Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami kuchangia Wizara hii ya Madini. Awali ya yote, nichukue fursa hii kumpa pole Mheshimiwa Spika na wananchi wa Buyungu pamoja na Viongozi wa CHADEMA kwa kupoteza mwakilishi hapa Bungeni, mwakilishi makini na mahiri. Mwenyenzi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze mchango wangu kwa kuwataka Mawaziri wote watatu wazingatie sana ushauri uliotolewa na Kamati na Nishati na Madini kwani umesheheni mambo muhimu sana. Yapo mambo kumi na moja nimeyaona pale ni muhimu sana, kama kweli dhamira ni kuiondoa nchi hapa ilipo kuelekea kwenye uchumi wa kati basi huu ushauri uzingatiwe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nijikite kwenye shughuli za utafiti wa madini kama mchangiaji aliyepita amesema kwamba hii tasnia ya madini elimu yake bado ni ndogo sana. Hawa watafiti wa madini wanapoingia kwenye Halmashuri zetu elimu haipo yaani wananchi wanashindwa kujua mipaka ya watafiti ni ipi na wao wananufaikaje, kwa sababu mwisho wa siku wanaachiwa mashimo au mahandaki. Wanakijiji wanakuwa bado hawaelewi ni kwa namna gani wanaweza kufaidika na hizi shughuli za utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitolee mfano katika Kijiji cha Lilombe, kuna machimbo ya muda mrefu sana, yale machimbo yana zaidi ya miaka kumi, kuna madini ya sapphire na dhahabu lakini mpaka leo wananchi wa kijiji kile hawaelewi chochote zaidi na kuambulia mashimo. Nilikwenda kwa Mheshimiwa Waziri kumuulizia akaniambia kwamba ameshindwa kuweka mtu katika Mji wa Liwale kufungua soko pale ili na sisi tupate kunufaika na uwepo wa madini, wakasema yale madini pale wachimbaji wale ni wachache, halafu madini yenyewe siyo mengi kwa hiyo hakuna haja ya kuweka Kamishna pale wa Madini. Jambo hili niungane na mchangiaji mmoja alisema kwamba kuwepo na watu kwenye Halmashauri zetu wanaoshughulika na mambo ya madini iwe ni kwa ajili ya kutoa elimu watu wakajua mahali ambapo madini yanapopatikana wao wanawajibika vipi na kusaidia hawa wachimbaji wadogowadogo ambao wanahangaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kutoka Liwale kwenda Tunduru ambako ndiyo kuna soko, kuna umbali wa zaidi ya kilomita 200, mtu anachukua madini kutoka Liwale mpaka Tunduru akaenda kuuza kwa hiyo wanaonufaika na ushuru na mambo mengine ni wale walioko kule, je, kule ambako kuna mashimo kunaachwa nini. Kwa hiyo, jambo hili nalo lifanyiwe marekebisho ili tuone kwamba kuna umuhimu Halmashauri zetu kuwepo na watu wanaoshughulika na mambo ya madini katika kutoa elimu pamoja na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba Sheria ya Madini ifanyiwe marekebisho hasa kwenye madini haya kama mchanga, kokoto na mawe. Panapotokea ujenzi wa barabara kumetuletea migogoro sana na hasa hasa gharama kubwa ya ujenzi wa barabara inatokana na kodi za madini. Ili kujenga barabara unatakiwa upate kifusi, kokoto lakini zenyewe unakwenda kuzilipia.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta mkandarasi anatenda ile barabara aki-include gharama hizo. Sasa barabara inayojengwa ni Serikali, hayo madini ya Serikali, ifike wakati Serikali iangallie namna ya kurekebisha hii sheria labda kuwa na exemption kwamba kwenye madini ambayo yanakwenda kufanya kazi za kiserikali basi kuwe na exemption yasitozwe kodi na kama yanatozwa kodi basi iwe ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba niongelee Ofisi ya Madini Kanda ya Kusini ambayo iko Tunduru na wamejenga tawi lao pale Nachingwea lakini bado upatikanaji wa leseni ni mgumu sana hasa kwa wale wachimbaji wadogo wanaotoka kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Liwale. Ni mgumu kwa sababu ni lazima waende Nachingwea wakapate hiyo leseni. Hata vile wanaporudi na hizo leseni soko nalo linawapa shida vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee suala la uwepo wa madini. Jana nimezungukia kwenye mabanda yale kule nyuma, nimekuta kule kwetu katika Wilaya Liwale na Ruangwa kuna hiyo wanaita green garnet na nikaambiwa haya madini thamani yake ni mara kumi ya tanzanite. Sasa nataka nijue Wizara kupitia kile Kitengo cha Utafiti wa Madini wameyatangaza kwa kiwango gani na mkakati upi umewekezwa kutafuta wawekezaji ili upande wa Kusini uchumi wetu ukaimarika kwa sababu ya upatikanaji wa hayo madini ambayo yameonekana kwamba yenyewe yana thamani kubwa kuliko tanzanite.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli napata ukakasi kidogo, nimesoma kwenye kitabu kile cha Mheshimiwa Waziri kuhusu ukusanyaji wa maduhuli kwenye bajeti ya mwaka 2017/2018 inaonyesha kama maduhuli yameongezeka, imekusanya maduhuli zaidi ya asilimia 103 lakini sasa unakuja kwenye fedha za maendeleo zimekwenda asilimia 0.8. Nashindwa kuelewa inawezekana vipi ng’ombe huyo ambaye unaona ametoa maziwa ya kutosha ndiyo anayenyimwa malisho, tunadhamiria nini, mwisho wa siku tunataka kwenda wapi? Kama Wizara inaweza kukusanya maduhuli ikapindukia lakini kwenye fedha za maendeleo wakawa hawapewi fedha. Bado sijapata ufahamu vizuri tunakwenda wapi, yaani dhamira yetu ni ipi katika hilo.