Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya na kunipa fursa ya kuchangia siku ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa John Pombe Magufuli, Rais wetu ambaye ameamua kuleta mapinduzi kwenye sekta hii ya madini. Tunampongeza kuanzisha Wizara kamili ya Madini na Wizara ya Nishati. Kote sasa tunapata ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze wote, Waziri Mheshimiwa Angellah Kairuki, Naibu Mawaziri Mheshimiwa Nyongo na Mheshimiwa Doto pamoja na wataalam wote wa Wizara kwa kazi kubwa wanayofanya. Pia pongezi kubwa kwa Prof. Kikula kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Madini pamoja na team nzima ya Tume hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuchangia kwanza kwa kushauri Kituo cha Mafunzo cha Arusha (TGC), kiwezeshwe sana kwa vifaa vya kufundishia. Wanahitaji mashine 100 za kufundishia na sasa wanazo 45 tu. Pia nipongeze kwa kuwa na mitaala ya kufundishia kozi ya Diploma itakayoanza Agosti, 2018. Nashauri kuwe na short course (Certificate in Lapidary) ya kuchonga vito. Ni kozi ya miezi sita kote duniani, wala haihitaji msomi, hata mtu asiyejua kusoma, anaweza kuwa mchongaji mzuri. Tukiwa na mashine 100 za mafunzo, tunaweza kuzalisha wataalam mia 400 kwa miaka miwili.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nashauri pia kwenye leseni za utafiti (Prospecting License) au leseni kubwa, paruhusiwe kuwa na leseni za madini ya ujenzi kama mchanga, mawe, moramu na marumaru. Kwa sasa pamoja na kuwa tulirekebisha sheria kuruhusu kuwepo leseni hizo haifuatwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, nashauri katika madini ya chumvi, Serikali iangalie namna ya kupunguza kama siyo kuondoa kodi, tozo na ada kubwa wanatozwa tofauti na thamani ya madini hayo. Leo hii wanatozwa sawa na madini yenye thamani kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, nashauri Wizara itupe tafsiri ya neno “raw mineral” leo hii kila mtaalam ana tafsiri yake ili wakati wa ku-export madini suala la kisheria ya kodi lisilete tatizo. Pia naomba nishauri Serikali ikae kama Serikali moja na siyo Wizara ya Madini tu, kufanya juhudi za pamoja ya kuboresha mazingira ya kufanya Tanzania hususan Arusha kuwa kitovu cha ubora katika biashara ya vito Afrika. Tayari tulianza vizuri na tulianza kuwa maarufu lakini sera za kikodi na usumbufu mwingine ulifanya tupoteze sifa na kudorora kwa biashara hiyo Arusha na Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi zilizotuzunguka pamoja na zingine nje ya hapo wenye madini mengi walishaanza kuzoea kuja Tanzania kuuza madini yao katika mnada wetu. Walikuwa wanakumbana na usumbufu wa TRA kwenye ushuru wa import duty, VAT na pia madini ambayo hayakuuzwa ilikuwa ni usumbufu kurudisha kwao. Tofauti na nchi zingine kama Thailand, Belgium, India na kadhalika ambazo hawatozi kodi ya import na VAT. Pia wananufaika kutokana na biashara hizo katika sekta zingine kama katika service industry, hoteli, chakula, usafiri na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie namna ya kuondoa VAT kwenye madini yanayouzwa ndani ya nchi kama dhahabu, fedha, vito ili biashara hii ikue na magendo katika madini yaishe. Sisi kama Tanzania hatupangi bei ya madini kama dhahabu na fedha pamoja na vito (VAT on local sales of gemstone and jewellery), leo hii Dubai inatoza 5% ya mrabaha kwenye dhahabu, Tanzania ni asilimia 18 VAT pamoja na ada na tozo zingine. Nashauri tuweke mrabaha wa hata 7% ili biashara ihalalishwe na Serikali ipate mapato na madini yetu yasitoroshwe.