kujua hii STAMICO ndiyo iliyokuwepo kipindi kile madini haya yanaibiwa na kupotea hovyo. Je, STAMICO hii ambayo mnaendelea nayo na naona mnatenga hela kwa ajili ya kuiendeleza, ni STAMICO mpya au ni ile ya zamani? Inawezekana hawa watendaji bado ni walewale. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri lazima achukue hatua, kama tunataka kubadilika lazima tubadilishe mfumo wote vinginevyo huku juu mtachukua hatua lakini bado wale wale wanaendelea kufanya uharibifu uliokuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, Mwenyezi Mungu ametujaalia madini mengi sana na ninaamini tukiyasimamia tunaweza kuliingizia Taifa kipato kikubwa sana. Kwa hiyo, niombe sana, hawa wanaosema sijui haya madini yana mapepo, majini na vitu vingine, mimi naamini hilo halipo. Hatuhitaji kwenda kwa waganga, hii rasilimali tumepewa na Mwenyezi Mungu tuisimamie, tuwapate watu ambao ni wazuri kwa msaada wa Mungu aliyetupa rasilimali hizi zitaweza kunufaisha Taifa letu. Ashukuriwe Mungu ametupatia Mheshimiwa John Pombe Magufuli ambaye ameanza kusimama vizuri na ametupa Mawaziri wazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi niwatakie kila la kheri Waheshimiwa Mawaziri, Watendaji Wakuu wote wa Wizara lakini hii ni vita lazima tupambane kuhakikisha madini haya yanawanufaisha Watanzania.