Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adimu ya kuweza kuchangia sekta hii ambayo inaonekana ina manufaa makubwa kama tutachukua hatua zinazotakiwa. Nianze kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kama Waheshimiwa Wabunge waliotangulia walivyosema, amesimamia na kama hatua anazozitaka zikichukuliwa madini yataliletea Taifa hili manufaa makubwa kuliko ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri ninayemfahamu sana, pengine namfahamu kuliko watu wengi, alikuwa Msaidizi wangu na nafurahi kuona kwamba anapaa juu na Mungu ampe kila analolihitaji ili afanye kazi yake vizuri. Napenda kuwapongeza Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeanza kumshukuru Rais kwa sababu kama hatutachukua hatua madhubuti, kwa kweli hatutaenda mbali. Nasema hivyo kwa sababu ukiangalia statistics zinaonesha kwamba mifugo, kilimo na sekta nyingine zinachangia Pato la Taifa zaidi kuliko madini. Ilivyo sasa hivi, sekta ya madini inachangia kiasi cha asilimia 4 kwenye Pato la Taifa, ni ndogo sana. Projection inaonesha mwaka 2025 itachangia asilimia 10, naamini hatua hizi ambazo anazitaka Rais zikichukuliwa tutachangia zaidi hata kuliko asilimia 10 hii ambayo iko projected.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana kuongelea suala la wachimbaji wadogo. Wachimbaji hawa ndiyo kwa kweli wanao-discover au ndiyo wanaogundua madini ambayo yapo nchi hii, tunapaswa kuwathamini na kuwatambua. Ilivyo sasa wapo kwenye vikundi lakini bureaucracy inawacheleweshea hata kupata leseni. Naomba sana wapate leseni ili waweze kujiendeleza na wawe wenye fedha nyingi kuliko wengine, kuliko hao wanaotoka nje kwa sababu wanaotoka nje watapeleka mali nje bila manufaa kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vilevile Serikali, Mheshimiwa Angellah, angalia sera, kwa nini watu wanakimbiza tanzanite Nairobi, kwa nini wasitake kuuzia Manyara na Arusha, kwa nini? Lazima kwa upande wetu tukiangalia, kama Kenya inataka kuchukua tanzanite yetu hawataweka VAT na sisi tunaweka VAT. Sasa tunafanya nini, tuna mkakati gani wa kuona kwamba madini ya Tanzania hayakimbizwi nje na ni athari kubwa sana yakikimbizwa nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimepita kule kwenye maonesho na naomba Waheshimiwa Wabunge wote mkaangalie, inaonyesha kwamba ukipeleka dhahabu bila ya kuchenjua unaweza ukawa unapeleka madini mengine yenye thamani kubwa kuliko dhahabu yenyewe. Kwa sababu nilipopita kwenye stall moja kule nje wanaochimba dhahabu walionesha kwamba katika machimbo yao wamepata dhahabu, wamepata vanadium. Vanadium ni madini yenye thamani kubwa kuliko dhahabu lakini yanakwenda kuuzwa kama dhahabu. Kwa hiyo, naomba sana tukazanie hili la kuongeza thamani na kuchenjua madini ndani ya nchi ili yale yenye thamani kubwa yatakapoonekana na watu wa madini au wale wataalam waweze kutusaidia kuona kwamba kwenye migodi ile kama ni dhahabu tu au kuna madini mengine ili Tanzania isipoteze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu mwingine wa madini haya kuchenjuliwa hapa ni nini? Ajira ya vijana inakwenda nje. Ukienda India ajira nyingi za Wahindi kama Jaipur inatokana na tanzanite. Ingekuwa imebaki pale Mererani wananchi wa Manyara, Arusha na Watanzania kwa ujumla wengi wangeajiriwa pale badala yake tunawapa ajira Wahindi. Naomba tuangalie sana hizi sera ambazo zinaweza zikawa zinachangia madini yakimbizwe nje badala ya wawekezaji kuja kuchenjua madini haya na kuongezea thamani na kupata vitu mbalimbali kama pete, mikufu na mengine ambayo tunayafahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hanang au Manyara, sehemu kubwa iko chini ya Rift Valley na wanasema kwamba kule kwenye Rift Valley hakuna madini lakini tuna maeneo machache ambayo yako juu na kule kuna madini. Ukienda Hanang eneo linaloitwa Basotu kumekuwa na madini ambayo yana thamani kubwa na wako watafiti wanaoendelea kufanya kazi kule. Naomba watafiti wasisumbuliwe badala yake wapewe incentive waweze kufanya utafiti unaotakiwa na baadaye tujue Hanang ina nini nasi tuungane na Lake Victoria ambako wanatoa dhahabu kwa sababu inawezekana mwamba ule umetoka kule ukafikia mpaka kwetu au ulitoka kwetu kwenda kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena kutoa shukrani zangu za dhati, naomba wawekezaji kutoka nje waone kwamba Tanzania siyo shamba la bibi, Tanzania ni nchi ambayo inastahili kupata manufaa ya rasilimali zake na tuna bahati Watanzania tuna rasilimali nyingi za madini, ardhi, mifugo au mambo mengine Mwenyezi Mungu ametupendelea lakini sisi wenyewe hatujipendi. Naomba tujipende ili tulinde rasilimali hizi kama Mheshimiwa Rais wetu anavyotuonesha na Mungu ampe maisha marefu na afya njema ili haya ambayo Mwenyezi Mungu ametupa Watanzania wanufaike nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ambayo sijaitegemea, nawe Mungu akupe afya njema.